Tido Mhando 
            
Kwa ufupi
Tido Mhando ni miongoni mwa watangazaji wa radio 
wakongwe Afrika ya Mashariki. Tangu mwishoni miaka ya 1960, jina la Tido
 Mhando limekuwa maarufu katika kanda hii kama mtangazaji wa muziki, 
michezo na baadaye habari na matukio.
Tido Mhando ni miongoni mwa watangazaji wa radio
 wakongwe Afrika ya Mashariki. Tangu mwishoni miaka ya 1960, jina la 
Tido Mhando limekuwa maarufu katika kanda hii kama mtangazaji wa muziki,
 michezo na baadaye habari na matukio. Ndani ya simulizi zake hizi za 
kila Jumapili, Tido anasimulia baadhi tu ya mambo aliyokutana nayo 
katika kipindi chake hicho. Jumapili iliyopita aliendelea kusimulia 
kuhusu maandalizi yake ya safari ya kwenda New Zealand kwenye michezo ya
 Nchi za Jumuiya ya Madola ya 1974. Maandalizi ambayo yaliingia dosari 
kiasi wakati ilipofahamika kwamba isingewezekana kwa RTD kutuma 
watangazaji wawili kwenye michezo hiyo kama ilivyokuwa imetarajiwa. SASA
 ENDELEA…
Haikuwa rahisi kupokea kauli ile ya Naibu 
Mkurugenzi, Sammy Mdee, kwamba kwa sababu ya uhaba wa fedha imelazimika 
mimi pekee niende kwenye michezo hiyo ya New Zealand badala ya 
kuambatana na mtangazaji mwenzangu Abdul Omar Masoud.
Tulikaa kimya kwa muda, lakini hatimaye, Masoud 
alinishika mkono na kunitakia kila la kheri. Tulijaribu kutafakari 
kuhusu uamuzi huo na tukakubaliana kwamba bila ya shaka uamuzi wa 
kunichagua mimi ulitokana na ukweli ya kwamba Masoud, mbali ya mchezo wa
 mpira wa miguu, alikuwa si mzoefu sana kwenye michezo mingine kama vile
 riadha na ngumi, tofauti na mimi.
Wakati tulipokuwa tukifanya mipango ya safari kwa 
pamoja tulikuwa tumezungumza mengi, siyo tu kuhusu jinsi ambavyo 
tungetangaza michezo hiyo, bali hata ambavyo tungevinjari pamoja huko 
Christchurch. Sasa yote haya yakawa yamesukumwa pembeni. Ikanibidi 
nianze kujipanga upya mwenyewe.
Nilipobakia peke yangu, niliwaza na kumsikitikia 
mwenzangu Masoud. Nilifahamu ni kwa jinsi gani tungeweza kuusisimua umma
 wa Watanzania kwa matangazo yetu ya pamoja, kwani sote tulikuwa 
wabunifu na wachangamfu. Lakini nikajisemea mwenyewe: “Yote kwa yote, 
lazima mambo yaendelee, tena kwa kasi ile ile.” Nikapania kufanya 
vizuri, japo peke yangu.
Kwa kweli, niliwashukuru sana viongozi wangu kwa 
kuwa na imani nami, hivyo nikadhamiria kutowaangusha hata kidogo. Lakini
 zaidi, nilimshukuru Mwenyezi Mungu maana kama uamuzi ungekuwa tofauti, 
ndoto yangu ya kuitumia safari hii kwa matayarisho ya harusi yangu 
ambayo ilikuwa imepangwa kufanyika mara tu baada ya kurejea, ingeingia 
dosari.
Hii ni kwa vile, katika kujipanga kwa maandalizi 
hayo, nilikuwa nimeiona safari hii kuwa nafasi nzuri ya kujinunulia vitu
 muhimu vya harusi, hasa mavazi yangu na ya mke wangu mtarajiwa.
Tulikuwa tumekubaliana na wazazi wangu kuwa pamoja
 na mambo mengine, wao wangelipa mahari ambayo yalikuwa ni Sh2,000 
(Shilingi elfu mbili), kiasi cha kadiri sana hasa siku hizo, hasa kwa 
vile baba mkwe, Mzee Amos Mwaipopo ambaye alikuwa mzee mtaratibu sana, 
hakutaka makuu ya mahari makubwa na kwamba, mimi nami ningechuku gharama
 nyinginezo hasa hizo za mavazi yetu.
Kwa hiyo, nilipania kwenda kununua nguo za nguvu 
huko New Zealand, hasa za bi harusi, kwa kuwa pia nilikuwa tayari 
namfahamu vyema Mwangaza kwamba alikuwa mtu wa kupenda mavazi ambayo 
kwayo yalikuwa yakimkaa vizuri sana.
Katika desturi za mila za Kibondei, ilikuwa 
vilevile ni wajibu wangu mimi kama bwana harusi kuhakikisha ya kwamba 
namvalisha bi harusi, kwani wakati wa sherehe za kimila, tungetakiwa 
kutoka nje mara tatu, tukiwa tumevaa mavazi tofauti, na huku watu 
wakimwangalia zaidi bi hurusi. Kwa sababu hiyo, nilitarajia kuitumia 
safari hii vizuri kwa lengo hilo.
Kwa hakika siku zilikuwa zikienda haraka haraka 
sana na ghafla tukajikuta tumeingia kwenye mwaka mpya wa 1974, 
ikimaanisha ya kwamba siku za safari zilikuwa zimekaribia mno.
Kikosi cha wanamichezo wa Tanzania kilichokuwa 
kinakwenda kwenye michezo hii kilikuwa kikubwa kiasi. Kulikuwa na 
wanamichezo wengi wa riadha akina Suleiman Nyambui, Mwinga Mwanjala, 
Nzael Kyomo, Norman Chihota na nyota Filbert Bayi na wengine wengi 
wazuri sana.
Pia walikuwamo wachapa masumbwi wazuri tu kama vile Habibu 
Kinyogoli na Emmanuel Mlundwa. Hata tulikuwa na waendeshaji wa baiskeli 
waliokuwa na uhodari wa kushindana kwa kiwango cha juu kwenye mashindano
 kama haya ya kimataifa ikiwa ni pamoja na George Mulamula. 
Halikadhalika tulikuwa na wachezaji wa mpira wa meza (table tennis). Kwa
 kweli ilikuwa timu iliyosheheni vyema.
Wote hawa walipewa nafasi nzuri ya kufanya mazoezi
 ya kweli kweli huku Serikali ikiwa mstari wa mbele wa kugharimia 
maandalizi haya vyema. Vilevile, wale wote ambao tulikuwa kwenye safari 
hii, ikiwa ni pamoja na sisi waandishi wa habari, tulipatiwa sare 
maalumu za kupendeza. Mwandishi mwingine wa habari kwenye safari hii 
alikuwa ni Stephen Rweikiza aliyekuwa akiandikia gazeti la Daily News.
Tuliondoka sote kwa pamoja kuelekea New Zealand 
kwa kutumia ndege ya Shirika la Ndege la Afrika Mshariki (East African 
Airways) hadi Port Luis, Mauritius. Tulilala kwenye kisiwa hiki maarufu 
kwa zao la miwa kwa usiku mmoja.
Nakumbuka sana wakati tulipokuwa tukielekea kwenye
 hoteli hiyo tuliyopangiwa kulala tukipita kwenye ekari na ekari za 
mashamba makubwa sana ya miwa, huku tukipishana na viberenge vingi 
vilivyobeba malundo ya miwa iliyokatwa kupelekwa kwenye vinu vya 
kutengenezea sukari.
Tuliondoka Mauritius mapema asubuhi sana kwa ndege
 kubwa zaidi ya Shirika la Ndege la Qantas kwa safari ndefu ya saa kumi 
na ushei kuivuka Bahari ya Pacific. Ilikuwa vizuri kwamba tulikuwa 
kwenye kundi la watu wengi maana tuliweza kuchangamshana kwa kucheza 
michezo kadhaa midogo midogo mle ndani ya ndege kama vile karata, ili 
kupitisha muda maana hii ilikuwa safari ya kuchosha sana hii.
Tuliwasili mji wa Perth, Australia, kiza kikiwa 
kimeingia. Tulikuwa tumesimama kwa muda tu hapo kubadilisha ndege ya 
kutupeleka Christchurch. Nikiwa kiwanjani hapo nilianza kuona hali ya 
maisha ilivyo tofauti. Niliona maendeleo makubwa ya miundombinu ya 
kisasa zaidi.
Baada ya muda wa saa mbili hivi, tuliondoka Perth 
na ndege ndogo kiasi ya shirika hilo hilo la Qantas kwa mkondo wa mwisho
 wa safari yetu hii, tukawasili New Zealand kiasi cha saa tano usiku 
tukiwa tumechoka sana.
Hata hivyo nilifurahi hatimaye kuwasili nchini New
 Zealand, kwani baada ya miezi kama miwili ya kusubiri na kufanya 
maandalizi mbalimbali sasa nikawa nimetua kwenye hii ya nchi ya mbali 
sana. Maili elfu kadhaa kutoka nyumbani Tanzania. Kwa kweli sikuwa 
nimetarajia kwamba siku moja ningeweza kufika mahali kama huko, na 
mapema kiasi hicho kwenye maisha yangu ya kikazi.
Lakini pia nilifahamu kwamba nilikuwa nakabiliwa 
na changamoto pamoja na kazi kubwa mbele yangu na hasa kwa kuwa sasa 
nilikuwa peke yangu. Kabla ya kuondoka, nilikuwa nimefanya maandalizi 
mazuri ili kuhakikisha kuwa natekeleza kazi yangu kwa kiwango cha juu.
Nilihakikisha ya kwamba nilikuwa nimekusanya kila 
kitu ambacho kingeniwezesha kutoa habari kwa usahihi mkubwa. Nilisoma 
vitabu na majarida mbalimbali kuhusu Michezo ya Jumuiya za Madola. 
Nilifanya juhudi za kuwafahamu wanamichezo mbalimbali maarufu 
watakaokuwepo kwenye michezo hiyo na kuhakikisha nawafahamu vizuri sana 
wanamichezo wetu.
Halikadhalika, nilipata maelezo na maelekezo ya 
kutosha ya jinsi nitakavyokuwa ninatuma habari za michezo hiyo. Tayari 
kulikuwa kumefanyika mawasiliano ya kutosha baina ya RTD na wasimamizi 
wa matangazo ya radio ya mashindano haya ambapo nilikuwa nimepangiwa 
muda na studio maalumu wa kurusha matangazo yangu hayo.
Nilikuwa nimepangiwa kutuma kipindi maalumu cha 
muda wa dakika 15 kila siku za majuma mawili ya michezo hiyo, 
nikifahamisha yote yale muhimu na ya kusisimua ambayo yangekuwa 
yametokea siku nzima kwenye viwanja mbalimbali.
Ili kutia ladha katika matangazo yangu hayo, nilitafuta wimbo 
wangu maalumu, (signature tune) ambayo ningekuwa ninaicheza kila wakati 
wa kufungua na kufunga kwa ripoti hizo. Niliutafuta wimbo huo kwa 
umakini mkubwa, nikishinda kwa muda mrefu kwenye maktaba hadi 
nilipofanikiwa kupata wimbo mzuri wa ala tupu uliokuwa wa kusisimua, 
wenye mahadhi ya ngoma za kienyeji, uliokuwa umepigwa na bendi ya Jeshi 
la Tanzania.
Kwa hakika, nilikuwa nimejipanga vizuri. Lakini 
sasa tukiwa bado hapo kwenye uwanja wa ndege, baaada ya kukamilisha 
taratibu zote za uhamiaji ambazo zilifanyika kwa haraka sana kwa sababu 
tulikuwa wageni mashuhuri, hali ya taharuki ikanitokea baada ya kukosa 
kulipata sanduku langu.
Kama desturi ya safari za ndege, nakumbuka hii 
ilikuwa safari yangu ya kwanza ndefu, nililitoa sanduku hilo pale uwanja
 wa ndege wa Dar na kama wengine wote tukafahamishwa ya kwamba tusiwe na
 shaka yoyote tungepata masanduku yetu hayo mwishoni kabisa mwa safari.
Sasa wakati wenzangu wote walifanikiwa kupata 
masanduku yao, miye langu halikupatikana hata baada ya wasimamizi wa 
ndege na uwanja kufanya juhudi kubwa ya kulitafuta. Kikawa kisanga 
kingine. Nikawa nawaza na kuwazua, Nikaona hii balaa.
Hata hivyo maofisa wa ndege wa Qantas walinitoa 
shaka kwa kunifahamisha ya kwamba wangenipatia kiasi kizuri tu cha fedha
 kuweza kununua nguo chache za kutumia huku wao wakiendelea kulitafuta 
sanduku hilo.
Nilifarijika na kuondoka na wenzangu wote kuelekea
 hoteli tuliokuwa tumepangiwa kufikia sisi waandishi wa habari wakati 
wachezaji na viongozi wao walikuwa wanapelekwa kwenye kijiji maalumu cha
 wanamichezo.
Tulipita maeneo mengi mazuri ya mji huo wa 
Christchurch nikavutiwa nao sana. Mji ulikuwa umepangwa na kupangika 
ukiwa na vivutio vingi vinavyokufanya upende kuishi humo. Lakini pamoja 
na yote hayo, nilijua sasa kazi ndiyo imeanza.
INAENDELEA JUMAPILI IJAYO...
source: Mwananchi
source: Mwananchi
