Friday 6 September 2013

Kambi ya upinzani bungeni kutounga mkono Muswada wa katiba

Kambi ya upinzani bungeni imesema haitaunga mkono muswada wa sheria ya marekebisho ya katiba ya mwaka 2013.
          
 Kambi ya upinzani bungeni imesema kutokana na mtafuruku uliotokea bungeni kwa kutolewa nje kiongozi wa kambi hiyo Mh. Freeman Mbowe amesema hawaungi mkono muswada  wa sheria ya marekebisho ya katiba ya mwaka 2013 kwa kuwa  haiwatendei haki watanzania .
Akizungumza katika mkutano na vyombo vya habari katika ukumbi wa Pius Msekwa bungeni mjini Dodoma kuhusiana na mtafuruku uliotokea bungeni kiongozi huyo wa kambi ya upinzai bungeni Mh Freeman Mbowe amesema hawatashiriki katika mjadala huo kwa kile walichodai kuwa chama cha mapinduzi (CCM) kina ajenda ya siri na kushiriki kwao hawatakuwa wanawatendea haki watanzania
Akizungumzia juu ya kile kinachoonekana kwa sasa kuwa ni uhusiano mwema baina ya chama cha wananchi (CUF) na Chadema,mbunge wa Mkanyageni kupitia CUF  Mh Habib Mnyaa amesema siasa haina adui wala rafiki wa kudumu na hivo wameungana na Chadema katika kutetea haki,usawa na maslahi ya wananchi wa Zanzibara na wale wa Tanzania Bara
Katika tukio jingine  wanasheria wa masuala ya haki za binadamu wamesema kilichotokea bungeni ni kutokana na kitendo cha naibu spika kuchelewa kutoa majibu ya miongozo kama ilivyoombwa na baadhi ya wabunge na kuwafanya wabunge wa upinzani kuona wanaburuzwa na kuamua kutoka nje na kuongeza kuwa hawakufurahishwa na jambo hilo kwa kile alichodai kuwa mawazo yawachache yanapigwa kumbo.

source: ITV- Daima