Tuesday 29 October 2013

Kesi ya mauaji ya RPC Barlow Jumatatu


Na Sheilla Sezzy, Mwananchi

Posted  Jumatatu,Oktoba28  2013  saa 21:55 PM
Kwa ufupi
Kwa mara ya mwisho, kesi hiyo ilitajwa Oktoba 22 mwaka huu mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Mkoa wa Mwanza, Angelous Rumisha.



Mwanza. Kesi ya mauaji ya aliyekuwa Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mwanza, Liberatus Barlow, inatarajiwa kutajwa tena Novemba 4 mwaka huu, katika Mahakama ya Hakimu mkazi jijini hapa.
Watu saba wanashikiliwa mahabusi wakihusishwa na mauaji ya ofisa huyo mwandamizi wa polisi.
Washtakiwa hao ni, Muganyizi Michael (36) mkazi wa Nyakabungo na Magige Mwita Marwa, maarufu “Tatoo” (48) mkazi wa Bugarika.
Wengine ni Abdallah Petro au Amos Abdalah (32), ambaye ni mkazi wa Mjimwema na Abdulrahman Ismail (28), mkazi wa Mkudi jijini Mwanza.
Orodha hiyo inawajumuisha pia Chacha Wekena (50), ni mkazi wa Gongolamboto, Dar es Salaam, Buganze Edward Luseta (22), mkazi wa Tandika, Dar es Salaam na Bhoke Mwita (42), mkazi wa Mombasa Ukonga, Dar es Salaam.
Kwa mara ya mwisho, kesi hiyo ilitajwa Oktoba 22 mwaka huu mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Mkoa wa Mwanza, Angelous Rumisha.
Hata hivyo, upande wa mashtaka uliiomba mahakama kupangia tarehe nyingine kwa madai kuwa idadi ya mashahidi ilikuwa bado haijakamilika.
Ilielezwa kuwa kama upelelezi wa kesi hiyo utakuwa umekamilika, Novemba 4 mwaka huu upande wa mashtaka utaiomba mahakama ya mkoa kuihamishia katika Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza.
Mahakama ya mkoa haina mamlaka ya kisheria ya kusikiliza kesi za mauaji.
Inadaiwa kuwa Oktoba 13, mwaka jana, kati ya saa 7:00 na saa 8:00 usiku, katika eneo la Minazi Mitatu Kitangiri, katika Wilaya ya Ilemela, mkoani Mwanza, washtakiwa walimuua kwa kumpiga risasi Kamanda Barlow.

SOURCE: MWANANCHI