Aliyekuwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Bukoba, Hamis Kaputa ambaye uhamisho
 wake unahusishwa na mgogoro wa madiwani akitoa ufafanuzi katika Baraza 
la Madiwani mjini Bukoba. Katikati ni Meya wa Manispaa ya Bukoba, Dk 
Anatory Amani na Naibu Meya Alexander Ngalinda.   Picha na Phinias 
Bashaya
 
            
Kwa ufupi
Mgogoro huo wa kisiasa ni  wa muda mrefu. Kwa 
upande mmoja unamhusisha Menya, Dk Anatory Amani na badhi ya madiwani na
 upande wa pili yupo Mbunge, Balozi Khamis Kagasheni na kundi jingine la
 madiwani. Wote wanatuhumiana kwa mambo mbalimbali, lakini nyuma ya 
pazia inadaiwa ni mbio za uchaguzi mwaka 2015
Keshokutwa hatima ya madiwani wanane wa Chama Cha Mapinduzi (CCM)  waliotimuliwa itajulikana mjini Dodoma.
Mgogoro huu ulianza kama mchicha sasa umekua na 
kugeuka mbuyu. Ulianza kama tishio la chama hicho mkoani Kagera pekee na
 Baraza la Madiwani la manispaa ya Bukoba, leo umekomaa hadi unajadiliwa
 na Kamati Kuu ya CCM inayokutana Ijumaa.
Hatua ya CCM mkoa kuwatimua madiwani hao ni 
jaribio la kwanza kwa chama ngazi ya mkoa kufikia uamuzi mgumu tangu 
ilipotangazwa sera yake ya kujivua gamba.
Mgogoro huo dhidi ya Meya Dk Anatory Amani si 
habari mpya, umevuma kwa zaidi ya mwaka mmoja. Nyuma yake kuna kivuli 
cha mbunge wa Bukoba, mjini Balozi Khamis Kagasheki anayeunga mkono 
tuhuma za ufisadi dhidi ya meya.
Upepo wa kisiasa usingebadilika ghafla hivi, kama 
Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete asingefanya ziara mkoani hapa 
hivi karibuni na kushauri tofauti zilizopo baina ya makundi hayo 
zimalizwe.
Rais Kikwete wakati akihitimisha ziara yake 
alisema lazima soko jipya lijengwe, mpango unaopingwa kwa nguvu zote na 
madiwani waliotimuliwa.
Kauli hiyo ilionekana kutoa ushindi kwa upande wa pili na hivyo madiwani hao wakajipanga kulipa kisasi.
Kwa vyovyote vile kundi hili haliwezi kukubali 
mradi wa kujenga soko jipya kwani wengi wao wanamiliki idadi kubwa ya 
vibanda sokoni ambavyo huvikodisha kwa wafanyabiashara wengine.
Kabla Rais Kikwete hajatua Dar es Salaam, madiwani
 waliandika barua ya kumtaka Mkurugenzi wa Manispaa kuitisha kikao cha 
kupiga kura ya kutokuwa na imani na Meya. Kauli ya Kikwete ilionekana 
kuwa tofauti na matarajio yao.
Madiwani walitaka kumwonyesha Mwenyekiti wao kuwa 
upo wakati sikio linaweza kuzidi kichwa. Maelekezo yaliyotolewa na 
Mwenyekiti wao jinsi ya kumaliza mgogoro huo yalipuuzwa. Katika hatua 
hii pia walifanikiwa kumnasa Diwani wa Kata ya Bakoba, Felician Bigambo 
(Cuf).
Kabla ya kuhamia kundi hili, Bigambo alikuwa 
mstari wa mbele kutetea miradi waliyoibua. Alitoa ushahidi mbele ya Tume
 ya Abbas Kandoro jinsi madiwani walivyoshiriki hatua zote za vikao vya 
uamuzi. Ghafla alijiunga na kundi la madiwani wa CCM ili awasaidie 
kulipa kisasi dhidi ya matamshi ya Rais Kikwete.
Mwanzoni mwa mgogoro huu,Taasisi ya Kuzuia na 
Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Kagera ilithibitisha kuwahoji 
baadhi ya madiwani waliotimuliwa kwa tuhuma ya kupokea rushwa. Tangu 
wakati huo ukweli wa tuhuma hizo umebaki kuwa siri ya Takukuru
Vioja vya Madiwani
Madai ya madiwani hao yameambatana na vituko 
kadhaa zikiwamo tuhuma za kunyang’anywa simu na kufungiwa eneo moja ili 
wasipatikane wakati wa vikao vya Baraza. Ni mpango wa kumkomoa Meya wao,
 ili kukwamisha vikao baada ya akidi kupungua.
Hii ni dhambi inayowatafuna, kwani madiwani wale 
wale waliwekwa ‘mateka’ wilayani Chato ili kufanikisha mpango wa 
kumng’oa meya wa zamani, Samwel Ruhangisa kwa hofu kuwa wangerubuniwa. 
Diwani huyo wa zamani amejiunga na kundi la kumpinga meya wa sasa.
Kwa mwaka mzima madiwani wamegomea vikao hata 
walipofika ilikuwa kwa ajili ya kushinikiza ajenda yao ya kumng’oa Meya.
 Waligoma hata kujadili bajeti ya Manispaa ambayo ndiyo msingi wa 
kufanikisha shughuli za maendeleo ya wananchi wanaowawakilisha.
Miezi michache iliyopita madiwani hao walikwenda 
Dodoma kupeleka mashtaka yao kwa Waziri Mkuu dhidi ya Meya wao. 
Waliondoka kwa mbwembwe, ingawa walirejea kwa mafungu baada ya lengo lao
 kukwama.
Ni madiwani walewale walioibua madai kuwa hawakuwa
 na imani na Tume iliyoundwa na Waziri Mkuu kuchunguza tuhuma dhidi ya 
meya, wakidai kiongozi wa Tume hiyo  Abbas Kandoro alionekana 
akizungumza na mtuhumiwa.
Wakurugenzi wawili wang’oka
Katika mgogoro huu hata watumishi wa Manispaa ya 
Bukoba hawako salama. Wako makini kwa kauli na vitendo ili wasituhumiwe 
kuunga mkono moja ya makundi yanayopingana.
Tayari wakurugenzi wawili wameng’olewa kwa sababu 
za kisiasa zaidi kuliko utendaji wao wa kazi. Mkurugenzi aliyekuwepo 
wakati mgogoro unaanza, Hamis Kaputa alihamishwa ghafla baada ya moja ya
 pande zenye mgogoro kupoteza imani naye.
 Mkurugenzi aliyechukua nafasi yake, Trazias 
Kagenzi akitokea wilaya ya Arumeru, mkoani Arusha naye alikaa majuma 
mawili na baadaye kuondolewa ili kuridhisha moja ya upande wenye 
mgogoro.
Kilichomponza Mkurugenzi huyo ni kuwa baada ya 
uchunguzi wa madiwani ilionekana Mkurugenzi mpya alikuwa amesoma darasa 
moja na Meya, Dk Amani na kujenga hisia kuwa utendaji wake ungependelea 
upande mmoja.
Sasa kuna Mkurugenzi mpya Limbakisi Shimwela 
ambaye hofu ya kuogopa makundi yenye mgogoro inasomeka vyema usoni 
mwake. Hataki kuzungumza lolote kuhusu miradi ya Manispaa hadi hapo hali
 ya hewa itakapotulia.
souce: Mwananchi
Dar es Salaam. Polisi Makao Makuu Kitengo cha Makosa ya Jinai 
Rasimali Watu, juzi ilimhoji Amir Mkuu wa Jumuiya ya Taasisi za 
Kiislamu, Sheikh Mussa Kundecha kwa kile walichodai kuwa mtu huyo ni 
rafiki mkubwa wa Sheikh Kondo Bungo anayetafutwa polisi.
Taarifa kutoka kwenye vyanzo vya polisi Makao 
Makuu zilieleza kuwa Bungo anatafutwa na polisi kwa kile walichodai 
alitoa maneno ya uchochezi katika Mkutano wa Waislamu uliofanyika 
Viwanja vya Mwembeyanga wilayani Temeke, mwishoni mwa wiki iliyopita.
Kamishna Msaidizi wa Jeshi la Polisi, Advocate 
Nyombi, kutoka Kitengo cha Upelelezi Makao Makuu alipotafutwa jana 
kuzungumzia suala hilo, simu yake ilikuwa haipatikani.
Chanzo chetu kilidokezwa kuwa baada ya mkutano huo
 ambao pia ulihudhuriwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke, Engelbert 
Kiondo, Polisi walipanga kumkamata Bungo kwa wakati maalumu na siyo eneo
 lile ili kuepusha vurugu ambazo zingeweza kutokea endapo angetiwa 
nguvuni.
“Kundecha aliitwa jana (juzi) na kuhojiwa kwa saa 
kadhaa na kumtaka amlete Bungo ambaye ni mtu wake wa karibu, “ alisema 
mtoa habari huyo kuongeza kuwa: “Asipofanya hivyo kwa muda aliopangiwa 
basi atakamatwa yeye hadi hapo atakapo patikana Bungo.”
Katika hatua nyingine, Polisi Kanda Maalumu 
inamshikilia Profesa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaa m Kitengo cha 
Utafiti wa Mimea kwa tuhuma za kumjeruhi kwa risasi fundi ujenzi, 
Fadhili Mkachino.
Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, 
Kamishna Suleiman Kova alisema jana kuwa tukio hilo lilitokea juzi saa 
10 alasiri maeneo ya SalaSala Benako wilayani Kinondoni.
Alisema Mkachino akiwa na mafundi wenzake 
wakijenga nyumba moja ya Khadija, ndipo profesa huyo alitokea na 
kuwataka kusisitisha mpango huo mara moja kwa kile alichodai ni eneo 
lake.
“Kabla ya mafundi hao hawajafanya chochote ghafla 
Profesa huyo alitoa bastola na kumpiga risasi mbili tumboni Mkachino 
ambaye alikuwa kiongozi wa mafundi hao na kumsababishia maumivu makali,”
 alisema Kamishna Kova.
Kova alisema kitendo cha kumpiga risasi mtu ni 
kosa la jinai na kwamba ni jambo lisilokubalika katika jamii. Alitoa 
wito kwa wenye silaha kuwa wavumilivu wakati wote.
souce: Mwananchi