 
  
            
Mwenyekiti wa UVCCM, Sadifa Hamisi Juma (katikati) Katibu Mkuu wa CCM, 
Abdulrahman Kinana (kulia) wakiimba nyimbo ya chama hicho kabla ya 
kuanza kikao cha Baraza Kuu la jumuiya hiyo kilichofanyika White House, 
mjini Dodoma jana. Kushoto ni Katibu wa UVCCM, Sixtus Mapunda. Picha na 
Edwin Mjwahuzi 
            
Posted Jumatano,Oktoba30 2013 saa 8:15 AM
Baadhi ya wajumbe wa Baraza Kuu la Jumuiya ya 
Vijana wa CCM (UVCCM), wameanza kupanga upya mikakati ya kuwang’oa 
viongozi wa juu wa jumuiya hiyo baada ya kushindwa kwa mpango uliokuwa 
umepangwa kutekelezwa wakati wa kikao cha baraza hilo kilichofanyika 
juzi mjini Dodoma.
Wanamapinduzi walikuwa wamepanga kuwatoa 
madarakani Mwenyekiti wa UVCCM, Sadifa Juma Khamis na makamu wake, Mboni
 Muhita, lakini jaribio hilo
lilishindwa kutokana na kile kilichoelezwa kuwa ni
 wahusika kutojipanga vizuri, pia uwapo wa Katibu Mkuu wa CCM, 
Abdulrahman Kinana katika mkutano huo.
Kinana anatajwa kukwamisha mapinduzi 
yaliyokusudiwa kutokana na kauli yake aliyoitoa wakati akifungua mkutano
 huo kwamba haukuwa kwa ajili ya kuibomoa jumuiya bali kuijenga, hali 
ambayo iliwafanya wajumbe waliokuwa na ajenda ya kumng’oa mwenyekiti 
kunywea.
Hata hivyo, jana gazeti hili lilielezwa kuwa 
baadhi ya wajumbe hawakuridhika na hatua ya kutokujadiliwa kwa hali 
ilivyo ndani ya UVCCM, hivyo wameamua kujipanga upya ili kutekeleza azma
 yao ya kuwasulubu viongozi wao katika mkutano ujao.
Mmoja wa wajumbe wa kikao hicho alisema kumekuwa 
na woga unaowafanya viongozi wa juu wa UVCCM kutoruhusu kuwapo kwa 
ajenda zaidi ya moja katika vikao vya Baraza Kuu na kwamba huo ni 
utumiaji mbovu wa rasilimali za jumuiya.
“Kikao kimoja cha baraza kinagharimu zaidi ya Sh60
 milioni, lakini mwaka huu pekee tumefanya vikao vitatu kwa hiyo 
tumetumia zaidi ya Sh180 milioni. Fedha hizi zingeweza kugharimia mambo 
mengine kama uhaba wa kadi na kanuni za jumuiya kwenye ngazi za chini,” 
alisema mmoja wa wajumbe kutoka mikoa ya Kanda ya Kati, huku akiomba 
jina lake lihifadhiwe.
Alisema kwa mujibu wa kanuni za jumuiya hiyo, 
kikao cha Baraza Kuu kinapaswa kuwa kimoja kwa mwaka, lakini mwaka huu 
tayari wamefanya vikao vitatu ambavyo kimsingi havina tija kwani hakuna 
kilichojadiliwa kutokana na woga wa viongozi.
Mjumbe mwingine kutoka mikoa ya Kanda ya Kaskazini
 alisema jumuiya imeshindwa kuteua makamanda wa wilaya na mikoa kwa muda
 mrefu, pia kutofanya uteuzi wa wagombea wa nafasi za chipukizi katika 
ngazi za wilaya na mikoa.
“Mwakani tunakabiliwa na Uchaguzi wa Serikali za 
Mitaa, lakini cha ajabu hadi sasa tuna viporo vingi, mikutano kama hii 
ingetumika kufanya kazi hizo badala ya kujadili ajenda moja tu kama 
tulivyofanya Zanzibar mwezi uliopita na jana (juzi) hapa Dodoma,” 
alisema.
Hata hivyo, Katibu Mkuu wa UVCCM, Sixtus Mapunda 
akijibu hoja hiyo alisema: “Uhai wa jumuiya ni vikao, kwa hiyo siyo kosa
 kufanya vikao hata kama vitakuwa ni zaidi ya 10 kwa sababu katika vikao
 ndiko mambo muhimu yanakojadiliwa”.
Kuhusu uteuzi wa makamanda wa vijana wa wilaya na 
mikoa, Mapunda alisema kazi hiyo ilifanyika na kukamilika juzi katika 
kikao cha Kamati ya Utekelezaji cha jumuiya hiyo na kwamba suala la 
wagombea wa chipukizi nalo litakamilishwa.
SOURCE: MWANANCHI
Sarakasi za Sadifa
Uchambuzi wa kisiasa unaonyesha kuwa Sadifa 
alifanya mambo mawili makubwa katika kuwakabili wapinzani wake waliokuwa
 wamenuia kumng’oa katika nafasi yake.
Kwanza alikesha akiomba radhi katika vikao 
vilivyowahusisha wenyeviti wa UVCCM wa mikoa na baadaye wajumbe wengine 
wa Baraza Kuu na pili ni hatua yake ya kumteua hasimu wake kisiasa, Paul
 Makonda kuwa mmoja wa wakuu wa idara za umoja huo.
Wakati huo huo, Baraza la UVCCM, limeitaka 
Serikali kurejesha bungeni kwa hati ya dharura muswada wa marekebisho ya
 tozo ya Sh1000 kwa kila kadi ya simu.
Mapunda akizungumza na na waandishi wa habari jana
 alisema “Lengo ni kufanikisha malengo ya kufikisha mawasiliano ya simu 
kwa Watanzania wengi kwa haraka”.
Tozo hiyo ya Sh1000 kwa kila kadi ya simu, 
imetokana na sheria mpya ya fedha ya mwaka huu iliyopitishwa na Bunge . 
Hatua hiyo ya Serikali inalenga kukusanya Sh 178 bilioni katika Bajeti 
ya 2013/2014.
SOURCE: MWANANCHI
