Sunday 9 June 2013

SPEECH BY Dr. A. Lwaitama


NAFASI YA VIJANA WASOMI WA TANZANIA NA KATIBA MPYA (RASIMU YA KATIBA) KWENYE MAENDELEO YA TANZANIA
Na Mwalimu Azaveli Lwaitama
+255784432696

Ndugu Watanzania mliokusanyika hapa Oslo leo
Ndugu marafiki wa Wantanzania mlipo katika sherehe hii,
Kwanza naomba niwashukuru kwa kunipa mwaliko wakuhudhuria sherehe yenu bila kuchangia chochote.  Nasikitika na naomba kusamehewa kwa kukosa kuwepo uso kwa uso ingawa hotuba hii inawaonesha nipo nanyi kiroho.  Nasikitika kukosa kuwepo uso kwa uso maana niliambiwa kutakuwepo chakula kingi na vinyaji vya kutosha na mimi kwa msosi ndio mwenyewe, bia  na mvinyo  pia nakunywa ingawa hulewa mapema na kuanza kusinzisinzia.

Nasikitika kuukosa uhondo wa mapochopocho, ulaji na kinywaji. Nawashukuru Kwa dhati kunialika hata kama nimeshindwa kufika. Nimeshindwa kufika kwa kuwa  naondoka kesho  Jumapili asubuhi sana  na inabidi, kama  mnavyojua, niwe kiwanjani walau saa 10 usiku wa leo hii Jumamosi ( ingwa kwa Kimombo tunasema  saa 10 asubuhi ya Kesho Jumapili!).  Na masikini baba yake mwenyeji wangu alipata udhuru na kushindwa kupata muda wa kuweza kunileta hadi huku jijini Oslo halafu aniendeshe kwa gari lake binafsi kurudi karibu mwendo wa zaidi ya saa na zaidi usiku wa manane kunipeleka uwanja wa ndege wa Gardermoen, Oslo ambao upo kati kati ya huku jijini Oslo na huko kwao nilikokaribishwa kwenye mji mdogo wa HAMAR.

Ndugu Watanzania wenzangu ,
Ndugu marafiki wa Wantanzania,
Kwa kweli ingebidi aondoke kwao Hamar  saa 2 hivi usiku  na kunileta huku Oslo  jijini ili nifike hapa kwenye saa 4  halafu anirudishe nusu mwendo wa kurudi kwao na kuniacha uwanja wa ndege wa Gardermoen, Oslo usiku wa manane   na ende kwao Hamar na kufika pia usiku wa manane.. Hata na mimi nilikubali ingewa si uungwana kumwambia kunifanyia hisani kiasi hicho.  Yeye ni baba yake Dr AnnaMartha van Grieken ambaye alikuwa mwanafunzi wangu wa shahada ya uzamivu (PhD) aliyoipata Chuo Kikuu cha  Dar es Salaam miaka mitano iliyopita. Aliniomba nimtembelee katika shule anayofundisha ya Sekondari ya Juu (Upper Secondary School) ambayo nimeizungumzia katika makala yangu iliyochapishwa katika gazeti la kila siku la The Citizen Juamatano hii ya juzi tarehe 05.06.2013.

Ni moyo wa ukarimu  wa mwanafunzi wangu wa shahada ya uzamivu (PhD) wa zamani ulionipa fursa kutembelea shule za chekeche, msingi na sekondari hapa Norway ili kujifunza mengi iwezekanavyo kuhusu mfumo wa elimu katika nchi ya Norway  kwa lengo la baadaye kusambaza elimu hiyo  niliyopata kwa Watanzania wenzangu kupitia machapisho kama ile makala yangu kwenye gazeti la The Citizen juzi Juamatano. Nitaendelea kutoa machapisho na kuzungumza juu ya niliyojifunza kuhusu Norway nikirudi Tanzania.


Ndugu Watanzania
Kwa wale ambao wanapenda kuendelea kuchota kutoka kwenye elimu  niliyopata hapa  Norway kwa muda wa wiki moja  nawakaribisha kufuatilia   juu ya nitakachokuwa kuandika (naandika) na kuzungumza kwa kutafuta jina langu kwenye Googles na au kutafuta nilichoandika kwenye  The Citizen  Tanzania kila Jumatano au kusikiliza kwenye Youtube kipindi changu cha kila Ijumaa kiitwacho Hoja ya Mwalimu Lwaitama  kinachorushwa na SIBUKA Tv na Radio ambayo inasikia kwa kingamuzi sehemu nyingi Tanzania. 

Nyie pia nawaomba mfanye bidii kwenye masomo yaliyowaleta hapa na kurudi nyumbani na maarifa na stadi za ujuzi mbali mbali   wenye kusaidia watu wetu kule nyumbani Tanzania wafanye kazi zao za kila siku  kwa tija. Hata wale mtakaojikuta mmezamia hapa kwa kuoa au kuolewa hapa mimi sina matatizo na nyie ili mradi kukaa kwenu hapa kunafanywa kuwa kwa manufaa kwa ndugu zenu waliobaki nyumbani. Muhimu kuliko chochote soma kwa bidii na jifunze yote mazuri yaliyopo mbele yako hapa ili uwe mtu mwelevu zaidi na ambaye unapata heshima ya kujitambulisha kama mweledi wa mambo katika fani yako yoyote ile.  

Ndugu Watanzania mliokusanyika
Chonde chonde mtu hasitoke hapa na dhana kuwa ili kujinasua na umasikini wake  kama mtu binafsi sherti kujikomba kwa wana siasa ili wakupe vyeo vya kisiasa vya kuteuliwa au kupigiwa kura na watu ulio waonga vijikanga na na (imerudiwa) vijichumvi! Hapana jamani!!

Ndugu Watanzania wenzangu,

Toka hapa na weledi wa juu katika fani yako ili waajiri wakutafute popote duniani ili wakuajiri katika fani yako uliyosomea. Toka hapa na jeuri yenye unyenyekevu itokanayo na kujiamini kuwa yapo mambo unayoyajua na watu  mwisho wa siku watakutafuta au ukiwaonesha unachoweza  watakuajiri au kukupa kazi kwa vile wewe ni mjuzi wa mambo katika fani yako! Chonde chonde toka hapa na ujuzi fulani utakao kukomboa na utumwa wa daima kujikomba kwa wana siasa, wawe wa chama tawala au wa vyama vya ushindani!!!. Ukitaka kujiunga na vyama vya siasa basi jiunge huku viongozi wao wakijua kuwa kuishi kwako hakutegemei hisani zao, ng’o!!!

 Sasa ngoja nimalize salamu zangu kwenu kwa kugusia juu ya mada niliyoelezwa mlitaka nizungumzie leo.  Tume ya Rais ya Mchakato wa Kuandika Katiba  Mpya, Tume ya Jaji Warioba, imetoa Rasimu ya Katiba hiyo Mpya na niliombwa nizunguzie juu ya nafasi ya vijana wasomi wa Tanzania na katiba Mpya katika maendeleo ya Tanzania.  Hii ni mada pana lakini nitafupisha maneno kwa kusema mambo matatu yafuatayo.

Kwanza, kama vijana wasomi hoji kila kitu kwa kunukuu matokea ya utafiti na ushaidi wakujenga hoja  na jiepushe na tabia ya kukubalina na kila kitu kisemwacho  na wakubwa wako    kwa malengo ya kujikomba kwao ili ujinufaishe binafsi.  Nafasi ya vijana wasomi ni kusaka elimu   na baadaye kuisambaza ili Tanzania na Bara la Afrika  liondokane na kuchekwa kama watu omba omba  waliopewa baraka ya rasilimali watu na  vitu kama madini   lakini  tumelala usingizi wa pono wanongojea kuvulia na kuliwa na wavuvi wenye weledi!

Ndugu Watanzania wenzangu
Rasimu ya Katiba mpya  imetoka, ina mapendekezo mengi  ya kuiondoa Tanzania kwenye mifumo ya utawala  ya miungu mtu  na polepole kutupeleka kwenye mifumo ya utawala ya uwajibikaji na uwazi huku wengi wakishiriki katika kutoa  maoni juu ya lipi  lifanyike ili kuendesha shughuli zetu za uzalishaji na usambazaji hudumu wenye ufanisi na tija. Nafasi ya vijana wasomi ni kuhoji kila ibara iliyomo kwenye Rasimu hii kuona kama haiwezi kuboreshwa zaidi. Si kazi ya vijana  wasomi kusifia yaliyoisha pendekezwa na kulala usingizi wa pono kungojea kuvuliwa na kuliwa na wavuvi welevu au  wezi  wa matokeo ya uvuvi wa wengine lakini amabo  ni wajaja wa kuvuna wasichopanda!!!  Hiyo ndiyo nafsi ya vijana wasomi, tena waliosafiri masafa marefu hadi Oslo Norway kuupata usomi wenyewe!!! Nafasi ya vijana wasomi nikujikita kwenye tafakuri tunduizi (crititical thinking)  siyo kuwa mazezeta wanosema “Ndiyo” kwa kila kitu au kuwa na maono na dira  za muda mfupi kuhusu maswala  kama  ya  elimu  na lugha ya kufundishia,   muundo wa  Muungano wa Tanzania,  na utawala  wa majimbo.

Jambo la pili ninatamani kugusia ni kuhusu nafasi ya vijana wasomi katika kutetea uboreshaji wa sehemu ya Rasimu ya Katiba Mpya inayozungumzia juu wa Muundo wa Muungano.  Rasimu inapendekeza kuwepo muungano wa serikali tatu: ya Shirikisho yenye kuongozwa na Rais na Makamu Rais, na  mbili kwa kila washirika wa Muungano wawili, Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar  zitakazo ongozwa na Rais pia. 

Ndugu Watanzania wenzangu
Katika hili na waasa vijana wasomi wang’ag’anie kuendelea kuwepo kwa utaifa wa TANZANIA na kutokuvunjwa kwa MUUNGANO huu pekee AFRIKA uliodumu miaka 49.  Vijana wasomi wawe tayari kuboresha mapendekezo yaliyotolewa kwa kutaka kuwepo Rais na makamu Rais MMOJA tu katika Jamuhuri ya Muhungano ya Tanzania, RAIS wa SHRIKISHO ya JAMUHURI YA MUNGANO YA TANZANIA. Serikali za Washirika wa MUUNGANO huu, ya Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar ziongozwe na MAWAZIRI WAKUU, ili baadaye Shirikisho la Afrika Mashariki litakapo zinduliwa siku za karibuni basi tuwe na MAWAZIRI WAKUU 6 yaani wa ZANZIBAR, TANZANIA BARA, RWANDA, BURUNDI, UGANDA, na KENYA.
Nayasema haya kwa vile mimi ni muumini asiyekubali kuyumbishwa, wa itikadi ya Umajumui wa Kiafrika (Pan Africanism). Mimi natoa maoni yangu lakini najua na wengine wanaweza au kuniunga mkono au kunikatalia maana hiyo ndiyo demokrasia. Ikiwa ninachotetea kikikataliwa na hakuna madhara yatayotokea huko mbele ya safari itakuwa ni safi tu. Ikiwa nikishauri kitu watu wakakikataa na baadaye wakadhurika,  walau  mimi nitasema nilisema na  nafsi yangu itakuwa  na amani . 




Ndugu Watanzania wanzengu,
Mzee Abeid Karume aliweza kuwaongoza Wazanzibari wakakubali ushauri wa kuwa na   Muungano lakini leo wanao viongozi wengine wanaowashauri kutengana kuna masilahi kwa Wazazibari, kazi kwao kutafakari. Pia  kuna baadhi ya watanzania wa  Bara wengine wanadhani kuungana na Zanzibar  si lazima lakini mimi nafikiri itakuwa  haina usalama sana   kwa Tanzania Bara kuwepo Zanzibar  yenye  kuwa Kuwait ya Afrika Mashariki, yenye  jeshi lake  linalodhibitiwa na Uingereza na Marekani na  labda yenye  kuwa na  vituo vya kijeshi  vya Marekani,  huku viongozi wake wakijifanya eti Wazanzibari wote ni Waislamu kama vile wanavyofanya  viongozi wa  Kuwait au Oman...
Nakumbuka wapo Wazanzibari wengi wenye biashara zao Tanzania Bara na wenye mahusiano ya karibu na watu wa Tanzania Bara yanayosukumwa na ufuasi wa  dini moja ya Kiislamu au kupeana mikopo ya kuanzishia biashara..Wote hawa ni WATANZANIA na  wanayo haki kumiliki  ardhi Tanzania Bara na kujisikia  wako nyumbani. Mheshiwa Waziri  wa Afya   wa sasa aliwahi kuwa Mbunge jimbo  moja hapa Tanzania Bara  na baadaye karudi  Zanzibar na kuchanguliwa  Ubunge jimbo la Zanzibar na sasa ni Wazir wa Afya kwenye serikali ya Muungano inayoshughulikia mambo ya afya Tanzania Bara. .Mzanzibari anayedhani kuna manufaa kwa Wazanzibari  katika kufuta utaifa wa UTANZANIA nakufufua utambulisho wa Utanganyika sina  hakika amekaa na  kufikiria sana juu ya madhara ya kufufua utambulisho huo….Labda kama ni Mzanzibari anayeishi Omani au Kuwait kwa sasa na   hana mahusiano na Wazanzibari wenzake walio na mahusiano ya karibu na  Tanzania Bara.
Vile vile, kiulinzi na usalamana mtengamano kati ya waumini wa dini mbali mbali Tanzania Bara unasaidiwa kwa kuwepo dola moja la Tanzania. Watanzania Bara wanaodhani ulinzi na  usalama wa Tanzania Bara  utakuwa wa  gharama zile zile kama za sasa  ambapo kuna uraia wa Tanzania moja,  tuna jeshi  la ulinzi,  usalam na polisi moja ya dola moja  la taifa  moja   la UMAJUMUI wa KIAFRIKA la Tanzania, lisilo mbagua mtu kwa uzawa wake wala nasaba yake kuhusisha  nasaba za Asia au Ulaya, Niinashaka  kama  kweli hawa  wanao shabikia kurudi kwenye utambulisho wa UTANGANYIKA  tuliopachikwa  na wakoloni wa Kiingereza baada  ya sisi  kuitwa GERMAN EAST AFRIKA na Wagerumani  hadi 1919,  wamekaa nakutafakari kwa kina  juu ya jambo  ili kama  alivyo kuwa amefanya Mwalimu Nyerere.
 Ndugu Watanzania wanzengu,
Kinachounganisha Mzanzibari wa uzawa wa Urabuni au Uhindini ni kukubali kuitwa MUAFRIKA, au siyo? Kinachounganisha Mhehe wa Iringa   na Mhaya wa Bukoba na Muha wa Kigoma ni kukubali kuitwa MUAFRIKA, au siyo? Hivi ukianza kushabikia kuvunja nchi ya Tanzania iliyodumu zaidi ya miaka 49 (1964-2013) na kushabikia Utanganyika uliodumu miaka takribani 45 ( 1919-1964) (ambayo miaka zaidi ya 42 yake ilikuwa chini ya utawala wa kikoloni wa Waingereza na inawezekana Watanganyika wengi HAWAKUJITAMBUA kuwa walikuwa Watanganyika!) , una huhakika gani kuwa hii Tanganyika itakayo fufuliwa na wanasiasa wachovu wa kizazi hiki  cha mafisadi waliojaa udini na ukabila haitamegeka pia vipande vipande kwa misingi ya ukabila na udini?
Kinachoweza  kutuunganisha leo  na jana  hapa  Tanzania ni kujitambuwa kuwa sisi ni WAAFRIKA, na UTANZANIA ni  kituo cha kati kuelekea utambulisho ulio imara  na  wenye mashiko zaidi  wa UAFRIKA MASHARIKI na UAFRIKA  WA BARA ZIMA. Hayo ndiyo mawazo  yangu na mimi si Napoleon au  Bismark  au Musolini, kwa hiyo niko tayari kukaa kwa huzuni kwa kukataliwa maoni yangu ninayodhani ni sahihi! NJE ya UZALENDO wa UMAJUMUI wa KIAFRIKA hakuna uzalendo mwingine zaidi ya ushabiki wa kibaguzi wa kidini na kikabila!!! I am an Afrikan! I am an East African! I am a Tanzania! I refuse to return to being a Tanganyikan after 49 years of liberation!!!
Ndugu Watanzania wanzengu,
Jambo la tatu ninalotaka kugusia ni kuhusu nafasi ya vijana wasomi katika mchayo wenyewe wa kuandika Katiba Mpya. Tujikumbushe kuwa kutolewa Kwa Rasimu ni hatua moja muhumu lakini njia bado ni ndefu na hatujafika kwenye Katiba Mpya.   Vijana wasomi wapaze sauti zao sasa hivi, wiki hii na mwezi huu kunadi marekebisho ya Sheria iliyoanzisha mcahakato huu ili vifungu vinavyoaanisha nini liwe Bunge la Katiba litakalo pendekeza Rasimu ya Mwisho itakayo pigiwa kura ya maoni liwe si ili linaloainishwa kwenye Sheria kwa sasa ambalo litakuwa limejaa Wabunge na  Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kwa zaidi ya dheluthi mbili.
 Hivi karibuni Kamati Maalum ya Katiba iliyondwa na Kituo cha Haki za Binadamu Tanzania yaani LHRC kimetoa taarifa ifuatayo kwa vyombo vya habari:
 “Kwa mujibu wa Kifungu 22 cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya mwaka 2011 (Sura ya 83) Bunge la Katiba limetamkwa kuwa na wajumbe wafuatao; ambao jumla yao ni wajumbe 604:
(b)               Wajumbe wote wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar (yaani tunaweza kuwaita wabunge wote wa Bunge la Zanzibar) ambao jumla yao ni 81.
(c)                Wajumbe wengine wapatao 166 ambao watateuliwa na Rais kutokana na makundi yafuatayo: Asasi sizizo za kiserikali (NGOs), Taasisi za kidini (FBOs), Vyama vyote vya siasa venye usajili wa kudumu, Taasisi za Elimu ya Juu, Makundi ya watu wenye mahitaji maalum, Vyama vya wafanyakazi, Vyama vinavyowakilisha wakulima,Vyama vinavyowakilisha wafugaji, Makundi mengine yoyote yale ya watu (yakitumia jina lolote) ili mradi yawe na malengo ya aina moja.
Ni maoni thabiti ya Kamati yetu kuwa uundaji wa Bunge la Katiba lenye wajumbe waliotajwa hapo juu utakuwa ni upotezaji wa muda usiozingatia maslahi ya nchi na watu wake kwa kuwa Bunge hilo halitakuwa tofauti na Bunge la sasa kwa kuwa wajumbe walio wengi (zaidi ya asilimia 72) watakuwa ni wabunge wote kutoka Bunge la Muungano na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar.”

Ndugu Watanzania wanzengu,
Mimi ni mmoja wa wajumbe wa wajumbe wa Kamati hiyo Maalum iliyoundwa na Kituo cha Haki za Binanadamu na ninawaasa vijana wasomi wapaze sauti kudai marekebisho ya Sheria ya Mchakato wa Kuandika Katiba Mpya ili walau  wajumbe wa Bunge la Katiba watakao tokana na Bunge la Jamhuri la sasa pamoja na Baraza la Wawakilishi la saa , wasizidi THELUTHI MOJA, na  wajumbe wengine wa BUNGE MAALUUM LA KATIBA , yaani theluthi mbili zilizobaki, «  zitokane na wananchi na wadau walio nje ya mfumo wa vyama vya siasa ». Vijana wasomi walione hili na kulishupalia  kama kweli tunataka Mazuri yaliyo katika Rasimu hii yajitokeze kwenye Rasimu itakayopigiwa kura ya maono baada ya kupitishwa na BUNGE MAALUUM LA KATIBA. Vijana wasomi lazima wajue kuwa  ni lazima  « kupata Katiba mpya ambayo haitafuata misingi ya kiitikadi ya chama fulani na ambayo itazingatia misingi ya upatikanaji wa Katiba yenye kuleta tija na kuipeleka nchi hii katika hatua ya juu ya maendeleo.  
Ndugu Watanzania mliokusanyika hapa Oslo leo,
Ndugu marafikiwa Wantanzania manaowasidikiza katika sherehe hii,
Natamani kusema mengi lakini nafikiri tayari nimepunguza sana muda wenu wa kula , kunywa na kujirusha. Nawashuru kwa kuyasikiliza maoni yangu juu nafasi ya vijana  wasomi wa Tanzania kna Katiba Mpya katika Maendeleo endelevu ya Tanzania na Bara la Afrika kwa ujumla.  Jitaidini  basi ndugu zangu mzidue Mwalimu Julius Nyerere wa zama zenu miongoni mwenu  kwa kuzingatia ushauri wa  kuwa  wadadidisi na weledi.
Mungu ibariki Tanzania
Asantteni sana!!!
Mwl. Azaveli Lwaitama
Kringsjågrenda 1
Oslo, Norway,
8 Juni 2013