Thursday 15 August 2013

Rais Kikwete kamata mafisadi, Watanzania wapumue



Posted  Jumatano,Agosti14  2013  saa 21:5 PM.
Kwa ufupi
Kutokana na hali hiyo, ni wakati mzuri kwa Rais ambaye ni Mwenyekiti wa CCM kuwakamata mafisadi wizarani, mikoani, wilayani hadi vijijini.

Kutokana na hali ya ufisadi nchini ilipofikia sasa, kwa maoni yangu ipo haja kwa Rais Jakaya Kikwete kuwatuliza Watanzania kwa kutenda jambo ambalo halijawahi kutokea kwa kipindi kirefu.
Watanzania wengi wanaamini kwamba Rais Kikwete ni muumini mzuri wa dini, anajali hali za watu, ni kiongozi makini, lakini wanakata tamaa kutokana na kasi ya ufisadi inavyozidi kushika kasi katika Serikali yake.
Ufisadi kwenye halmashauri nchini sasa unatajwa kuwa ni kama chama kikuu kilichojipanga kuiangusha Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Pamoja na wakurugenzi wengi wa halmashauri kushughulikiwa, lakini ukweli ni kwamba ufisadi umekithiri serikalini.
Kutokana na hali hiyo, ni wakati mzuri kwa Rais ambaye ni Mwenyekiti wa CCM kuwakamata mafisadi wizarani, mikoani, wilayani hadi vijijini.
Rais achukue hatua ikiwamo ya kuwataka warudishe fedha zote ndani ya muda maalumu. Wakabidhi kwa serikali ‘mahekalu’ yote yaliyojengwa kwa ufisadi. Pamoja na kwamba wamejenga kwa majina ya watoto, wajukuu na hata ndugu wengine, lakini wajisalimishe na kujieleza ni jinsi gani walivyopata fedha.
Kwa wale wanaotuhumiwa kwa ufisadi mpya, Rais aseme neno likiwamo la kuwataka wajibu hadharani mbele ya Watanzania kupitia vyombo mbalimbali vikiwamo vya habari na hatimaye kuwapeleka kortini.
Ikumbukwe, Watanzania wengi wanaipenda Serikali iliyoko madarakani.
Watanzania wamesikia mambo ya watumishi wa Serikali kukamatwa na nyara, mambo ya Bandari, Mambo ya Wizara ya Mambo ya Nje, ufisadi ujenzi wa barabara ambako ufisadi umesababisha gharama za ujenzi kuwa kubwa. Kilometa moja ya lami sasa inakaribia Sh1 bilioni bila sababu za msingi.
Wizi mwingine wa mafisadi sasa ni wa maandishi kwa kuongeza cha juu kuanzia Sh100 milioni na kuendelea hadi mabilioni. Viongozi waliopewa dhamana wanapokubali kila kitu wanachoambiwa na wataalamu wao hususan masuala ya fedha, ni wazi wanaruhusu ufisadi. Kikwete atoe neno sasa.
Taarifa za ufisadi zinaripotiwa kuanzia wizarani, mikoani, halmashauri hadi vijijini. Hata mwanasheria mkongwe wa kimataifa, Nimrod Mkono anaamini kwamba asilimia 60 ya fedha za Serikali kwa ajili ya kununua madawati zinaishia kwenye mikono ya watu binafsi. Rais kamata wanaotajwa kuhusika.
Mkono alinukuliwa na gazeti hili akisema ufisadi kwenye fedha za Serikali ni balaa. Kwa hali hiyo Rais anaweza kuwatuliza Watanzania kama atatenda lolote zito dhidi ya watu wanaotuhumiwa.

Mwananchi news paper