Makamu wa Kwanza wa Rais, Maalim Seif Sharrif Hamad. 
            
    Na Mwinyi Sadallah, Mwananchi
Posted Jumatatu,Oktoba28 2013 saa 10:38 AM
Posted Jumatatu,Oktoba28 2013 saa 10:38 AM
Kwa ufupi
Kiongozi huyo wa UVCCM, alisema watu wa 
Tanzania Bara wanaoishi Zanzibar, si wakimbizi kwa mujibu wa Katiba ya 
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.
Wanasema Serikali inatumia fedha nyingi 
kugharimia matibabu ya kiongozi huyo nje ya nchini, kinyume na ahadi 
yake ya kutotibiwa nje.
Zanzibar. Mwenyekiti wa Umoja wa 
Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), Sadifa Juma Khamis amesema baadhi
 ya viongozi ndani ya Serikali ya Umoja wa Kitaifa, wameshindwa 
kutekeleza wajibu wao.
Amesema wajibu huo  ni pamoja na  kushindwa 
kutatua kero za madaktari na kusababisha kuzorota kwa huduma za afya 
visiwani humo. Sadifa aliyasema hayo jana alipokuwa akihutubia mkutano 
wa hadhara  katika Uwanja wa Vuga katika Mkoa wa Mjini Magharibi, 
Unguja.
“Serikali imekuwa ikitumia gharama kubwa 
kumhudumia kwa matibabu, Makamu wa Kwanza wa Rais, Maalim Seif Sharrif 
Hamad, itakumbukwa aliwahi kuwaahidi wananchi wa Zanzibar kuwa akiwa 
kiongozi atahakikisha anatibiwa hapa hapa badala ya kusafirishwa nje ya 
nchi,” alisema.
Wabara waishio Zanzibar
Kiongozi huyo wa UVCCM, alisema watu wa Tanzania 
Bara wanaoishi Zanzibar, si wakimbizi kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya
 Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.
Sadifa alisema wapinzani wanaohoji uhalali wa watu
 hao kuishi na kufanya kazi Zanzibar, hawafahamu haki ya  kila mtu 
kikatiba kwa maana ya kuwa huru kuishi na kufanya kazi katika sehemu 
yoyote ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Alisema ibara ya 11 na 26 ya 
katiba imeweka wazi kwa kila Mtanzania ana haki ya kuishi sehemu atakayo
 ndani ya Jamhuri ya Muungano.
Huku akishangiliwa na wanachama wa CCM alisema 
sera za ubaguzi hazitasaidia kujenga amani na umoja wa kitaifa baada ya 
kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Novemba mwaka 2010.
Naibu Katibu Mkuu wa UVCCM Zanzibar, Shaka Hamdu 
Shaka, alisema umoja huo umeamua kuchunguza kikundi cha watu wenye asili
 ya India ambao wamekuwa wakipinga misingi ya Mapinduzi na  Muungano wa 
Tanganyika na Zanzibar.
Alisema ni jambo la kushangaza kuona watu hao 
wakiwa katika mstari wa mbele kuhoji uhalali wa Muungano wa Tanganyika 
na Zanzibar, wakati hakuna muafrika anayeweza kwenda kuhoji uhalali wa 
harakati za ukombozi wa India au Iran kama hali ilivyojitokeza visiwani 
Zanzibar.
Alisema kitendo hicho hakikubaliki.
SOURCE: MWANANCHI
SOURCE: MWANANCHI
