Lazaro Nyalandu 
            
Na Sharon Sauwa na Habel Chidawali,Mwananchi
Posted Jumatano,Oktoba30 2013 saa 24:0 AM
Posted Jumatano,Oktoba30 2013 saa 24:0 AM
Kwa ufupi
“Inashangaza sana kuwa wale wanaotajwa hawachukuliwi
 hatua, lakini wananchi wanazidi kuteseka… Mathalani, zipo taarifa kuwa 
wakuu wa polisi katika mikoa inayopakana na Mbuga ya Serengeti ndio 
waratibu wa shughuli za ujangili, lakini hatujasikia hao wakichukuliwa 
hatua,”
Dodoma. Wabunge jana 
walichachamaa na kushinikiza kutolewa kwa orodha ya vigogo 
wanaojihusisha na ujangili wakati wa kikao cha kwanza cha mkutano wa 13 
wa Bunge unaofanyika mjini Dodoma.
Wabunge hao walitaka kutajwa kwa majina ya mawaziri, viongozi wa Serikali na wabunge wanaojihusisha na biashara hiyo.
Baada ya kumalizika kwa kipindi cha maswali na 
majibu, Mbunge wa Mwibara (CCM), Kangi Lugola, aliomba mwongozo, 
akiitaka Serikali kuwataja hadharani na kuwachukulia hatua viongozi wake
 na wanasiasa, wakiwamo mawaziri na wabunge, ambao wanatajwa kuhusika na
 vitendo vya ujangili nchini.
Lugola aliomba mwongozo wa Naibu Spika baada ya 
kutoridhishwa na jibu lililotolewa na Naibu Waziri wa Maliasili na 
Utalii, Lazaro Nyalandu, wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa 
Kahama (CCM), James Lembeli.
Katika jibu hilo, Nyalandu alilieleza Bunge kuwa 
Operesheni Tokomeza inayolenga kukomesha vitendo vya ujangili nchini 
bado inaendelea, lakini alishindwa kulieleza Bunge ni nani hasa 
wamebainika kuhusika na vitendo hivyo.
Lugola, hata hivyo, aliitaka Serikali kuwasilisha ripoti bungeni kuhusiana na utekelezaji wa operesheni hiyo.
“Tangu Aprili tumekuwa tukipewa majibu mepesi kuhusiana na operesheni hii, wakati suala hili si la masihara,” alionya Lugola.
Lugola alisema kuwa taarifa zimewataja watu 
wanaohusika na vitendo hivyo wakiwamo viongozi serikalini, mawaziri 
pamoja na wabunge, lakini tangu operesheni hiyo ilipoanza hakuna yeyote 
miongoni mwa hao wanaotajwa ambaye amekamatwa isipokuwa wananchi wa 
kawaida.
Alisema operesheni hiyo imekuwa ikiendeshwa kwa 
unyama kwani wanaokamatwa hupigwa na kuteswa bila ya ushahidi 
unaoonyesha kuhusika kwao na vitendo vya ujangili.
“Inashangaza sana kuwa wale wanaotajwa 
hawachukuliwi hatua, lakini wananchi wanazidi kuteseka… Mathalani, zipo 
taarifa kuwa wakuu wa polisi katika mikoa inayopakana na Mbuga ya 
Serengeti ndio waratibu wa shughuli za ujangili, lakini hatujasikia hao 
wakichukuliwa hatua,” alisema.
Kabla ya Naibu Spika kutoa majibu ya mwongozo 
ulioombwa na Lugola, Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, 
Uratibu na Bunge), William Lukuvi, alisimama na kukiri kuwapo kwa 
vitendo vya utesaji wa watu wanaokamatwa katika operesheni hiyo.
Alitolea mfano tukio la kukamatwa kwa msaidizi 
wake jimboni ambaye alipigwa na kuteswa na askari hao kabla ya kuachiwa 
baada ya kushikiliwa kwa siku moja, huku akionyesha kuwa ushahidi wa 
tukio hilo anao kwenye simu yake.
SOURCE: MWANANCHI
Serikali yakiri tatizo
Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamsi
 Vuai Nahodha akizungumza bungeni kwa niaba ya Waziri Mkuu, alikiri 
kuwapo fununu za wanasiasa ambao wamekuwa wakijihusisha na biashara hiyo
 na kusema Serikali italifanyia kazi jambo hilo.
Nahodha aliwataka Watanzania kuwa watulivu wakati 
vyombo vya Ulinzi na Usalama vinaposhughulika na kusafisha tatizo hili 
na kuonya wanasiasa kuacha kutoa shinikizo kwa kutumia nguvu zao za 
kisiasa.
SOURCE: MWANANCHI

