Na Aidan Mhando, Mwananchi
Posted Alhamisi,Oktoba31 2013 saa 24:0 AM
Posted Alhamisi,Oktoba31 2013 saa 24:0 AM
Kwa ufupi
Ni kauli ya aliyekuwa mchumba wa marehemu Luteni Rajabu, aliyeuawa nchini DRC .
Dar es Salaam. Mchumba wa 
askari wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), aliyeuawa kwa 
kupigwa risasi akiwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Luteni Asia
 Hussein aliyekuwa naye kabla ya kuuawa mchumba wake amesema, marehemu 
alimwomba amwombee arudi salama kutoka kwenye mapigano.
Pia, alisema kauli hiyo ndiyo ya mwisho kuisikia 
kutoka kinywani mwa mchumba wake huyo aliitoa baada ya kutolewa amri ya 
kijeshi kwamba anatakiwa kwenda kuwasaidia wenzake waliokuwa kwenye 
mapigano na askari wa waasi wa M23.
Askari huyo wa(JWTZ), Luteni Rajab Ahmed Mlima, 
aliuawa akiwa kwenye uwanja wa mapambano na vikosi vya askari wa waasi 
wa M23 katika milima ya Gavana, karibu na Goma, DRC wakati akitekeleza 
jukumu la ulinzi wa amani.
Akizungumza katika mahojiano maalumu na gazeti 
hili jana nyumbani kwake, Luteni Asia alisema, “Ninachokumbuka 
walitakiwa kwenda kuwasaidia wenzao waliokuwa kwenye mapigano kwa muda 
mrefu, tayari walikuwa wamezidiwa nguvu na askari wa waasi wa M23, 
ukweli hali ilikuwa mbaya na mimi nilimkataza asiende kwa kuhofia 
usalama wake,” alisema Luteni Asia huku akibubujikwa machozi.
Alisema wakati akimsihi asiende alimjibu kwamba ni
 lazima aende kuwasaidia wenzao, kwani kazi waliyotumwa kuifanya ni 
pamoja na hiyo hivyo asingeweza kuacha kwenda.
Aidha, Luteni Hussein alibainisha kuwa baada ya 
kwenda kutoa msaada na kufanikiwa kuwadhibiti waasi, muda mfupi baadaye 
alipata taarifa kuwa Luteni Mlima amefariki kwa kupigwa risasi jambo 
lililomshtua kiasi cha kuishiwa nguvu kabisa.
Alisema kwa kuwa kazi ya Mungu haina makosa, yeye 
anamwombea huko aliko apumzike kwa amani kwani amefariki akiwa 
anawatetea wananchi wa DRC na kuiwakilisha nchi yake.
Mipango ya harusi
Akielezea mipango yao ya harusi, Luteni Asia 
alisema Desemba 28, mwaka huu walipanga kufunga ndoa na kwamba taratibu 
zote zilikuwa zimekamilika ikiwa pamoja kutolewa mahari.
“Kwa kweli jambo linalo niuma sana na siwezi 
kusahau ni kwamba, tulikuwa tumebakiza muda mfupi tufunge ndoa na kila 
kitu kilikuwa kimeshakamilika hadi ukumbi wa kufanyia sherehe ya harusi 
yetu tulishaulipia,” alisema Luteni Hussein huku akibubujikwa na 
machozi.
Kaka wa marehemu
Akizungumza na gazeti hili, kaka wa marehemu Dk 
Aziz Mlima alisema ndugu yao atazikwa leo Alhamisi saa 10 kwenye 
makaburi ya Kisutu, Dar es Salaam.
JWTZ yatoa tamko
Msemaji wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania
 (JWTZ), Meja Erick Komba alisema mwili wa Luteni Rajab Ahmed Mlima 
ulitarajiwa kuingia jana saa moja jioni na kuhifadhiwa kwenye kambi ya 
Jeshi Lugalo. Alisema taratibu za kuuaga mwili huo zitafanyika kijeshi 
kwenye kambi hiyo kuanzia leo saa tatu asubuhi na mazishi yatafanyika 
kwenye makaburi ya Kisutu Dar es Salaam.
SOURCE: MWANANCHI
SOURCE: MWANANCHI
