Monday 17 June 2013

MADIBA:: Usinipigie simu, nitakupigia mimi


Kwa ufupi
Pamoja kuwa nje ya ulingo wa siasa, ameendelea kuwa kiongozi anayeheshimika na mchango wake wa mawazo umekuwa ukithaminiwa duniani kote.“Usinipigie simu, nitakupigia.” Hayo ni maneno aliyosema Rais wa zamani wa Afrika Kusini, Nelson Mandela alipotangaza kustaafu maisha ya siasa na kuhudumia jamii.
Mandela alisema kuwa hataki kupigiwa simu ya kualikwa sehemu yoyote isipokuwa, ikiwa anahitaji kuwapo atapiga simu kuomba ashirikishwe.
Tangu wakati huo ameonekana hadharani mara chache. Mwaka 2010, ofisi yake ilitoa picha ikimwonyesha kiongozi huyo akiwa na viongozi wa vyama vya soka vya Marekani na Afrika Kusini.
Pamoja kuwa nje ya ulingo wa siasa, ameendelea kuwa kiongozi anayeheshimika na mchango wake wa mawazo umekuwa ukithaminiwa duniani kote.
Kwa miaka miwili sasa hali yake kiafya imetetereka. Mwanzoni mwa mwaka 2011, alilazwa katika hospitali moja huko Johannesburg kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi wa afya yake.
Mzee Mandela amekuwa akisumbuliwa na matatizo ya uambukizi katika mapafu. Inaelezwa kuwa alipofungwa katika gereza la Robben miaka ya 1980, aliwahi kuugua ugonjwa wa TB.
Hata hivyo mwanzoni mwa mwaka jana, alipatiwa matibabu mengine kwa madai kuwa alikuwa akisumbuliwa na maradhi ya tumbo. Katika miezi ya karibuni maambukizi katika mapafu ndiyo yamekuwa yakimsumbua.
Mandela alizaliwa Julai 18, 1918 na kupewa jina la Rolihlahla Dalibhunga huku akipewa jina la ukoo Madiba. Jina la Nelson alipewa na mwalimu wake.
Baba yake, Henry Mandela aliyekuwa kiongozi wa Kabila la Thembu, alifariki wakati Madiba akiwa na umri wa miaka minane.
Mwaka 1941, akiwa na umri wa miaka 23, Madiba alikimbilia Johannesburg, baada ya kutakiwa amuoe binti aliyechaguliwa na wazee kijijini kwake.
Miaka miwili baadaye alijiunga na Chuo cha Witswaterand University kusomea sheria, huko alikuwana na watu mbalimbali ambao walimfungua macho na hapo ndipo mwamko wake kisiasa ulianza.
Mwaka huohuo alijiunga na Chama cha African National Congress (ANC), baadaye alishirikia kuanzisha tawi la vijana la chama hicho, ‘ANC Youth League’.

Alifunga ndoa na mke wake wa kwanza, Evelyn Mase, mwaka 1944 na walifanikiwa kupata watoto wanne. Ndoa yake na mwanamke huyo ilidumu kwa miaka 14 na waliachana mwaka 1958.
Mzee Mandela alipata leseni ya kuwa Mwanasheria mwaka 1952. Akishirikiana na rafiki yake Oliver Tambo walifungua ofisi inayoshughulikia masuala ya kisheria katika Jiji la Johannesburg.
Akiwa na rafiki yake huyo, walipambana kuondoa utawala wa kibaguzi nchini Afrika Kusini kwa miaka mingi. Mwaka 1959 yeye na washirika wake walishtakiwa kwa makosa ya uhaini. Hata hivyo, kesi yao ilifutwa baada ya miaka minne.
Mandela alipohukumiwa kifungo cha maisha katika kipindi cha miezi 18 ya mwanzo, mama yake mzazi na mtoto wake walifariki dunia. Hata hivyo hakuruhusiwa kushiriki mazishi hayo.
Maisha ya Mandela
Nelson Mandela ni mmoja wa viongozi wanaoheshimika zaidi duniani kutokana na juhudi zake za kupigania usawa na demokrasia.
Alifungwa kwa miaka 27, aliachiwa huru mwaka 1990 na kuwa Rais wa Kwanza mweusi wa Afrika Kusini. Miaka minne baadaye aliachia wadhifa huo. Alishinda tuzo ya amani ya Nobel mwaka 1993.
Watu waliomfahamu Mandela kwa miaka mingi wanasema kuwa ni mtu anayeipenda familia yake kuliko kitu kingine, hata wakati alipostaafu alisema anataka muda uliobaki autumie akiwa na familia yake.
Akiwa na umri wa miaka 80 alifunga ndoa na Graca Machel akisema kuwa anataka kuiunganisha familia yake baada ya kuachana na mkewe wa pili, Winnie Mandela.
Na Julieth Kulangwa kwa msaada wa Mashirika ya Habari