Saturday, 7 September 2013

Msikiti wa Manyema Dodoma wateketea


Na Rachel Chibwete na Masoud Masasi, Mwananchi

Posted  Septemba7  2013  saa 11:38 AM
Kwa ufupi
Moto huo ulianza saa 8 mchana baada ya swala ya Ijumaa hatua ambayo ilileta taharuki kwa waumini waliokuwapo ndani ya msikiti huo.


Dodoma. Moto mkubwa umezuka jana kwenye Msikiti wa Manyema uliopo Barabara ya Saba katika Manispaa ya Dodoma na kusababisha uharibifu mkubwa wa mali pamoja na jengo hilo.
Moto huo ulianza saa 8 mchana baada ya swala ya Ijumaa hatua ambayo ilileta taharuki kwa waumini waliokuwapo ndani ya msikiti huo.
Mmoja wa mashuhuda wa tukio hilo, Juma Mohamed alisema walianza kuona moshi mzito ukitoka ndani ya jengo la ghorofa ya pili ya msikiti huo na baadaye moto mkubwa ulizuka.
“Baada ya kuona moto huo, tuliwasiliana na Kikosi cha Zimamoto ambao walifika katika eneo la tukio na kuuthibiti moto huo japo kuna uharibifu wa mali uliotokea,” alisema Mohamed.
Shuhuda mwingine Sauda Ally alisema, alikuwa nje ya duka lake lililopo karibu na msikiti huo na kushuhudia moto mkubwa ukiwa unawake kwenye ghorofa ya pili ya jengo hilo hali iliyowafanya kufunga maduka yao.
Mmoja wa maofisa wa polisi aliyefika katika tukio hilo alisema, bado hawajua chanzo halisi cha moto huo japo kwa taarifa za awali zinaonyesha kuwa ulisababishwa na hitilafu ya umeme.
“Sisi baada ya kupata taarifa hizo tuliwasiliana na wenzetu wa Kikosi cha Zimamoto na Tanesco kwa ajili ya kuuzima moto huu,” alisema ofisa huyo. Kaimu Kamanda wa Polisi Suzan Kaganda, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo.
source: Mwananchi