Thursday 15 August 2013

Hofu madaraka ya Rais yamchefua Kabudi



                     
Katiba 
Na Julieth Ngarabali, Mwananchi  (email the author)

Posted  Jumatano,Agosti14  2013  saa 14:34 PM
Kwa ufupi
Ataka watu waseme kama Tanzania haina mtu mwenye sifa ya kuwa Rais au la ili nafasi hiyo ifutwe


“Kama mnaona hakuna mtu anayefaa kuwa Rais mseme mapema ili hiyo nafasi ikiwezekana ifutwe na la, mkiona yupo anayefaa kuwa Rais, mjue kuna mambo atayafanya kama Mkuu wa Jamhuri ya Muungano na hili halina ubishi jamani.”
Hii ni kauli ya Mwenyekiti wa Timu ya Wajumbe wa Tume ya Taifa ya Katiba, Profesa  Palamagamba Kabudi wakati akitoa ufafanuzi wa Rasimu ya Katiba kwa wajumbe wa Baraza la Katiba la Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha Vijijini.
Profesa Kabudi alitoa kauli hiyo baada ya kuzuka malumbano miongoni mwa Wajumbe wa Mabaraza ya Katiba kuhusu mamlaka ya Rais yaliyopendekezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba kwenye rasimu hiyo ya awali.
Aliendelea “Mbona mna wasiwasi sana na hii nafasi ya Rais? Jamani naomba muiamini Tume na msiwe  na hofu na madaraka ya Rais wa Jamhuri ya Muungano yaliyopendekezwa katika hii Rasimu ya Katiba ambayo mtaenda kuijadili hapa na kutoa maoni yenu.”
Mwenyekiti huyo anasema kuwa tume imeangalia mbali na kupendekeza Serikali tatu ambapo katika nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano, imependekeza afanye mambo machache ambayo ni ya Muungano tu na siyo mambo madogo kama ilivyokuwa awali.
Alisema katiba ya sasa imekuwa ikimpa Rais madaraka makubwa mno ambayo mengine amekuwa akiyafanya na kujikuta yanamtia doa yeye Rais moja kwa moja, huku makosa yakiwa yamefanyika chini kwa watendaji waliopo.
“Mnajua hivi sasa kuna baadhi ya mambo ambayo Rais amekuwa akipata doa kwa sababu tu katiba imemvisha moja kwa moja kama mtendaji. Kwa mfano masuala ya kudorora elimu nchini na mengineyo yamemchafua, lakini sasa katika hii rasimu, Tume imependekeza yeye kushughulika na mambo ya Muungano tu hayo mengine ya elimu, barabara, zahanati yatamhusu mtu mwingine,” alisema Profesa Kabudi.
Ametaja baadhi ya madaraka na majukumu ya Rais wa Jamhuri ya Muungano kuwa ni pamoja na kuwa Amiri Jeshi Mkuu, kusimamia na kulinda katiba, kulinda utaifa wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, kuteua mabalozi na kuteua Mwanasheria Mkuu.
Akiendelea kutoa ufafanuzi wa hoja za wajumbe hao, mwenyekiti huyo ameongeza kwa kuwataka wananchi wasiangalie madaraka bali waangalie uwakilishi wa maendeleo.
Aidha amewataka wajumbe wa Mabaraza ya Katiba wilayani humo kutoa maoni yao waliyotumwa na wananchi na siyo vyama vyao kwani wao hawajafika kwenye vikao hivyo kwa sura ya vyama bali uwakilishi wa wananchi wa maeneo wanakoishi.

chanzo: Mwananchi news paper