Na Rachel Chibwete na Masoud Masasi, Mwananchi
Posted Septemba7 2013 saa 11:38 AM
Posted Septemba7 2013 saa 11:38 AM
Kwa ufupi
Dodoma. Moto mkubwa umezuka jana kwenye Msikiti 
wa Manyema uliopo Barabara ya Saba katika Manispaa ya Dodoma na 
kusababisha uharibifu mkubwa wa mali pamoja na jengo hilo.
Moto huo ulianza saa 8 mchana baada ya swala ya 
Ijumaa hatua ambayo ilileta taharuki kwa waumini waliokuwapo ndani ya 
msikiti huo.
Mmoja wa mashuhuda wa tukio hilo, Juma Mohamed 
alisema walianza kuona moshi mzito ukitoka ndani ya jengo la ghorofa ya 
pili ya msikiti huo na baadaye moto mkubwa ulizuka.
“Baada ya kuona moto huo, tuliwasiliana na Kikosi 
cha Zimamoto ambao walifika katika eneo la tukio na kuuthibiti moto huo 
japo kuna uharibifu wa mali uliotokea,” alisema Mohamed.
Shuhuda mwingine Sauda Ally alisema, alikuwa nje 
ya duka lake lililopo karibu na msikiti huo na kushuhudia moto mkubwa 
ukiwa unawake kwenye ghorofa ya pili ya jengo hilo hali iliyowafanya 
kufunga maduka yao.
Mmoja wa maofisa wa polisi aliyefika katika tukio 
hilo alisema, bado hawajua chanzo halisi cha moto huo japo kwa taarifa 
za awali zinaonyesha kuwa ulisababishwa na hitilafu ya umeme.
“Sisi baada ya kupata taarifa hizo tuliwasiliana 
na wenzetu wa Kikosi cha Zimamoto na Tanesco kwa ajili ya kuuzima moto 
huu,” alisema ofisa huyo. Kaimu Kamanda wa Polisi Suzan Kaganda, 
alithibitisha kutokea kwa tukio hilo.
source: Mwananchi
source: Mwananchi
