Friday 16 August 2013

Madiwani waliotimuliwa Bukoba wazidi kuigawa CCM

 
Katibu wa Itikadi na Uenezi ya CCM, Nape Nnauye 
Na  Phinias Bashaya  (email the author)

Posted  Alhamisi,Agosti15  2013  saa 21:12 PM
Kwa ufupi
Kauli ya Nape ndiyo iliyomfanya Buhiye jana kuitisha mkutano wa waandishi wa habari na kusema haamini kama kauli ya kupinga uamuzi huo imetolewa na kiongozi huyo wa kitaifa ambaye anaifahamu vyema Katiba ya CCM inayowapa mamlaka hayo.

Bukoba. Sasa ni dhahiri kwamba kuna mvutano baina ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Kagera na taifa kuhusu kufukuzwa uanachama kwa madiwani wake wanane katika Manispaa ya Bukoba.
Mvutano huo unadhihirishwa na kauli iliyotolewa jana na Mwenyekiti wa CCM wa mkoa huo, Costansia Buhiye ambaye ametetea uamuzi wa kuwatimua madiwani hao, huku Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahaman Kinana akisema wameitisha mafaili yenye nyaraka zinazoeleza jinsi uamuzi huo ulivyofikiwa.
Kinana akizungumza na gazeti hili jana kwa simu kutoka Arusha alisema: “Tayari katibu wetu wa mkoa ametuletea mafaili yenye nyaraka zinazohusu suala hilo na suala hilo litapelekwa kwenye kamati ya maadili na baadaye kuamuliwa na Kamati Kuu.”
Kinana alisema msingi wa suala hilo kuamuliwa na vikao vya juu vya CCM unazingatia azimio lililowahi kupitishwa na vikao vya chama hicho likielekeza kwamba uamuzi wa kuwafukuza wanachama ambao waliochaguliwa na wananchi unapaswa kupata baraka za vikao vya juu.
Kauli ya Kinana inaunga mkono ile iliyotolewa juzi na Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye ambaye alisema madiwani waliotimuliwa waendelee na kazi hadi vikao vya juu vitakapofanya uamuzi wa mwisho na kwamba halmashauri ya chama hicho mkoani Kagera ilifanya makosa kufikia uamuzi wa kuwafukuza.
Kauli ya Nape ndiyo iliyomfanya Buhiye jana kuitisha mkutano wa waandishi wa habari na kusema haamini kama kauli ya kupinga uamuzi huo imetolewa na kiongozi huyo wa kitaifa ambaye anaifahamu vyema Katiba ya CCM inayowapa mamlaka hayo.
Buhiye alisema uamuzi wa kuwatimua madiwani hao ulichukuliwa kwa wakati na muda mwafaka na kwamba lazima vikao vya chini pia viheshimiwe kwani hakuna kikao chenye uhalali wa kufuta uamuzi wa kikao kingine kilichofanyika kwa mujibu wa katiba ya chama hicho. “Uamuzi wa kuwawajibisha madiwani ni sahihi na uamuzi wa vikao vya chini lazima uheshimiwe. Hata Halmashauri Kuu (Nec) ikikutana itarejea katiba ya chama chetu na kanuni zilezile tulizopitia,’’ alisema Buhiye.
Buhiye alisema amelazimika kuitisha mkutano huo ili kupunguza shinikizo la wanachama aliodai wanataka kuandamana kutetea uamuzi uliofanywa na uongozi wa CCM Mkoa.
“Nimewaita ili kutoa ufafanuzi sahihi nipunguze shinikizo la wanachama wanaotaka kuandamana hadi hapa ofisini, wana imani na Halmashauri Kuu ya Mkoa tuendelee kutulia,’’ alisema Buhiye.
Chadema yawaponda waliotimuliwa
Chadema Wilaya ya Bukoba Mjini kimewaponda madiwani wa CCM waliotimuliwa kikisema wanastahili kutokana na kugomea vikao kwa mwaka mzima, ikiwamo bajeti ya maendeleo ya wananchi


Mwenyekiti wa chama hicho, Victor Shelejei alisema zipo njia nyingi za kuwashughulikia watuhumiwa wa ufisadi lakini si kugoma kujadili mambo yanayohusu maendeleo ya wananchi.
Mwenyekiti huyo alisema malumbano ya madiwani na meya yanazidi kudidimiza maendeleo ya wananchi. Madiwani waliotimuliwa ni Yusuph Ngaiza ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Bukoba na Diwani wa Kashai, Naibu Meya wa Manispaa hiyo, Alexander Ngalinda (Buhembe), Samuel Ruhangisa (Kitendagulo), Robert Katunzi (Hamugembe), Deus Mutakyahwa (Nyanga), Richard Gasper (Miembeni), Mulungi Kichwabuta (Viti Maalumu) na Dauda Kalumuna (Ijuganyondo).
Ofisi ya Waziri Mkuu yatajwa
Katika hatua nyingine, ukimya wa Ofisi ya Waziri Mkuu kukalia taarifa ya tume ya kuchunguza tuhuma za ufisadi dhidi ya Meya wa Manispaa ya Bukoba, Dk Anatory Aman unadaiwa kuchochea mgogoro huo.
Tume hiyo ilichunguza tuhuma zilizoibuliwa na Mbunge wa Bukoba Mjini, Balozi Khamis Kagasheki dhidi ya Meya Aman kwamba ameiingiza manispaa hiyo kwenye miradi ya ufisadi, madai ambayo yalikuwa yakiungwa mkono na madiwani waliotimuliwa.
Serikali iliunda tume iliyoongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Abbas Kandoro kuchunguza tuhuma hizo na ilimaliza kazi yake miezi mitatu iliyopita lakini hadi sasa majibu yake hayajawekwa wazi. Alipoulizwa sababu za majibu ya tume hiyo kutowekwa hadharani hadi sasa, Kandoro alijibu waulizwe viongozi waliomtuma.
Kwa upande wake, Buhiye alisema CCM mkoani Kagera haifahamu lolote kuhusu taarifa ya Tume ya Kandoro na kwamba wameomba makao makuu ya chama hicho iwasaidie kuipata kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu.

source : mwananchi

Sou