Na Mwandishi Wetu, Mwananchi
Posted Septemba7 2013 saa 12:0 PM
Posted Septemba7 2013 saa 12:0 PM
Kwa ufupi
Marekani yahaha kutafuta kuungwa mkono kuhusu
uamuzi wake wa kuivamia kijeshi. Urusi yashikilia msimamo wa kuzuia
uvamizi wa kijeshi.
St Petersburg. Viongozi wa nchi zenye nguvu
zaidi kiuchumi duniani wameshindwa kuafikiana kuhusu mzozo wa Syria
katika mkutano unaofanyika nchini Urusi, huku Marekani ikitafuta
uungwaji mkono kuchukua hatua za kijeshi dhidi ya Syria.
Katika mkutano huo wa mataifa hayo makubwa
kiviwanda (G20) uliofanyika huko Petersburg, Urusi, suala la namna ya
kuchukua hatua katika mgogoro unaoendelea nchini Syria ndilo
lililotawala agenda za mkutano huo, ambao ni maalumu kwa ajili ya
masuala ya uchumi na biashara.
Kumekuwa na mikutano ya dharura miongoni mwa pande
mbili zinazotofautiana kuhusu namna ya kuchukua hatua kwenye mgogoro
huo, ambapo Rais Barack Obama wa Marekani na Vladmir Putin wa Urusi
wamekuwa wakijaribu kutafuta ushawishi kwa ajili ya kuungwa mkono.
Hadi jana mchana, viongozi waliopata fursa ya
kulizungumzia suala hilo la Syria walisema hakukuwa na maafikiano kuhusu
hatua za kuchukuliwa, ambapo Waziri Mkuu wa Italia, Enricco Letta,
alithibitisha kupitia mtandao wa Twitter kuwa hakukuwa na maafikiano
kuhusu mzozo wa Syria.
Urusi imekuwa ikisimama kidete kuhusu
kutochukuliwa hatua za kijeshi dhidi ya utawala wa Rais Bashar al-Assad
kuhusiana na madai kuwa ulitumia silaha za kemikali dhidi ya raia wake
Agosti 21.
Hadi jana mchana, Rais Barack Obama alikuwa
akiendelea na jukumu lake la kutaka kuungwa mkono kuhusu kuichukulia
Syria hatua za kijeshi, ambapo aliweza pia kukutana na Rais wa China
pembezoni mwa mkutano huo na baadaye kukutana na mshirika wake, Rais wa
Ufaransa, Francois Hollande.
Mjumbe wa Marekani kwa Umoja wa Mataifa, Samantha
Power, ameishutumu Urusi kwa kulishika mateka Baraza la Usalama la Umoja
wa Mataifa (UN) kwa kutumia kura yake ya turufu. Waziri Mkuu wa
Uingereza, David Cameron, naye alisema nchi yake ina ushahidi mpya
kuhusu shambulio hilo la kemikali.
Hata hivyo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN),
Ban Ki-Moon, aliwaambia viongozi hao wa G20 kuwa kutoa silaha kwa upande
wowote katika mzozo wa Syria sio suluhisho kwani hatua za kijeshi
haziwezi kuwa suluhisho la mzozo huo.
Washirika wa Syria bado hawaonekani kushawishika na kampeni za Obama za kuchukuliwa hatua za kijeshi.
Papa Francis ataka suluhisho
Wakati mkutano huo ukiendelea, kiongozi wa Kanisa
Katoliki duniani, Baba Mtakatifu Francis, pia ameelezea hisia zake
kuhusu mzozo huo na kutoa wito kutafutwe suluhisho la amani na wala si
kwa kutumia nguvu za kijeshi akionya hatua za kijeshi zitaambulia patupu
katika kuumaliza mzozo wa Syria.
Kansela wa Ujerumani, Angela Merkel, pia alisema
mara kadhaa kuwa nchi yake haitashiriki katika shambulio la kijeshi
litalaoongozwa na Marekani dhidi ya Syria na tayari Bunge la Uingereza
lilipiga kura kupinga nchi hiyo pia kuhusika katika hatua hiyo.
Mkutano huo wa G20 uliofanyika kwa siku mbili ulimalizika jana
ambapo Rais Putin aliyekuwa mwenyeji alipanga muda maalumu kujadili
mzozo huo katika chakula cha usiku wa juzi, licha ya kuwa Syria haikuwa
katika ajenda.
Utawala wa Syria umekuwa ukishutumiwa kwa kutumia silaha za kemikali dhidi ya raia wakati wa mzozo huo uliodumu miezi 30 sasa.
source: Mwananchi
source: Mwananchi