Monday 16 September 2013

Ninakililia kizazi chetu, ninalililia taifa letu!

15th September 2013
Ni nani anatuloga Watanzania, ingawa kwa baadhi yetu, kufikia hatua ya ndugu wa nchi moja, kushamirisha vitendo viovu vinavyoathiri utu na heshima ya binadamu?
Uovu dhidi ya ubinadamu unaofanyika, unatokana na utashi binafsi ama ‘nguvu za nje’ zinazotufanya kuonekana wajinga kiasi hiki?

Kwa maana safari ya kulijenga ‘taifa ovu’ lenye ‘waovu’ na matendo maovu, inazidi kusonga mbele, hakuna udhibiti unaofanyika kiasi cha kuiaminisha jamii, kwamba tupo imara.
Katika siku za hivi karibuni, nchi imekumbwa na aibu, matendo maovu yanafanywa dhidi ya raia wasiokuwa na hatia, nchi imetulia!
Wapo wanaoamini kuwapo kwa vitendo viovu dhidi ya ubinadamu ndani ya Tanzania, kwa miongo kadhaa sasa. Inawezekana.
Wapo wenye orodha ya majina na picha za raia waliowahi kutendewa uovu kwa kupigwa, kunyanyaswa, kuporwa mali na wengine kufa, tena kwa namna ya kizembe.
Ingawa ni hivyo, lazima ikubalike kwamba kwa muda mrefu, Tanzania imekuwa mahali salama pa kuishi. Amani na utulivu vikawa miongoni mwa nguzo kuu za umoja wa kitaifa.
Tukalelewa hivyo, tukakua hivyo na kuishi hivyo, japokuwa kwa kizazi ambacho kwa mujibu wa idadi ya miaka ya uhai wao, sasa wanaondoka duniani kupitia ‘mauti ya haki’.
Kizazi kilichopo ndicho kinachoushuhudia uovu ambao, kutokana na ukosefu wa takwimu sahihi, hakuna sababu ya kuulinganisha na mwingine uliowahi kutokea kwa ‘kizazi kinachoondoka’.
Ninajua wazi kwamba jamii iliyo hai, haikosi kuwapo na tofauti za fikra, maneno, hulka, matendo na mengineyo.
Lakini uwapo wa tofauti hizo hauwezi kuwa sababu ya kuibua, kutenda na kuendeleza vitendo viovu dhidi ya ubinadamu na wanadamu.
Miongoni mwa matendo maovu yanayolikabili taifa ni kushambuliwa, kujeruhiwa na kuuawa kwa viongozi wa dini.
Inapotazamwa orodha ya viongozi hao, Kanisa Katoliki hususani upande wa Zanzibar, linakuwa miongoni mwa waathirika wakuu wa uovu huo.
Wapo viongozi wengine waliojeruhiwa, wakiwa katika idadi inayoweza kulingana na wale wa Kanisa Katoliki ama kuwa chini ya hao, lakini ukweli unabaki kwamba wote wanabeba uzito unaolingana-matendo maovu dhidi ya ubinadamu.
Inawezekana mashambulizi, kujeruhi na kuwaua viongozi wa dini kusihusishwe na tofauti za kidini, isipokuwa ushiriki wa waovu kama wanavyoshiriki katika uovu mwingine.
Kwa maana haingii akilini, kwamba kwa shambulizi la juzi la Padre Joseph Mwang’amba, anayehudumiwa kituo cha malezi ya vijana wa Zanzibar, atendewe unayama huo!
Ni nani asiyetambua changamoto zinawakabili vijana, kwamba ‘awe kipofu’ kiasi cha kukerwa na utekelezaji wa majukumu ya Padre Mwang’amba, kiasi cha kummwagia tindikali? Haingii akilini!
Kama nilivyokuwa nikielezea katika makala zangu zilizopita, tukio kama hilo la juzi huko Zanzibar, linapaswa kuhusishwa na mfumo unaochochea kushamiri kwa vitendo hivyo.
Kuangalia malezi wanayoyapata vijana ndani ya familia, majirani na jamii inayowazunguka. Yanayotolewa kwa kadri inavyostahili, haki na usawa?
Kwa maana kama wazazi na walezi hawatatimiza wajibu wao ipasavyo, wakitegemea ‘dunia’ itafunza watoto ama vijana, inakuwa mfano wa kufungua ‘mlango wa uovu’ nchini, kizazi cha sasa kikaingia.
Mbali na wazazi ama walezi, viongozi wa jumuiya za watu, wakiwamo watendaji na watumishi wa umma (serikali), wanatekeleza wajibu na majukumu yao kwa raia na taifa?
Haiwezekani kwa nchi yenye viongozi wasiokuwa na maono, mtazamo chanya na uthubutu wa ‘kulijenga taifa imara’ lisilokuwa na matendo maovu kama kuwashambulia, kuwajeruhi ama kuwaua wasiokuwa na hatia.
Upo msemo wa Kiswahili, kwamba ‘serikali ina mkono mrefu’. Lakini inakuwaje mkono huo ushindwe kuzibaini mbinu, mfumo na mtandao unaotumika katika utekelezaji wa matendo hayo?
Kwamba linatokea tukio la kwanza, la pili, la tatu na kuendelea, yote yakiwa na `taswira’ inayofanana, kwamba kikipatikana chanzo kimoja, mtandao mzima utajulikana, nini kinafanyika kwa walio na mamlaka ya kulitekeleza hilo!
Ama ni kauli za kipropaganda, zinazopambwa na ahadi za ‘tumejipanga, tutawasaka wahusika na kuchukua hatua kali ili tukio kama hilo lisotokee tena.’
Zinapotolewa kauli kama hizo, watu wanajisahau siku kadhaa, kunaibuka tukio jingine, inashangaza na kuikera jamii, hata wengine kufikia hatua ya kufikiria ‘waingie kazini’ kujilinda na kuwadhibiti wanaowashambulia na kuzishambulia mali zao.
Wapo viongozi wa dini wanaoweza kuwa sehemu ya kushamirisha uovu unaotendeka sasa, kutokana na muingiliano wao dhidi ya walio katika utawala, wakashindwa kutimiza wajibu wao.
Viongozi wa dini wanapaswa kuwa huru, wakishirikiana na watawala, walio katika utawala na wanasiasa kwa namna ya ubinafsi, pale wanapoingia kwenye nyumba za ibada ‘kuziokoa’ roho zao dhidi ya dhambi.
Lakini inapotokea kiongozi wa dini kuwa mshirika wa karibu wa mtawala wa kidunia, walio katika utawala ama wanasiasa, inakuwa vigumu kutimiza wajibu wao wa kuonya na kukaripia, japo kwa unyenyekevu wote.
Kwa hali hiyo, safari ya amani, umoja na mshikamano nchini ni kama imezongwa na miiba. Miiba inazidi kumea, inasongea karibu na kutaka kuiathiri, isiendelee kumea.
Hapo ndipo ninapokitazama kizazi chetu, ninakililia. Ninaitazama nchi yetu, ninaililia, kwamba miiba hiyo inapozidi kusogea, nini hatima yake?
Si wakati wa kunyoosheana vidole, bali kupambana ili uovu unaotokea sasa, usiwe sehemu ya `utamaduni’ wa Mtanzania.
Kwa maana walio katika orodha, wakifikia ukomo wa kupigwa, kujeruhiwa ama kuuawa, watawageukia walio katika shirika nao, watawageukia ndugu na jamaa zao, watawatenda vivyo hivyo, kwa mujibu wa historia ya mwanadamu.
Hali ikiwa hivyo, nchi haitakuwa salama, kwa wanaolengwa na hata watekelezaji wenyewe. Haipaswi kufika huko.
Tuchukue hatua!
Mashaka Mgeta ni Mhariri wa Makala wa gazeti hili na mchambuzi wa masuala ya siasa. Anapatikana kupitia simu namba +255754691540/716635612 ama barua pepe: mgeta2000@yahoo.com.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI