Kwa ufupi
Alisema Serikali imeshindwa kutekeleza ilani yake ikiwamo kuwapatia maisha bora wananchi.
Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi 
(CUF), Profesa Ibrahim Lipumba ametupa kombora kwa Serikali ya Chama Cha
 Mapinduzi (CCM), akisema imeshindwa kutekeleza ahadi zake na badala 
yake inatumia vyombo vya dola kuwakandamiza na kuwaumiza wananchi.
Lipumba pia aliishutumu Serikali kwa kuwakumbatia 
viongozi ambao wanatuhuma za ubadhilifu kwa kuwahamisha katika vituo 
vyao vya kazi, hivyo kuendelea kuzorotesha uchumi wa nchi na kusababisha
 hali ya ugumu wa maisha kwa wananchi.
Aliyasema hayo jana wakati akifugua mkutano wa 
Baraza Kuu la chama hicho, Dar es Salaam, ambapo alisisitiza kuwa 
ubadhilifu ambao unakumbatiwa na Serikali hiyo umedhihirishwa pia na 
Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mtaa (LAAC)ambayo imebaini 
kuwapo mtandao unaohusisha viongozi wa Serikali wanaotafuna fedha za 
umma.
“Hii ni Serikali ya kisanii sana maana kila inachokisema haitekelezi kwa mfano kule Mtwara wananchi wanaendelea kuteswa .
Alisema Serikali imeshindwa kutekeleza ilani yake ikiwamo kuwapatia maisha bora wananchi.
Profesa Lipumba pia alieleza kusikitishwa kwake na
 nguvu kubwa iliyotumika katika kumkamata Kiongozi wa Jumuiya ya Taasisi
 ya Kiislam Sheikh Issa Ponda, akidai kuwa licha ya kwamba naye kuna 
wakati huwa haungi mkono kauli zake, lakini haoni kama ni sahihi 
kumhukumu kwa kumshambulia kwa risasi.
Alisema hatua yake ya kuzungumzia mara kwa mara 
suala la Sheikh Ponda haimaanishi kuwa anafanya hivyo kwa kuwa ni 
Mwislamu mwenzake, bali anafanya hivyo kwa kutambua ni wajibu wake 
kutetea haki kwa wananchi wote.
Alisema ni wajibu wake kukemea na kulaani vitendo 
kama hivyo akisema vilianza kwa Mwandishi wa Habari wa Channel Ten, 
Mwangosi, vikafuata kwa Ponda na kwamba kesho vinaweza kumkuta yeye.
Kuhusu mchakato wa maoni kwenye Katiba Mpya, 
Profesa Lipumba, alikosoa akisema kuwa baadhi ya vipengele havijafafanua
 bayana kuhusu muundo wa Serikali na namna inavyoweza kujiendesha.