Na Daniel Mjema, Mwananchi
Posted Septemba7 2013 saa 11:40 AM
Posted Septemba7 2013 saa 11:40 AM
Kwa ufupi
Dodoma. Polisi mkoani Dodoma, wanaumiza vichwa
namna ya kumpata Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi (Chadema)
wanayemtafuta kwa udi na uvumba kwa tuhuma za kumpiga Polisi wa Bunge.
Mbunge huyo kijana alifanikiwa kuwapiga chenga ya
mwili(kutoroka) polisi hao waliokuwa wametanda eneo la Bunge juzi,
mahususi kwa lengo la kumkamata lakini aliwatoroka bila wao kumtambua.
Habari za uhakika zilizopatikana jana na juzi,
zilisema tayari polisi wamesambaza taarifa ya simu ya upepo katika mikoa
ya jirani ya Morogoro na Singida ili wamkamate watakapomuona.
Polisi hao wa Bunge na makachero wengine, juzi
jioni walitanda katika Viwanja vya Bunge kwa lengo la kumkamata lakini
mavazi aliyokuwa ameyavaa mbunge huyo yakawachanganya wasimtambue.
“Unajua Polisi walikuwa wamejiandaa wakijua Sugu
(Mbilinyi) angefika jioni kipindi cha Bunge akiwa amevaa suti aliyovaa
asubuhi yake, lakini akaja na mavazi tofauti kabisa,”kilidokeza chanzo
chetu.
Sugu alifika eneo hilo la Bunge juzi saa 11:00
jioni akiwa katika gari la Kiongozi wa Upinzani Bungeni (KUB), Freeman
Mbowe na kushiriki mkutano wa wanahabari Ukumbi wa Msekwa.
Akizungumza na gazeti hili juzi kabla ya mkutano
huo na wanahabari, mbunge huyo alisema, tayari amepata taarifa ya kuwapo
maagizo ya yeye kukamatwa lakini akasema yuko tayari kutetea haki yake.
“Nimeambiwa OC-CID (mkuu wa upelelezi) ametoa
maagizo nikamatwe eti kwa kumpiga Polisi… Mimi nashangaa sana kwa sababu
mimi ndiye niliyepigwa lakini natakiwa kukamatwa,”alisema.
Haifahamiki aliwezaje kuwatoroka polisi na
kufanikiwa kuondoka lakini waliendelea kuganda viwanja vya Bunge hadi
saa 3:00 usiku wakiamini bado alikuwa ofisi za Kambi Rasmi ya Upinzani
Bungeni.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Susan
Kaganda, jana alilithibitishia gazeti hili kumsaka mbunge huyo kwa
mahojiano na kwamba tayari taarifa hiyo wameiwasilisha kwa Katibu wa
Bunge.
“Ni kweli tunamhitaji kwa ajili ya mahojiano na
kama unavyojua utaratibu unavyosema lazima uliarifu Bunge na sisi tayari
tumemuandikia katibu wa Bunge ili amtaarifu (Mbilinyi) ili aje,”alisema
Kaganda.
Juzi jioni wakati akiahirisha Bunge, Ndugai
alisema mbunge huyo amefanya vitendo vya aibu kwa kumpiga kichwa na
kumchania sare polisi mmoja wa Bunge na kuharibu kipaza sauti cha Bunge.
Wakati Ndugai akisema hivyo, jana Mbunge wa Simanjiro,
Christopher Ole Sendeka aliomba mwongozo wa Spika kuhusu Mbilinyi
kujichukulia sheria na kumpiga Polisi nje ya ukumbi.
Mwenyekiti wa Bunge, Jenister Mhagama alisema
atautolea maamuzi mwongozo huo baada ya kushauriana na Wanasheria wa
Bunge na viongozi wa taasisi nyingine zinazoshabihiana na hilo.
Kiini cha kutafutwa kwa mbunge huyo ni vurugu
zilizotokea juzi mchana ndani ya ukumbi wa Bunge baada ya Naibu Spika
,Job Ndugai kuwaamuru polisi kumtoa kwa nguvu kiongozi wa Upizani,Mbowe.
source: Mwananchi
source: Mwananchi