Askari wa Kikosi cha Zimamoto wakipambana kulizima jengo la kanisa la 
Jeshi la Ukombozi lililotiwa kiberiti na waandamanaji mjini Mombasa leo 
mchana. PICHA | AFP 
            
    Na AFP
Posted Ijumaa,Oktoba4 2013 saa 17:56 PM
Posted Ijumaa,Oktoba4 2013 saa 17:56 PM
Kwa ufupi
- Hali ilianza kuonekana tete toka leo asubuhi, 
ambapo wanausalama wa Kenya walionekana wakijaribu kuboresha ulinzi 
katika mitaa mbali mbali ya mji wa Mombasa kufuatia mauaji ya Omar.
Mombasa. Watu 4 wameuawa
 na wengine 7 kujeruhiwa mjini Mombasa katika ghasia zilizoanza baada ya
 swala leo mchana kufuatia mauaji ya Shehe Ibrahim ‘Rogo’ Omar na 
wenzake watatu jana.
Shehe ‘Rogo’ Omar  na wenza walifariki baada ya 
gari walilokuwa wakisafiria kumiminiwa risasi likiwa njiani kwenye 
barabara ya Malindi-Mombasa, katika shambulizi linaloolekana lilikuwa 
limepangwa  ili kuwatoa roho.
Mkuu wa polisi katika eneo la Kisauni, Jolius 
Wanjohi alithibitisha mauaji hayo ya Shehe Omar, lakini akashindwa kutoa
 maelezo zaidi, hali iliyochochea hisia za wafuasi wa mhubiri huyo na 
kusababisha waingie mtaani mapema mchana wa leo.
Hali ilianza kuonekana tete toka leo asubuhi, 
ambapo wanausalama wa Kenya walionekana wakijaribu kuboresha ulinzi 
katika mitaa mbali mbali ya mji wa Mombasa kufuatia mauaji ya Omar.
Hata hivyo kufikia mchana, waandamanaji waliokuwa 
wakijikusanya katika vikundi vidogo vidogo waliingia barabarani kwa 
ghadhabu, wakirushia magari mawe na kuwasha moto huku wakipambana na 
polisi.
Angalau mmoja kati ya waliokufa katika vurugu hizo
 alipigwa risasi, kwa mujibu wa Red Cross Kenya, huku magari na kanisa 
la Jeshi la Ukombozi (Salvation Army) katika wilaya ya Majengo vikitiwa 
kiberiti.
Shirika la habari AFP linaripoti marehemu wengine 
yaonekana walikufa baada ya kuchomwa na vitu vyenye ncha kali katika 
vurumai hiyo, likimnukuu msemaji wa Kituo cha Kukabiliana na Matukio ya 
Hatari nchini Kenya.
Polisi wanadai walilazimika kutumia mabomu ya 
machozi kuwatawanya waandamanaji katika viunga vya Majengo – eneo ambalo
 wanaishi Wakenya wa kada ya kati, wengi wao wakiwa waumini wa dini ya 
Kiislamu.
Huku Maimamu na viongozi wa kijamii wakiomba 
utulivu, baadhi ya mashuhuda wameiambia AFP kuwa polisi walionekana 
wakipiga risasi za moto hewani wakati wakijaribu kudhibiti vurugu hizo.
Kamanda wa polisi mjini Mombasa, Kipkemoi Rop, 
amethibitisha wamewakamata watu 24 kufuatia ghasia za leo mchana, 
akisisitiza jeshi lake halitavumilia “vikundi vya vijana wahuni  
kuukamata mji [wetu].”
Marehemu Omar alikuwa mhubiri katika msikiti wa 
Musa, na alikuwa mwandani wa mhubiri mwingine machachari wa Kenya, Shehe
 Aboud Rogo Mohammed ambaye pia aliuawa katika tukio lisiloeleweka 
Agosti, 2012.
Tukio hili la jana lilikuja katika kipindi kigumu 
kwa wakazi wa Kenya, wengi wao wakiwa wamejawa hofu kufuatia shambulizi 
la jumba la biashara la Westgate wiki mbili tu zilizopita – tukio hatari
 lililoacha vifo zaidi ya 67 na kusababisha hatihati jijini Nairobi.
Shehe Omar anashutumiwa kuwa na uswahiba wa karibu sana na 
wanamgambo wa Kisomali wa Al-Shabab ambao wamekiri kuhusika katika 
uvamizi wa Westgate.
Baadhi ya Waislamu mjini Mombasa wamevilaani 
vyombo vya dola, wakivituhumu kwa kuchukua ‘hatua za makusudi’ kumwinda 
Shehe Omar na wenzake kama sehemu ya vita yao dhidi ya ugaidi – kauli 
ambayo serikali ya Kenya imeikataa katakata. 
SOURCE: MWANACHI