Mbunge wa Mkoani, Zanzibar (CUF) akiomba mwongozo wa Spika kutaka Bunge 
liondoe Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba 
uliosababisha vurugu bungeni Juzi. Picha na Fidelis Felix 
            
    Na Daniel Mjema, Mwananchi
Posted Septemba7 2013 saa 11:43 AM
Posted Septemba7 2013 saa 11:43 AM
Kwa ufupi
Hata hivyo, muswada huo ulipitishwa na wabunge wa 
CCM na mbunge wa Vunjo, Augustino Mrema (TLP) huku wabunge wa vyama 
vingine vya upinzani wakiususia.
Dodoma. Dakika 90 zilitosha kwa Bunge jana 
kupitisha muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya mabadiliko ya 
Katiba na sasa Rais Jakaya Kikwete ndiye anayesubiriwa kutia saini ili 
uwe sheria.
Hata hivyo, muswada huo ulipitishwa na wabunge wa 
CCM na mbunge wa Vunjo, Augustino Mrema (TLP) huku wabunge wa vyama 
vingine vya upinzani wakiususia.
Vyama vilivyosusia majadiliano na upitishaji wa 
muswada huo ni Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi kutokana na kile walichosema
 kuwa ni kukiukwa kwa kanuni na utaratibu mzima wa mchakato wake. 
Wabunge walikaa kama Kamati ya Bunge zima kuanzia saa 6:30 mchana na 
ilipofika saa 8:00 mchana, muswada huo ulikamilika kwa hatua zote.
Wakati wabunge wa upinzani wakiwa wametoka nje, 
Mbunge wa Maswa Magharibi (Chadema), John Shibuda na Clara Mwaituka 
(CUF) walikuwepo bungeni hadi Bunge lilipofikia kuwa kamati ndipo 
walitoka ndani ya ukumbi.
Hata hivyo, Serikali ilikubali mapendekezo ya 
wabunge kikiwemo kifungu kilichohusu taasisi kupeleka majina kwa Rais 
ili ateue mjumbe mmoja kuingia katika Bunge Maalumu la Katiba.
Waziri wa Sheria na Mambo ya Katiba, Mathias 
Chikawe alisema kutokana na Serikali kuridhia mapendekezo hayo ya 
wabunge, sasa taasisi hizo zitapeleka majina tisa ili Rais ateue jina 
moja.
Hata hivyo pamoja na kupeleka majina hayo tisa, 
sheria haitambana Rais kwamba ni lazima ateue mmojawapo kutoka katika 
orodha hiyo na idadi ya wajumbe kutoka taasisi hizo haitazidi 166.
Pia Serikali iliridhia pendekezo la wabunge la 
kuondoa takwa la lazima la mwombaji wa nafasi ya Mwenyekiti wa Bunge la 
Katiba kwamba awe na ama shahada ya sheria, uchumi ama sayansi ya siasa.
 Chini ya mabadiliko hayo sasa, mwombaji wa nafasi hiyo sasa atatakiwa 
kuwa na shahada kutoka katika chuo kikuu chochote kinachotambuliwa na 
Tume ya Vyuo Vikuu nchini (TCU).
Pia Serikali imeridhia kukifanyia marekebisho 
kifungu kinachohusu ukomo wa Bunge la Katiba kutoka siku 90 zilizokuwa 
zimependekezwa awali na sasa suala hilo litakuwa mikononi mwa Rais.
Wakati wa mchakato huo, suala la wabunge wa 
upinzani kutoka nje na kususia vikao vya Bunge liliendelea kuchomoza, 
huku Serikali ikisisitiza kwamba Zanzibar ilishiriki kikamilifu katika 
kutoa maoni ya mabadiliko hayo
source: Mwnanachi