Tuesday 18 June 2013

Mlipuko Soweto-ArushaMtoto: Nilipigwa risasi na polisi

 
 
Na Waandishi Wetu,  (email the author)

Posted  Jumatatu,Juni17  2013  saa 20:45 PM
Kwa ufupi
“Namkumbuka aliyenipiga risasi alikuwa amevaa sare za polisi,” alisema Adam mwanafunzi katika Shule ya Msingi Levolosi huku akitokwa machozi.
 
Arusha/Dodoma. Wakati watu waliofariki kwenye tukio la kurushwa bomu katika mkutano wa Chadema ikifikia watatu baada ya jana kufariki kwa mtoto Amir Ally (7), mtoto mwingine wa miaka kumi na moja aliyejeruhiwa, amedai kwamba alipigwa risasi na polisi kwenye tukio hilo.
Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe naye ametoa tamko kuwa chama chake kina ushahidi wa kutosha wa watu waliohusika na tukio la kurushwa bomu katika mkutano wa kampeni wa chama hicho.
Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali ya Arusha Medical Lutheran Center (ALMC), Dk Paul Kisanga alisema jana kuwa, Amir alifariki jana asubuhi baada ya kupata majeraha makubwa kichwani yaliyodhuru ubongo wake.
Dk Kisanga alisema huyo ni mmoja wa watoto watano, waliojeruhiwa wakati wakitoka madrasa huko Kaloleni, jirani na Uwanja wa Soweto kulipokuwa na mkutano na alifariki jana asubuhi hospitalini hapo.
Alisema watoto wengine wawili ambao ni ndugu; Fatuma na Sharifa Jumanne wamepelekwa Nairobi kwa matibabu zaidi baada ya miili yao kukutwa na vyuma. Dk Kisanga aliwataja watoto wengine waliojeruhiwa kuwa ni Fahad Jamal (7) ambaye yupo ICU akisubiri timu ya madaktari bingwa kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kutokana na hali yake kutoruhusu kusafirishwa. Pia yupo Abubakar Adam (11) ambaye amejeruhiwa mguuni na amelazwa katika Hospitali ya Mkoa, Mount Meru.
Mtoto aeleza kupigwa risasi
Adam alisema jana kuwa alipigwa risasi na mtu aliyekuwa amevalia sare za polisi, wakati akitoka madrasa akiwa na ndugu yake, Fahdi katika eneo la Soweto.
Alisema akiwa njiani, aliona watu wakimkimbiza mtu na ghafla alishangaa kupigwa risasi na kuanguka chini.
“Namkumbuka aliyenipiga risasi alikuwa amevaa sare za polisi,” alisema Adam mwanafunzi katika Shule ya Msingi Levolosi huku akitokwa machozi.
Muuguzi wa zamu, katika katika wodi ya watoto katika Hospitali ya Mount Meru, Asha Semdeli alisema jana kuwa mtoto huyo ana vyuma viwili katika mguu wake.
“Tunasubiri afanyiwe upasuaji kwani tayari mashine ya X-ray inaonyesha vyuma kuwepo katika mguu wa Adam siwezi kusema ni risasi au la,” alisema Semdeli.

Polisi wazungumzia risasi
Mkuu wa Ufuatiliaji na Tathmini wa Polisi, Kamishna Isaya Mngulu alisema hakuwa na taarifa za watu kufa na kujeruhiwa na polisi kwa risasi. Hata hivyo, alikiri kuwa wameokota maganda ya risasi, ambayo wanafanyia uchunguzi.
“Ni kweli tulikuta maganda ya risasi kwenye tukio lakini ni vigumu kusema kama polisi ndio walipiga bunduki. Nadhani ni mapema mno kwani bado tuko kwenye uchunguzi,” alisema Mngulu, ambaye yumo katika timu iliyoteuliwa na Mkuu wa Polisi (IGP), Said Mwema kuchunguza tukio hilo.
Lakini, Kamanda wa Polisi wa Arusha, Liberatus Sabas alisema hana taarifa ya watu kupigwa risasi... “Mimi sijui lolote kuhusu watu kupigwa risasi. Naomba usiniulize mambo ya ajabu ajabu,” alijibu kwa ukali na kukata simu alipoulizwa juu madai hayo ya polisi kutumia risasi za moto.
Majeruhi mwingine
Majeruhi mwingine, Abdallah Hilali (39), aliyelazwa katika Hospitali ya Arusha Lutheran Center, amedai kuwa majeraha aliyopata miguuni yametokana na kupigwa risasi na polisi na kudondokewa na vipande vya bomu.
Alisema alikuwa nyuma ya jukwaa kuu akimsikiliza Mbowe na alipomaliza kuhutubia alishuka jukwaani kukusanya sadaka, ndipo alipoona mfuko wa mweusi mdogo wa plastiki ukipeperuka juu.
“Nilidhani ni upepo unapeperusha kitu, lakini ghafla nilisikia kishindo na nikamsikia mama mmoja akipiga kelele kuwa aliyerusha mfuko anakimbia, nilipogeuka nikajikuta nipo chini,” alisema Hilali.
Alisema alipokuwa anaangalia aliona kijana mmoja amekaribia kumfikia aliyerusha bomu lakini ghafla akapigwa risasi na kuanguka chini na aliyekuwa anafuatia kwa nyuma naye akapigwa risasi akaona anaruka na kudondoka chini huku damu zikivuja.
“Lakini mwisho wa yote kijana aliyerusha hilo fuko aliingia kwenye gari na kuondoka kwa kasi. Mimi nilikuwa chini,” alisema Hilal mbele ya Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, alipotembelea majeruhi hospitalini hapo.
Jana, Makamu wa Rais, Dk Mohamed Gharib Bilal na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda walitembelea majeruhi waliolazwa katika hospitali mbalimbali za Arusha.
Mbowe tunawajua watuhumiwa
Mbowe amedai kuwa wamewagundua watu waliohusika na urushaji wa mabomu katika Viwanja vya Soweto Juni 15, mwaka huu na kusababisha vifo vya watu watatu na majeruhi zaidi ya 60.
Akizungumza jana baada ya kutembelea majeruhi katika Hospitali ya Seliani, Mbowe alisema Chadema tayari imewajua wahusika wakuu wa mabomu hayo kwa ushahidi wa picha. Alidai kuwa ni askari mmoja wa Kikosi cha Polisi wa Kuzuia Fujo (FFU).
Alidai kuwa ushahidi huo unaonyesha kuwa wakati askari huyo akirusha bomu, alikuwa na kofia inayofanana na ile inayotumiwa na Polisi na mara baada ya kurusha bomu na risasi za mfululizo alikimbilia kwenye gari aina ya Land Cruiser na kusindikizwa na Polisi.
“Duniani hakuna siri yoyote ile. Tumeshafanikiwa kugundua chanzo kikubwa na ushahidi unaonyesha wahusika ni polisi. Ushahidi huu tutauweka hadharani na kila mwanadamu aweze kujionea kwa kuwa waliokufa hawana hatia yoyote na sisi tumechoka kila siku kuonewa na Polisi,” alisema.
Aidha, Mbowe amepinga kauli ya Spika wa Bunge, Anne Makinda na ile ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Bunge, Uratibu na Sera), William Lukuvi kuwa Arusha inaharibiwa na wanasiasa pamoja na asasi binafsi.
Nape aituhumu Chadema
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye amekituhumu Chadema kuwa ndicho kilichofanya mpango wa kulipua bomu lililosababisha vifo vya watu watatu jijini Arusha baada ya kubaini kuwa kitashindwa katika uchaguzi wa udiwani katika kata nne.
Amedai kuwa mpango huo ulipangwa na Chadema baada ya wananchi wa Arusha kuapa kutokichagua tena kutokana na kuchoshwa na kauli za viongozi wake zinazochochea maandamano na vurugu, jijini humo.
Akizungumza na waandishi wa habari Dodoma jana, Nape alisema Chadema kinatakiwa kuacha kutafuta umaarufu kwa mtindo wa kumwaga damu za Watanzania na kwamba juhudi hizo zinatakiwa kulaaniwa vikali.
Alipoulizwa sababu za kukitaja Chadema kuwa kinahusika moja kwa moja licha ya kuwa uchunguzi wa awali uliofanywa na Jeshi la Polisi umeonyesha kuwa mazingira ya tukio hilo yanafanana na lile la kanisani alisema, “Tunasema hivyo kutokana na kauli zilizokuwa zikitolewa na viongozi wa Chadema kabla ya tukio na walipanga ndani ya chama chao ili uchaguzi usifanyike.”
Mamia wakusanyika Soweto
Mamia ya wananchi jana walikusanyika katika Viwanja vya Soweto ulikotokea mlipuko huo, kwa ajili ya kuomboleza
Share

Mazishi ya waathirika wa tukio hilo yanatarajiwa kufanyika mara baada ya uchunguzi wa madaktari kukamilika na miili itaagwa katika eneo hilo kabla ya kusafirishwa katika maeneo yao ya asili. Mwili wa Judith Moshi utasafirishwa kwenda Kilimanjaro, Ramadhan Juma (Tabora) na wa Amir utapelekwa Lushoto.
Mlipuko huo ulitokea juzi wakati Chadema, kilipokuwa kikihitimisha kampeni zake za udiwani na kusababisha kuahirishwa kwa uchaguzi katika kata za Themi, Kaloleni, Elerai na Kimandolu hadi Juni 30.
Marekani yalaani
Balozi wa Marekani nchini Tanzania, Alfonso Lenhardt ameshutumu vikali mlipuko wa bomu kwenye mkutano huo wa kampeni wa Chadema Arusha ambao ulisababisha vifo vya watu watatu na wengine zaidi ya 60 kujeruhiwa.
Balozi Lenhardt ametuma salamu za rambirambi kwa familia zilizofiwa na kutoa pole kwa wale walioumia.
“Tunaomba vyombo vya dola kuhakikisha wahusika wanakamatwa na kushtakiwa,” alieleza Balozi huyo katika taarifa yake.

chanzo: Mwananchi