Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Utafiti wa Kupunguza Umaskini 
(REPOA),Profesa Samuel Wangwe akizungumza jijini Dar es Salaam jana 
wakati wa kutoa matokeo ya utafiti uliongozwa na taasisi ya 
Afrobarometer. Picha na Silvan Kiwale. 
            
    Na Goodluck Eliona, Mwananchi
Posted Jumatano,Oktoba16 2013 saa 24:0 AM
Posted Jumatano,Oktoba16 2013 saa 24:0 AM
Kwa ufupi
Dar es Salaam. Ripoti mpya ya utafiti imebaini 
kuwa asilimia kubwa ya Watanzania wenye elimu ya darasa la saba na wale 
wasiosoma, ndiyo wanaokubaliana na utendaji kazi wa Rais Jakaya Kikwete.
Ripoti ya utafiti huo iliyopewa jina la ‘Namna 
Watanzania wanavyouangalia utendaji kazi wa Bunge na Rais wa Jamhuri ya 
Muungano wa Tanzania’ ilitolewa jana jijini Dar es Salaam na Asasi ya 
Afrobarometer, inaonyesha kuwa asilimia 77 ya waliokosa elimu ndiyo 
wanamuunga mkono Rais Kikwete.
Afrobarometa ni Asasi ya Kimataifa inayojumuisha 
taasisi tatu za Institute for Democracy ya Afrika Kusini, Ghana Centre 
for Democratic Development ya Ghana na Political Science Department ya 
Chuo Kikuu cha Michigan cha Marekani.
Mtafiti Msaidizi wa Afrobarometer, Stephen 
Mwombela akisoma ripoti hiyo mbele ya waandishi wa habari jijini Dar es 
Salaam, alisema asilimia 72 ya wale walioishia darasa la saba ndiyo 
wanamuunga mkono Rais.
Wakati asilimia 23 ya watu wasiosoma ndiyo 
hawamkubali Rais na asilimia 28 ya wale walioishia darasa la saba, pia 
hawaridhishwi na utendaji wa kiongozi huyo.
Mwombela, hata hivyo, alisema utafiti huo 
uliohusisha watu 2,400 wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania unaonyesha 
kuwa idadi kubwa ya wasomi wa kiwango cha sekondari na kuendelea 
wanaunga pia mkono utendaji wa Rais, lakini siyo kwa kiwango cha juu 
kama wale ambao hawajasoma.
“Asilimia 60 ya waliosoma elimu ya sekondari na 
kuendelea wanaunga mkono utendaji wa Rais, lakini 40 hawakubaliani na 
utendaji wake,” ilisema taarifa ya matokeo ya utafiti huo uliofanyika 
kati ya Mei hadi Juni mwaka jana.
Matokeo ya utafiti huo yanatofautiana na yale ya 
mwaka 2008, ambayo yalionyesha kuwa wasomi walikuwa wanamuunga mkono 
Rais kwa asilimia 92.
Pia katika matokeo ya utafiti huo wa mwaka 2008, ulionyesha kuwa wasiosoma walimuunga mkono kiongozi huyo kwa asilimia 92.
Imani ya wananchi kwa Rais
Ripoti hiyo ilisema pia imani ya wananchi kwa 
utendaji wa Rais imeshuka hadi kufikia asilimia 74 kwa mwaka jana, 
tofauti na asilimia 94 ya mwaka 2005 wakati aliposhika wadhifa huo.
SOURCE: MWANANCHI
Pia utafiti huo uliodhaminiwa na Taasisi ya Utafiti kuhusu 
Kuondoa Umaskini (Repoa) umebainisha kuwa imani ya wananchi kwa Rais 
imeshuka kutoka asilimia 88 mwaka 2008 hadi asilimia 74, huku idadi ya 
watu wasiokubaliana kabisa na Rais ikiongezeka kutoka asilimia 11 mwaka 
2008 hadi asilimia 26 mwaka 2012.
Imani kwa Bunge
Wananchi wengi pia wameonyesha kutokuwa na imani 
na mwenendo wa Bunge, kwa kulipa asilimia 76 mwaka 2012, idadi yao 
ikishuka kutoka asilimia 83 ya mwaka 2008.
Imani ya wananchi kwa Bunge imeshuka katika 
kipindi hiki ambalo liko chini ya Spika Anne Makinda, ambaye alichukua 
uongozi mwaka 2010 wakati mwaka ule wa 2008 lilikuwa chini ya Samuel 
Sitta imani ilikuwa juu. Taarifa hiyo pia inaeleza kuwa watu wanaoishi 
vijijini ndiyo wanaoridhishwa zaidi na Bunge kwa kupata asilimia 63, 
ikilinganishwa na wakazi wa mijini ambao ni asilimia 60.
Pia imebainika kuwa wananchi wa Zanzibar 
wanaridhishwa zaidi na utendaji wa Bunge kwa asilimia 64, tofauti na 
wananchi wa Tanzania Bara ambao wanaridhishwa kwa asilimia 61.
“Watu waliokuwa wanakubaliana na utendaji wa Bunge
 mwaka 2003 walikuwa asilimia 31, lakini mwaka 2012 idadi iliongezeka 
hadi asilimia 61,” alisema Mwombela wakati akiwasilisha matokeo ya 
utafiti huo unaofanyika kwa mara ya tano nchini Tanzania.
Hata hivyo, Mwombela alisema kuwa wananchi wengi 
bado wanafurahishwa na utendaji wa Mahakama, lakini idadi yao imepanda 
kutoka asilimia 73 kwa mwaka 2008 na kuwa asilimia 74 mwaka 2012.
Akichangia baada ya ripoti hiyo kuwasilishwa, Dk 
Abel Kinyondo, alisema kuwa matokeo ya utafiti huo hayajaonyesha 
kuporomoka kwa imani kwa Rais badala yake yameonyesha uhalisia.
“Inawezekana imani kwa Rais haijashuka, badala 
yake imekaa katika hali yake, kwa sababu kitu gani alikifanya 2008 watu 
wakampenda sana, ambacho leo hii hajakifanya hadi wasimpende?” alihoji 
Kinyondo. Kinyondo alionekana kushangazwa na namna Rais alivyoweza 
kupata asilimia 71 wakati nchi inapita katika kipindi kigumu cha rushwa 
na ufisadi.
Mwakilishi kutoka Chama cha Demokrasia na 
Maendeleo (Chadema), Victor Kimesera alisema utafiti huo una kasoro 
kadhaa ikiwa ni pamoja na kumtaja Rais kuwa ndiye mwakilishi pekee wa 
Serikali wakati kuna viongozi wengine wengi. “Kwa upande wa Rais 
walitakiwa kuhoji viongozi wengi zaidi kwa sababu Rais siyo kiongozi 
pekee yake katika Serikali,” alisema.
Naye Naibu Katibu Mkuu wa zamani wa Wizara ya 
Fedha, Dk Jonas Kipokola alisema kama utafiti huo ungefanyika Mei hadi 
Juni mwaka huu, huenda matokeo yangekuwa tofauti. “Siwezi kusema 
yangekuwaje, lakini yasingekuwa hivyo yalivyo,” alisema Kipokola.
SOURCE: MWANANCHI