Rais Jakaya Kikwete 
            
    Na Kelvin Matandiko, Mwananchi
Posted Jumatano,Septemba25 2013 saa 13:53 PM
Posted Jumatano,Septemba25 2013 saa 13:53 PM
Kwa ufupi
Oktoba 10 mwaka huu umoja wa vyama vya siasa 
vya CUF, Chadema, NCCR Mageuzi, na vingine kadhaa visivyokuwa na wabunge
 wameitisha maandamano nchi nzima kuendelea kushinikiza rais asikubali 
kusaini muswada huo.
Kila upande miongoni mwa wanasiasa 
unaonzungumzia Katiba Mpya unajificha kwenye kivuli cha masilahi ya 
wananchi. Chama tawala, CCM, kinasema kinatetea maslahi ya wananchi na 
wapinzani nao wanadai kutetea maslahi hayo hayo.
Swali kuu, ni nani kati yao hasa anatetea 
wananchi? Mwenye majibu ni Rais Jakaya Kikwete anayetupiwa mpira wa ama 
kusaini au kutosaini sheria ya marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya 
Katiba, ambayo inaaminika kuwa ama inaweza kuipatia Tanzania Katiba bora
 au bora Katiba.
Wakati upande wa CCM wamekwishatumia nguvu ya 
wingi wao kwa kupitisha sheria hiyo ndani ya Bunge, wapinzani wameanza 
kuunganisha makundi mbalimbali ya jamii kuikataa, huku wakisema “Katiba 
Mpya lazima ipatikane kwa gharama yoyote.”
Miongoni mwa makundi yaliyokutana na viongozi 
upinzani, ni wanahabari, viongozi wa dini, wasomi, wanaharakati na sasa 
wameanza kufanya mikutano ya wananchi wa kawaida.
Pamoja na kauli “katiba kupatikana kwa gharama 
yoyote”, viongozi hao wa upinzani waliokutana na wananchi jijini Dar es 
Salaam, wameweka bayana kuwa iwapo Rais Kikwete hatasikiliza hoja za 
umoja wao na kuachana na sheria hiyo, mapambano yataendelea kufanyika 
ndani na nje ya Bunge, lakini hawataingia katika Bunge Maalumu la 
Katiba.
Vilevile Oktoba 10, mwaka huu, umoja wa vyama vya 
siasa vya CUF, Chadema, NCCR Mageuzi, na vingine kadhaa visivyokuwa na 
wabunge wameitisha maandamano nchi nzima kuendelea kushinikiza rais 
asikubali kusaini muswada huo.
Viongozi hao Freeman Mbowe (Chadema), James Mbatia
 (NCCR-Mageuzi), Profesa Lipumba(CUF), na akina Fahmi Dovutwa (UPDP), 
Emmanuel Makaidi (NLD) na Said Miraji (ADC) wanasema hawatarudi nyuma 
katika suala hili kwa kuwa lina maslahi ya wananchi.
Mbowe anaweka msisitizo: “Kosa kubwa katika kudai 
haki ni woga. Hatutapata Katiba Mpya kama tutaendelea kuwa taifa la watu
 wenye hofu. Hatutakubali kurudi nyuma katika mchakato huu na endapo 
rais atasaini muswada huu, tutajitoa kabisa katika harakati za kuandaa 
Katiba na badala yake tutaendelea kupiga kelele mpaka dunia yote itambue
 tunataka Katiba Mpya yenye tija kwa Watanzania.
Kwa vyovyote vile, mtu pekee wa kutegua 
kitendawili hiki ni Rais Kikwete, ambaye tayari viongozi wa CCM na 
Serikali yake wamekuwa wakimwomba asaini sheria hiyo na pengine kumtisha
 kuwa iwapo atasaini sheria hiyo machafuko yatazuka bungeni.
Marekebisho ya sheria hiyo yanaelezwa kuwa 
yamepitishwa bila kuwashirikisha Wazanzibari, wakati kwa ushirika wao 
wana haki sawa na Tanganyika ndani ya Muungano.
Inaelezwa pia kuwa marekebisho hayo yameweka 
wajumbe wa Zanzibar katika Bunge Maalumu la Katiba kuwa asilimia 36 ya 
wahumbe wote wakati nchi hiyo licha ya odogo wake kijiografia, ina haki 
sawa na Tanganyika. Usawa huo unaonyeshwa tu kwenye idadi ya wajumbe wa 
Tume ya Marekebisho ya Katiba ambayo inaundwa na wajumbe 15 kutoka kila 
nchi.
Pamoja na hoja ya kupinga Rais kuteua wajumbe 166 
wasiokuwa wabunge, muswada huo unadaiwa kuwa, kinyume na katiba ya sasa,
 umeruhusu iwapo theluthi mbili za kila upande hazikupatikana kwa mara 
mbili katika Bunge Maalumu la Katiba, kwa mara ya tatu itakuwa kwa 
uwingi wa kawaida (‘simple majority’)  ya kila upande.
SOURCE: MWANANCHI
Sheria yenye vipengele hivyo ilipishwa na wabunge wa CCM baada 
ya wale wa upinzani kutoka nje ya Bunge kupinga kuwa sehemu ya uamuzi 
hayo na tangu kuanza kwa mvutano huo Rais Kikwete yuko kimya, bila shaka
 akitafakari ni njia ipi yenye unafuu aweze kupenya ili abaki na heshima
 yake na usalama ndani na nje ya chama chake.
Kwa upande wa CCM na Serikali yake, pia shinikizo 
si haba. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mahusiano, Uratibu wa Sera, 
Stephen Wasira yeye anakipinga hoja zote za kumshinikiza asisaini mswada
 huo. Anasema endapo Rais hatakubali kusaini mswada huo, taifa litaingia
 kwenye mgogoro wa kikatiba.
Naye Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe 
anaongeza kuwa mswada huo ulipitishwa kwa haki na demokrasia ya kuhesabu
 kura ya wabunge, hivyo Rais anapaswa kuusaini.
Mitego aliyovuka JK
Huu si mtego wa kwanza  kwa Rais Kikwete tangu kuanza kwa mchakato wa Katiba Mpya.
Mhadhiri mstaafu wa Chuo Kukuu cha Dar es Salaam 
(UDSM), Dk Azaveli Lwaitama anasema hatua ya Watanzania kutaka Katiba 
Mpya ilipingwa na viongozi wengi wa CCM,  lakini Rais Kikwete akafikia 
uamuzi wa kukubaliana na ombi hilo.
Mbali na hatua hiyo, Dk Lwaitama anasema Rais 
Kikwete aliamua pia kutofautiana na chama chake baada ya kuagiza mjadala
 wa sheria ya mabadiliko ya Katiba urudishwe bungeni kwa mara ya pili 
ili kuleta maridhiano.
“Ninaamini huu pia ni mtego mwingine anaokutana 
nao Rais kutoka ndani ya chama chake, ninaamini kama kiongozi anayepima 
hoja za Katiba kwa mustakabali wa kizazi kijacho, atafanya uamuzi wa 
kutokusaini muswada huo,” anasema Lwaitama.
Kwa upande wake, Askofu Mkuu wa Kanisa la Full 
Gospel Bible Fellowship, Zacharia Kakobe anasema kuwa Rais Kikwete 
akisaini muswada huo, Watanzania watajua kuwa hana nia njema na taifa 
kwa kuwa wengi wanaupinga.
Hofu ya Kakobe juu ya muswada huo, anasema 
inatokana na mamlaka ya Rais kuteua wajumbe nje ya majina 
yaliyopendekezwa. “Sina hakika kama CCM ina dini ya kutuwakilisha hata 
sisi, ni hatari sana kuiteka Katiba ya Watanzania, ninamwomba Rais 
usikubali mtego huo,” anasema Kakobe.
Naye kiongozi wa maimamu nchini, Sheikh Rajab 
Katimba anasema Katiba Mpya ni kwa ajili ya Watanzania na siyo chama, 
dini au kundi lolote.
 “CCM ilikataa Katiba isianzishwe, Jakaya Kikwete 
pekee alijipiga kifua akakubali, ingawa alishambuliwa na chama chake, 
kwa hiyo ninaomba kwa msimamo aliotumia awali, asisaini muswada huo,” 
anasema Shekh Katimba.
SOURCE: MWANANCHI
