Monday 12 August 2013

Simulizi ya shuhuda wa tindikali

 


Posted  Jumapili,Agosti11  2013  saa 16:23 PM
Kwa ufupi
Kuongezeka kwa ukubwa wa jeraha la kumwagiwa tindikali kati ya mmoja wa waathirika wawili raia wa Uingereza, kumeelezwa kumetokana na kumwagiwa maji machafu wakati wa kuwasaidia wasichana hao.


Uingereza, London
Gazeti la Uingereza la Daily Mail toleo la jana, liliripoti kuwa watu walioonekana kukata tamaa wakati wa kutoa msaada kwa wasichana hao, kwa nia njema walitumia maji machafu kumsafisha mmoja wa majeruhi.
Taarifa zaidi kuhusiana na tukio la kihalifu pia zilieleza kuwa wasichana, Katie Gee na Kirstie Trup, wote wakiwa na umri wa miaka 18, waliwaona waliowamwagia tindikali ambapo kabla ya kutenda uhalifu huo, walitazamana, wakatabasamu na kupeana ishara kwa kichwa.
Wasichana hao waliokuwa wakifanya kazi ya kujitolea katika Shule ya St Monica mjini Unguja, Zanzibar, wamehamishiwa kwenye Hospitali ya Chelsea and Westminster, London wanakotibiwa majeraha ya tindikali.
Mtalii aliyeshuhudia
Mmoja wa mashuhuda wa tukio hilo, Sam Jones, ambaye ni mtalii kutoka Uingereza aliyekuwa Zanzibar kwa mapumziko akiwa na mpenzi wake Nadine, aliliambia gazeti la The Sun la Uingereza namna alivyomsaidia Katie Gee baada ya kumwagiwa tindikali.
Jones alisema akiwa na mpenzi wake kwenye mitaa ya Mji Mkongwe, Unguja, walisikia sauti ya msichana anayeugulia maumivu makali, ikitoka katika choo cha mkahawa uliokuwa jirani.
Alisema walipoingia ndani ya choo walimkuta msichana raia wa Uingereza akiwa ameungua vibaya mwilini, huku wasamalia wema wakijitahidi kumfuta kwa maji yaliyokuwemo ndani ya choo hicho.
Jones alisema dakika mbili baadaye aliingia msichana mwingine ambaye naye alikuwa ameungua, ambapo waliwapa msaada wa kuwasaifisha kwa maji.
“Tulihisi kuna kitu kinawasumbua na kinahitaji kutolewa,” alisema Jones na kuongeza kuwa waliwapeleka wasichana hao kwenye zahanati ya jirani, ambapo Nadine na wanafunzi wa uuguzi walianza kuwamwagia maji yaliyowekwa chumvi.
Alisema kutokana na kuwepo daktari mmoja tu, waliamua kuwapeleka hotelini wasichana hao na kuwatumbukiza ndani ya bwawa la kuogolea, katika jitihada za kuwasaidia kuondokana na maumivu waliyokuwa nayo.
“Maji ya bahari yalionekana kusaidia kwa sababu msichana mmoja aliungua vibaya kwa sababu mwanzo tulitumia maji ya bomba na mengine yalichukuliwa kutoka kwenye ndoo,” alisema.

Jones ambaye alisafiri na majeruhi hao kuja Dar es Salaam na baadaye Uingereza aliongeza kusema: “Tulishtushwa sana na namna walivyokuwa na maumivu makali.
“Kitu ambacho nataka kuweka sawa ni kwamba hawakuwa wamevaa nguo mbaya. Mmoja alikuwa amevaa sweta, suruali ndefu na raba na mwingine alivaa kama hivyo. Walikuwa Zanzibar kusaidia wananchi wa kawaida na walimaliza kazi yao salama.”
Alisema tindikali hiyo ilikuwa kali sana kiasi ambacho hata yeye (Jones), alibabuka mkono wakati akitoa msaada kwa Gee.
Jones alisema akiwa na mpenziwe Nadine na wananchi wengine wa Unguja wakati wakiwasaidia nguo zao zilianza kupukutika kama zilizooza, zikitoa harufu kali yenye uvundo.
Mwalimu mkuu
Akizungumza na gazeti hili Mwalimu Mkuu wa shule ya St Monica ambayo wasichana hao walikuwa wakifundisha, Denis Mayemba alisema waalimu wote wamesikitishwa na tukio na kuitaka kukomesha vitendo hivyo ambavyo vinaoneka kushamiri visiwani.
“Tulikaa nao kama Watanzania wezetu, lakini tunashangaa kusikia wamemwagiwa tindikali, kwa kweli wametuumiza sana mioyo yetu,” alisema Mayemba.
Mwalimu mwingine wa shule hiyo, Margareth Kaleza alisema wasichana hao walimwagiwa tindikali wakati tayari walishamaliza muda wao wa kufanya kazi katika shule hiyo, na kwamba walishafanyiwa sherehe ya kuwaaga.
Alisema walitarajia kuondoka jana kurejea kwao nchini Uingereza.
“Tuliishi nao vizuri bila kukwaruzana lakini nasikitika nani kawaumbua wale watoto,” alisema Margareth.
Alisema wako watu wachache ambao hawapendi kusikia amani iliyopo hapa kwetu ndiyo ambao wanafanya vitendo hivi.

Chanzo: Mwananchi.co.tz