Na Daniel Mjema,Mwananchi
Posted Ijumaa,Novemba1 2013 saa 24:0 AM
Posted Ijumaa,Novemba1 2013 saa 24:0 AM
Kwa ufupi
Wadaiwa kuwa wamesharejesha Sh80 milioni baada ya kubanwa na makachero wa polisi.
Moshi. Askari polisi wawili wa 
Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), wametiwa mbaroni kwa tuhuma za kula 
njama na kushiriki katika uporaji wa Sh220 milioni za Kampuni ya Dot 
Services ya mjini Moshi.
Habari za uhakika zilisema baada ya kubanwa na 
makachero, askari hao walirejesha Sh60 milioni na watuhumiwa wengine 
wawili ambao ni raia, walirejesha Sh23 milioni. Askari hao ni wale 
walioko katika Kikosi cha Polisi wa doria wanaotumia pikipiki na jana 
watuhumiwa wote walitawanywa katika vituo mbalimbali ili wahojiwe kwa 
nyakati tofauti tofauti.
Habari za kipolisi zilisema askari hao hawakwenda 
eneo la tukio lakini walifahamu mpango mzima kuhusu uporaji huo 
uliowawezesha kupata mgawo wa fedha hizo.
Waliotiwa mbaroni wana vyeo vya Constable (majina 
tunayo) na inaelezwa kuwa tukio hilo limewachukiza baadhi ya polisi 
wakidai ni kuwa mfululizo wa matukio yanayochafua sura ya jeshi hilo.
Habari hizo zimebainisha kuwa tukio hilo ni mpango
 mahususi uliowashirikisha watu wasiopungua 10 wakiwamo baadhi ya 
watumishi wa Kampuni ya Dot Services waliovujisha mpango wa kuhamisha 
fedha hizo.
Kulingana na vyanzo vya habari, idadi ya 
walioshiriki katika mpango wa kupora fedha hizo ni kati ya watu wanane 
na 10 na tayari polisi wameanzisha msako mkali wa kuwatafuta.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa Kilimanjaro, Robert Boaz
 alikaririwa akisema kuwa fedha hizo ziliporwa Jumanne asubuhi katika 
makutano ya Barabara za Arusha na Boma mjini Moshi.
Kwa mujibu wa Kamanda Boaz, baada ya kufika katika
 makutano hayo, wafanyakazi wa Kampuni ya Dot Services waliokuwa na gari
 aina ya Toyota Hilux T.864 AZM walisimama kuruhusu pikipiki ipite.
Kamanda Boaz alisema wakati wakisubiri pikipiki 
ipite, ghafla walijitokeza watu wawili wakafungua milango na kuingia 
ndani ya gari na kuwateka wafanyakazi na kuwaamuru waelekee eneo la 
Shanty Town.
Hata hivyo mkurugenzi wa Fedha wa kampuni hiyo ya 
ujenzi yenye makao yake makuu nchini Uganda, Shuresh Bab alifanikiwa 
kuruka kwenye gari hilo na kutoa taarifa polisi.
Kamanda Boaz alifafanua kuwa msako wa kuwatafuta 
wahusika ulianza mara moja ambapo polisi walifanikiwa kulipata gari hilo
 na wafanyakazi wakiwa wametelekezwa mto Karanga mjini Moshi.
SOURCE: MWANANCHI