Friday 6 September 2013

Tetesi kuhusu hali ya Muslim Brotherhood

                        
                                       Wafuasi wa Mohammed Morsi

Serikali ya Misri, imekanusha madai kuwa imeamua kufutilia mbali vuguvugu la Muslim Brotherhood.
Msemaji katika wizara ya maswala ya kijamii, alinukuliwa akisema kuwa wizara itafutilia mbali hadhi ya vuguvugu hilo kama shirika lisilo la kiserikali katika siku chache zijazo.
Lakini taarifa kutoka katika ofisi ya waziri mkuu Sherif Shawki, alisema kuwa waziri wa maswala ya kijamii bado hajatoa taarifa rasmi kuhusu uamuzi wake.
Maafisa wa kijeshi, wameanzisha msako mkubwa dhidi ya vuguvugu hilo tangu kuondolewa mamlakani kwa aliyekuwa rais na kiongozi wa chama hicho, Mohammed Morsi.
Mamia ya maafisa wakuu akiwemo Generali Mohammed Badie,wamezuiliwa kwa madai ya kuchochea ghasia na mauaji.
Mamia ya watu wanaotaka Morsi aachiliwe pia wameuawa kwenye makabiliano na maafisa wa usalama wanaosema kuwa harakati zao ni vitendo vya ugaidi.
Vuguvugu hili lenye miaka 85 liliharamishwa Misri mwaka 1954, ingawa likajisajili kama shirika lisilo la kiserikali,mnamo mwezi Machi.
Muslim Brotherhood pia lina tawi lake la kisiasa lililosajiliwa kama-chama cha Freedom and Justice kilichoundwa mwaka 2011 mwezi Juni baada ya mapinduzi ya Hosni Mubarak.

source: BBC Swahili