Saturday 28 September 2013

Wanamageuzi Katoliki wamtega Papa Francis

Papa Francis 
Na Mwandishi Wetu na Mashirika ya Umma

Posted  Septemba28  2013  saa 8:23 AM
Kwa ufupi
Wanamageuzi hao kupitia kundi lao lenye vikundi vidogo 100 vya Wakatoliki wanataka suala lao liwe sehemu ya mazungumzo baina ya Papa Francis na kamati yake ya ushauri yenye makadinali wanane yanayofanyika wiki ijayo.


Paris, Ufaransa. Harakati za kutaka mabadiliko makubwa ndani ya Kanisa Katoliki zimezidi kushika kasi baada ya kundi la waumini wanaojiita wanamageuzi kumwandikia barua Papa Francis, wakiomba akutane nao kuzungmzia mustakabali wa kanisa hilo.
Wanamageuzi hao kupitia kundi lao lenye vikundi vidogo 100 vya Wakatoliki wanataka suala lao liwe sehemu ya mazungumzo baina ya Papa Francis na kamati yake ya ushauri yenye makadinali wanane yanayofanyika wiki ijayo.
Papa Francis anatarajiwa kukutana na makadinali hao wanaounda Baraza la Ushauri kati ya Oktoba 1-2 mjini Vatican kwa lengo la kuangalia mageuzi katika uendeshaji wa kanisa hilo.
Hadi sasa, haijulikani endapo Papa Francis ataafiki ushauri wa wanamageuzi hao au la.
Katika mkutano huo, Papa Francis na bodi yake wanatazamiwa kuangalia sera mbalimbali zinazohusu uendeshaji wa kanisa hilo. Makadinali hao wanane wanatoka Italia,Chile,India,Ujerumani, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC), Marekani, Australia na Honduras.
Msemaji wa kundi hilo la wanamageuzi kutoka mataifa mbalimbali duniani, Rene Reid ameeleza kuwa matumaini yao ni kwa kiongozi huyo wa kanisa kukubali kukutana nao.
Kundi hilo lina Wakatoliki kutoka nchi mbalimbali zinazozungumza Kiingereza pamoja na Ujerumani, Austria, Ufaransa, Poland, Hispania na India.
Barua hiyo inaorodhesha mambo ambayo Papa Francis aliyechaguliwa Machi amekuwa akitaka yafanyiwe marekebisho na mengine ambayo tayari amepingana nayo.
Katika mahojiano mbalimbali wiki iliyopita, Papa Francis amezungumzia mambo ambayo angependa yafanyiwe marekebisho na kanisa,ingawa siyo yale yanayohusu mafundisho na kumsihi aishi kwa matendo ahadi zake.

SOURCE: MWANANCHI