Kutoka kushoto ni Rais Paul Kagame wa Rwanda, Rais Yoweri Museveni wa 
Uganda na Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta. Picha ya Maktaba. 
            
    Na Zacharia Osanga, Mwananchi
Posted Alhamisi,Septemba5 2013 saa 12:28 PM
Posted Alhamisi,Septemba5 2013 saa 12:28 PM
Kwa ufupi
Rais Jakaya Kikwete naye ana mipango ya kujenge reli kutokaTanzania Rwanda- Burundi mpaka DRC.
Wiki iliyopita Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta, 
Rais wa Uganda, Yoweri Museveni na Rais wa Rwanda, Paul Kagame 
walikutana Mombasa nchini Kenya na kuzindua mradi mkubwa wa ujenzi wa 
reli.
Katika uzinduzi huo marais hao wameweka muda wa 
kuanza kwa miradi mitatu mikubwa. Mosi kuanza kwa mradi wa ujenzi wa 
reli kutoka Mombasa-Kampala mpaka Kigali, ujenzi wa bomba la mafuta 
kutoka Eldoret-Kampala mpaka Kigali na kujenga miundombinu ya umeme wa 
uhakika.
Pia wamewaagiza mawaziri wa fedha wa nchi hizo 
kuandaa mapendekezo ya utekelezaji wa miradi hiyo mitatu na taarifa ya 
mapendekezo hayo wanatakiwa kuitoa kwa marais hao katika mkutano ujao.
Wanazungumza lugha moja
Kwa mujibu wa mratibu wa miradi hiyo, Monique 
Mukaruliza, ujenzi wa bomba la kusafisha mafuta kutoka Eldoret-Kampala 
mpaka Kigali, unatarajiwa kukamilika 2017 huku  kabla ya mwisho mwa 
mwaka huu, viongozi wa  nchi hizo wamekubaliana kuzindua ushuru wa 
pamoja wa forodha kwa ajili ya kusafirisha bidhaa kwa masharti nafuu 
kutoka nchi moja hadi nyingine.
Wakati hayo yakiendelea, taarifa zinaeleza kwamba 
ujenzi wa reli hiyo utagharimu Dola 3.5 bilioni, lakini taarifa nyingine
 zinasema kwamba mradi huo una thamani ya Dola 13 bilioni na mradi huo 
utakamilika mwaka 2018 huku ujenzi wa awali wa mradi wa reli kutoka 
Mombasa mpaka jijini Nairobi unatarajiwa kuanza Novemba, mwaka huu.
Vilevile kuanzia Januari mwakani,  Rais wa Kenya, 
Kenyatta na Kagame wamekubaliana kwamba wananchi wao waanze kutumia 
vitambulisho vya uraia kusafiria katika nchi hizo wakati Uganda itatumia
 kadi ya kupiga kura kusafiri Kenya na Rwanda.
Mbali na hayo taarifa iliyotolewa hivi karibuni 
imebainisha kwamba katika mkutano wa pili uliofanyika Mombasa wiki 
iliyopita, marais hao waliwaagiza mawaziri wa fedha wa nchi hizo kuandaa
 mapandekezo ya utekelezaji wa miradi hiyo ndani ya mwezi mmoja na nusu 
ujao.
Wataalamu wa masuala ya uchumi, wanabainisha 
kwamba reli hiyo itakuwa na uwezo wa kubeba mizigo na kwenda kilometa 80
 kwa saa wakati itakapoanza kusafirisha mizigo katika ukanda huo.
Bandari ya Mombasa, inategemewa kwa zaidi ya 
asilimia 50 na Rwanda katika kuagiza mizigo huku ikitegemewa na Uganda, 
Mashariki mwa Demokrasia ya Kongo (DRC), Burundi, Kaskazini mwa mikoa ya
 Tanzania na Sudani Kusini.
Burundi na Sudani Kusini
Katika mkutano huo marasi wa nchi hizo tatu 
walikubali kuijumuisha Burundi na Sudani Kusini katika miradi hiyo baada
 ya kuhudhuria mkutano huo kama wageni waalikwa.
Kutokana na makubaliano hayo ni dhahiri kwamba nchi hizo tano 
zimekubaliana kufanya kazi pamoja katika utekelezaji wa miradi hiyo kwa 
lengo la kuboresha maisha ya wananchi wa nchi hizo kiuchumi.
“Wawakilishi wa Burundi na Sudani Kusini wanapaswa
 kuwa sehemu ya miradi hiyo na hasa katika kamati za ufundi,” inaeleza 
sehemu taarifa ya mkutano huo.
Mukaruliza anabainisha kwamba Burundi na Sudani 
Kusini walialikwa kwenye mkutano huo kama watamazaji na baadaye waliomba
 kuwa sehemu ya kuanzisha miradi hiyo.
Katika mkutano huo Rais Kenyatta alitoa taarifa ya
 maendeleo ya miradi hiyo baada ya mkutano uliofanyika  Entebbe, Juni 
mwaka huu.
 “Ninayo furaha kutoa taarifa ya mradi wa bomba la
 mafuta na katika hatua ya kwanza ya maendeleo ya mradi wa bomba la 
mafuta, unaendelea vizuri na hatua ya awali tayari imeanza na upembuzi 
yakinifu umekamilika,” anasema Rais Kenyatta.
Pia Kenyatta anasema kuna changamoto zinazokabili 
nchi hizo na kwamba wanapaswa kuungana pamoja kwa ajili ya kuzitatua na 
kufikia malengo yaliyokusudiwa.
Kuhusu hati za kuruhusu watu wa Jumuia ya Afrika 
Mashariki kuingia katika nchi moja hadi nyingine, katika mkutano huo 
suala hilo lilijadiliwa na mawaziri husika waliagizwa kutoa taarifa kwa 
nchi ya Kenya, Rwanda na Uganda katika mkutano wa tatu utakaofanyika 
Oktoba mwaka huu ili mpango huo uanze Januari mosi, mwakani.
Vilevile mawaziri husika wameagizwa kukamilisha 
mchakato wa kutumia vitambulisho vya uraia kabla ya Oktoba, mwaka huu 
ili vitumike kama hati rasmi kusafiria katika nchi hizo Januari mosi, 
mwaka huu.
Katika mkutano huo, Rais wa Sudani Kusini, Salva 
Kiir Mayardit aliwakilishwa na waziri wake wa masuala nje Dk Barnaba 
Marial Benjamin wakati waziri wa usafirishaji wa Burundi, Deogratias 
Rurimunzu alimwakilisha  Rais Pierre Nkurunziza.
Mkutano mwingine utafanyika Oktoba mwaka huu jijini Kigali.
Tanzania
Mwishoni mwa Mei, Rais Jakaya Kikwete alipofanya 
ziara  nchini Japan aliiomba nchi hiyo kuangalia uwezekano wa kugharimia
 ujenzi wa reli mpya kutoka Tanzania kwenda nchi za Rwanda, Burundi  
mpaka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), ombi ambalo Serikali ya 
nchi hiyo ilikubali.
Rais Kikwete anasema ujenzi wa reli hiyo utarahisisha 
usafirishaji wa mizigo wa nchi hizo ambazo zinaitegemea bandari ya Dar 
es Salaam kusafirishia bidhaa zake.
Taarifa zinasema Kampuni ya Burlington Northern 
Santa Fe Railway ya Marekani ndiyo itakayofanya ukarabati huo ambao 
utahusisha ujenzi wa reli mpya kutoka Isaka hadi Kigali ambayo pia 
itaunganisha Jiji la Bujumbura, Burundi. 
Hata hivyo uzinduzi wa mradi wa reli ya 
Mombasa-Kigali, huku Rwanda na Uganda zikitishia kujitoa kutumia bandari
 ya Dar es Salaam unaacha maswali mengi.
source: Mwananchi
source: Mwananchi