Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni,Freeman Mbowe akizungumza 
kwenye kikao cha maamuzi ya pamoja  na Vyama vingine juu ya kususia 
mjadala wa Marerkebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba Bungeni  juzi 
jioni.Kushoto ni Mbunge wa Mkanyageni,Hbib Mnyaa(CUF)na Mbunge wa 
Kuteuliwa NCCR Mageuzi,James Mbatia.Picha na Fidelis Felix 
            
Kwa ufupi
Gazeti hili limefanikiwa kuona nakala inayodaiwa 
kuwa ni maoni ya awali ya kamati hiyo ambayo yalikuwa na mapendekezo 
yanayotaka kuwapo kwa marekebisho kadhaa kwenye muswada huo, tofauti na 
yale yaliyowasilishwa bungeni juzi na Mwenyekiti wa Kamati, Pindi Chana.
Dodoma. Maoni ya Kamati ya Bunge ya Katiba, 
Sheria na Utawala kuhusu Muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba wa 
2013 yanadaiwa kuwa yalibadilishwa dakika za mwisho na kwamba suala hilo
 ndicho kiini cha vurugu zilizotokea bungeni mjini Dodoma juzi.
Gazeti hili limefanikiwa kuona nakala inayodaiwa 
kuwa ni maoni ya awali ya kamati hiyo ambayo yalikuwa na mapendekezo 
yanayotaka kuwapo kwa marekebisho kadhaa kwenye muswada huo, tofauti na 
yale yaliyowasilishwa bungeni juzi na Mwenyekiti wa Kamati, Pindi Chana.
Jumatano na Alhamisi wiki hii kulikuwa na mvutano 
mkubwa bungeni kiasi cha wabunge wa upinzani kutoka vyama vitatu vya 
NCCR -Mageuzi, Chadema na CUF kuungana na kususia mjadala kuhusu muswada
 huo.
Imedokezwa kuwa mvutano mkali kuhusu muswada huo 
ulianza ndani ya kamati hiyo wakati wajumbe wake ambao ni wabunge wa CCM
 walipotumia wingi wao kubadili maoni ya awali na kuweka maoni mapya, 
hatua ambayo inadaiwa kuwa ilikuwa na msukumo wa Serikali nyuma yake.
Ndani ya Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na 
Utawala, wabunge wa upinzani ambao kwa idadi yao ni wachache walishindwa
 kuzuia mabadiliko hayo ya “lala salama” yanayodaiwa kuwa yaliwekwa 
Septemba 2, mwaka huu, hivyo waliazimia kuhamasisha wabunge wote wa 
upinzani kupinga marekebisho hayo kutokana na sababu kuu mbili.
Sababu hizo ni kutofanyika kwa mikutano ya wazi 
kwa umma (public hearing) upande wa Zanzibar na hatua ya kuwapo kwa 
mapendekezo ya Rais kurundikiwa madaraka makubwa ya uteuzi wa wabunge 
kutoka asasi za kijamii watakaoingia katika Bunge la Katiba.
Habari zinasema wakati fulani Naibu Spika wa 
Bunge, Job Ndugai alitembelea kamati hiyo wakati ikiedelea na vikao 
vyake na kukuta mvutano mkali kuhusu suala la marekebisho ya sheria ya 
sheria hiyo na alishauri kwamba pale ambapo hawataweza kuelewana basi 
wasubiri uamuzi ndani ya Bunge.
Jana gazeti hili lilimtafuta Chana kupitia simu 
yake ya mkononi na baada ya kumweleza kuhusu madai hayo alisema: 
“Tafadhali sana kwa sasa niko kwenye kikao, kwanza simu yako nimeipokea 
kwa heshima tu, tutafutane wakati mwingine”.
Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe 
alikiri kwamba kulikuwa na mapendekezo ya kuongeza idadi ya wabunge na 
namna ya kuwapata, lakini Serikali iliyakataa katika hatua ya 
majadiliano kabla ya suala hilo kufikishwa bungeni.
Tofauti ya maoni
Nakala ya taarifa ya awali ilipendekezwa kuwa 
katika kuteua wajumbe 166 wa Bunge la Katiba, Rais azingatie kikamilifu 
mtiririko wa mapendekezo ya kila kundi lililoainishwa katika kifungu cha
 (1) (c).
“Na endapo Rais hatazingatia mapendekezo ya kundi 
mojawapo, Rais afanye mrejesho kwa taarifa kwa kundi husika juu ya 
sababu za kutozingatia mtiririko wa mapendekezo yaliyowasilishwa kwake,”
 inasema taarifa hiyo.
Taarifa hiyo inaongeza kuwa kamati hiyo ilikuwa na maoni kwamba 
makundi mengine ya kijamii yaongezwe katika kifungu cha 22(1) (c) cha 
sheria mama, ili kupanua wigo wa uwakilishi mpana katika Bunge la 
Katiba, hivyo kuongeza idadi ya wabunge hao kutoka idadi ya awali 166 
hadi kufikia 201.
“Kamati inashauri kuwa idadi ya wajumbe iwe 201 
badala ya idadi ya wajumbe 166 iliyotajwa katika sheria mama, ili kupata
 idadi ya wajumbe watakaounda Bunge Maalumu la Katiba,” inasomeka 
taarifa hiyo.
Hata hivyo, maoni hayo yanatofautiana na yale 
yaliyowasilishwa bungeni juzi na jana, kwani yanaonyesha kwamba kulikuwa
 na majadiliano na mashauriano baina ya kamati na Serikali, hivyo 
ilikubaliana kuwa “Rais apewe mamlaka ya kufanya uteuzi wa wajumbe Bunge
 la Katiba” huku idadi ya wabunge wa kuteuliwa wakibaki 166.
Kifungu hicho kiliondoa haki ya kila taasisi 
kuteua jina la mjumbe wake katika Bunge hilo na badala yake, 
ikapendekezwa kuwa Rais atapelekewa matatu ili ateue moja kati ya hayo.
Hata hivyo, jana wakati Bunge lilipoketi kama 
kamati kwa ajili ya kupitia vifungu vya marekebisho ya muswada huo, 
Serikali iliwasilisha marekebisho ya nyongeza ambayo yanazitaka asasi za
 kiraia ziteue majina tisa na kati ya hayo Rais anaweza kuteua jina moja
 na kama asiporidhika anaweza kuteua mtu kutoka nje ya orodha hiyo.
Kuhusu suala hilo Chikawe alisema: “Tangu awali 
ilikuwa inaonyesha wajumbe ni 166. Ni kweli Kamati ilipendekeza wajumbe 
hao waongezeke hadi 201 lakini pendekezo hilo halikukubaliwa, ikabakia 
wajumbe watakuwa 166.”
Ushiriki wa Zanzibar
Itakumbukwa kuwa Kamati ya Katiba, Sheria na 
Utawala ilipewa wiki nne za kuendesha vikao vyake kabla ya kuanza kwa 
Mkutano wa 12 wa Bunge uliomalizika jana, tofauti na kamati nyingine 
ambazo zilipewa wiki mbili.
Baadhi ya wabunge (hasa wa upinzani) wanasema 
madhumuni ya kupewa muda huo ni kama hayakutimia kwani hawakuweza 
kupokea maoni kutoka kwa makundi muhimu hasa ya upande wa Zanzibar kama 
ilivyokusudiwa.
Hata hivyo, jana Makamu wa Pili wa Rais wa 
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), Balozi Seif Ali Idd, 
alilihakikishia Bunge kuwa upande wa Zanzibar ulishirikishwa katika 
kutoa maoni ya muswada huo.
Hatua ya Balozi Idd kutoa ufafanuzi ilitokana na 
mwongozo ulioombwa na Mbunge wa Sikonge, Said Nkumba(CCM) aliyeomba kwa 
vile Balozi Seif yuko ndani ya Bunge basi apewe fursa kufafanua utata 
huo.
Kauli ya Balozi Idd inapingana na ile iliyotolewa 
juzi jioni na Mnadhimu wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu ambaye 
alisema ni kosa kubwa kamati kutochukua maoni ya Wazanzibar.
Lissu alisema kulikuwa na njama tangu mwanzo za kuhakikisha kuwa
 Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala haichukui maoni ya 
Wazanzibari na hilo linathibitishwa na ratiba zilizokuwa zimeandaliwa na
 kamati.
“Katika orodha ya wadau wote 22 waliokuwa 
wameorodheshwa katika kutoa maoni yao juu ya muswada huu hakukuwa na 
Mzanzibari hata mmoja…tulipoipitia tukasema hapana Wazanzibari wako 
wapi,” alisema.
Lissu alisema yeye, Mwenyekiti wa Kamati, Chana na
 Makamu Mwenyekiti, William Ngeleja walikwenda kumwona Katibu wa Bunge, 
Dk Thomas Kashililah na kumweleza azma yao ya kwenda kuzungumza na wadau
 wa Zanzibar.
“Katibu akatwambia kwamba yeye ana fedha za 
kutuwezesha kukaa Zanzibar hata wiki moja, kwa hiyo tukarudi kwenye 
kamati tukatengeneza ratiba mpya na tukaongeza wadau sita wa Tanganyika 
na Wazanzibari wanane,” alisema Lissu.
Aliwataja wadau hao kuwa ni Chuo cha Taifa 
Zanzibar, Chuo Kikuu cha Zanzibar, Chama cha Mawakili Zanzibar, Chama 
cha Wanasheria Wanawake Zanzibar, Chama cha Walemavu Zanzibar na Profesa
 Abdul Shariff.
Wadau wengine walikuwa ni Shirikisho la Vyama 
visivyo vya Kiserikali Zanzibar (Angoza) na Jumuiya ya Misikiti Zanzibar
 na Jumuiya ya Maimamu Zanzibar, lakini hatukuwahi kukutana nao na 
kupokea maoni yao.
“Tukakubaliana kuwa tutakaa Zanzibar kwa siku tatu
 kuanzia Julai 14 hadi Julai 16 mpaka leo hatujawahi kuambiwa kwa nini 
tulizuiwa kwenda Zanzibar, lakini maneno yaliyokuwa yakisikika eti kwa 
sababu za kiusalama,” alisema.
Lissu alisema wakati kamati yao ikiambiwa haiwezi 
kwenda Zanzibar kwa sababu za kiusalama, wajumbe wa Kamati ya Ulinzi ya 
Bunge hilo ilikuwa Pemba ikiendelea na ziara zake.
source: Mwananchi
source: Mwananchi