Monday 16 September 2013

Mwakyembe: Wafanyakazi haramu JNIA kukiona

15th September 2013
Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe
Baada ya kufanikiwa kuwadhibiti wasafirishaji dawa za kulevya katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa JK Nyerere jijini Dar es Salaam, Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, amesema sasa atakabiliana na waajiriwa haramu katika uwanja huo.

Akizungumza jana na wafanyakazi wa Wakala wa Ndege za Serikali, Dk. Mwakyembe alisema baada ya kupata malalamiko ya kuwepo na wafanyakazi ambao ni wahamiaji haramu na kuajiriwa katika ofisi mbalimbali uwanjani hapo, anatarajiwa kufanya msako wa kushitukiza ili kuwabaini.

“Nawashukuru sana kwa kunipa taarifa ya kuwepo wafanyakazi haramu, lakini naomba Jumatatu nipate taarifa kamili ili niweze kufanya msako wa kushitukiza kuwanasa…hawa ndio wanaosababisha kuwepo na wahamiaji haramu wengi,” alisema Dk. Mwakyembe.
Dk. Mwakyembe alisema hayo wakati akizungumza na wafanyakazi hao alipokuwa akimtambulisha Katibu Mkuu mpya wa wizara hiyo, Dk. Shaban Mjaka.

Awali akizungumza mbele ya waziri, mmoja wa wafanyakazi wa wakala wa ndege hizo za serikali, alisema pamoja na juhudi za Mwakyembe kudhibiti usafirishaji dawa za kulevya uwanjani hapo, lakini bado tatizo la uingizaji wahamiaji haramu unafanyika kwa kasi kubwa.

“Wapo watu wengi wanaingia hapa nchini kupitia uwanja huu pasipo kufuata taratibu za nchi kutokana na baadhi ya wafanyakazi walioajiriwa katika nafasi nyeti nao kutokuwa na sifa za kuishi nchini kihalali,” alisema mmoja wafanyakazi hao.

Kufuatia madai hayo ya wafanyakazi ambayo yalionekana kumshtua Dk. Mwakyembe, alisema kuanzia wiki ijayo baada ya kupata taarifa kamili atafanya msako wa kuwanasa watu hao ambao wanachangia bila aibu kuingiza watu wengine bila kufuata taratibu za nchi.

Awali akiwa katika Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) kuzungumza na wafanyakazi wa mamlaka hiyo kwa lengo la kumtambulisha Katibu Mkuu wa wizara hiyo na kupata majibu ya maagizo yake aliyoyatoa Desemba 21, mwaka jana katika madai 17 ya wafanyakazi.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI