Na  Joseph Zablon na Elizabeth Edward, Mwananchi
Posted Jumatano,Oktoba16 2013 saa 24:0 AM
Posted Jumatano,Oktoba16 2013 saa 24:0 AM
Kwa ufupi
Anastazia Saro ambaye ni mama mzazi wa Mwandishi wa ITV, Ufoo Saro aliuawa kwa kupigwa risasi mwishoni mwa wiki.
Dar es Salaam. Mamia ya waombolezaji jana 
walimiminika Kibamba nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam kwa ajili ya 
kuaga mwili wa Anastazia Saro ambaye ni mama wa Mwandishi wa ITV, Ufoo 
Saro, aliyeuawa kwa kupigwa risasi mwishoni mwa wiki.
Wakati hayo yakijiri nyumbani, hali ya Mtangazaji 
Ufoo Saro aliyepata majeraha baada ya kupigwa risasi na mzazi mwenzake 
imeendelea kuimarika huku ndugu, jamaa na marafiki wakizuiwa kumwona.
Mwandishi huyo wa habari yuko kwenye uangalizi 
maalumu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa kile kilichoelezwa kuwa 
anahitaji mapumziko ya saa 72 kabla ya kuanza kuonana na watu.
Akizungumza jana nyumbani kwa marehemu, Msemaji wa
 familia, Allelio Swai alisema shughuli za kuaga zimechelewa kutokana na
 taratibu za polisi na pia upasuaji ulikuwa mgumu na marehemu alitolewa 
risasi tano.
Mwili wa mama yake Ufoo, ulitolewa katika chumba 
cha kuhifadhia maiti saa 7 mchana na kupelekwa nyumbani kwake Kibamba 
kwa ajili ya kuagwa.
Naye fundi seremala, Leonard Kiondo alisema siku 
ya tukio alisikia milio ya risasi na baadaye alimwona Ufoo akiwa na 
shumizi ya kulalia akikimbia huku akivuja damu kabla ya kumuhifadhi na 
baadaye kumuwahisha hospitali kwa usafiri wa bodaboda.
Iliwachukua polisi saa moja nzima kabla ya kufika 
eneo la tukio. Mwili wa Anastazia ulisafirishwa jana jioni kwenda 
Machame, Wilaya ya Hai, Mkoa wa Kilimanjaro kwa maziko yatakayofanyika 
leo.
Swai alisema maziko hayo yatafanyika baada ya ibada itakayofanyika katika Kanisa la KKKT Usharika wa Uraa.
Katika hatua nyingine, ndugu, jamaa wa mzazi 
mwenzake Ufoo marehemu walikutana kwa mara nyingine jana kwenye Hoteli 
ya 92, kupanga taratibu za maziko ya ndugu yao Antery Mushi aliyejiua 
kwa kujipiga risasi.
Kaka wa marehemu, Andrea Mushi alisema jana kuwa 
wanakutana kupanga taratibu hizo kabla ya kuusafirisha mwili wa marehemu
 kwenda Moshi kwa mazishi yatakayofanyika kesho.
Hospitali ya Taifa Muhimbili
Ofisa Uhusiano Mwandamizi wa Hospitali ya Taifa 
Muhimbili, Aminiel Aligaesha alibainisha kuwa hali ya Ufoo inaimarika 
ukilinganisha na mara ya kwanza alipofikishwa hospitalini hapo.
“Nimezungumza na daktari anayemshughulikia anasema maendeleo 
yake kiafya ni mazuri ingawa haruhusiwi mtu yeyote kwenda kumuangalia 
kulingana na tiba anazokabiliana nazo”alisema Aligaesha.
Hata hivyo, Aligaesha alikataa kuzungumzia ripoti 
ya daktari kuhusiana na idadi ya risasi zilizotolewa katika mwili wa 
Ufoo kwa madai kuwa hiyo ni siri ya mgonjwa.
“Sina chochote cha kusema zaidi ya anaendelea 
vizuri mambo mengine ni siri ya mgonjwa na daktari atakapoamua mwenyewe 
atawaambia lakini sina jukumu hilo.”
SOURCE: MWANANCHI
SOURCE: MWANANCHI