Tuesday 1 October 2013

Serikali yatafakari kutoa ruzuku kwa shule binafsi

30th September 2013
Naibu Waziri wa Nishati na Madini,George Simbachawene
Serikali inatafakari uwezekano wa kutanua wigo wa kutoa ruzuku hadi kwa shule zinazomilikiwa na watu binafsi, ikiwa ni sehemu ya azma ya kuzipunguzia gharama za uendeshaji.

Naibu Waziri wa Nishati na Madini, George Simbachawene, amesema hayo wakati akizungumza kwenye mahafali ya darasa la saba katika Shule ya St. Anne Marie Academy jijini Dar es Salaam jana.

Alisema shule nyingi za binafsi zinafungwa kutokana na kushindwa kujiendesha miongoni mwa sababu kubwa ikiwa ni kupanda kwa gharama za uendeshaji.

Simbachawene alisema kuziacha shule binafsi `zife’ kutokana na sababu iliyo ndani ya uwezo wa nchi kuitatua, ni hasara kwa taifa na kwamba njia pekee ya kuzisaidia kwa kuzipa ruzuku ili ziweze kujiendesha.

Kwa mujibu wa Simbachawene, shule binafsi zimesaidia kwa kiasi kikubwa kuinua kiwango cha elimu, hivyo kupunguza idadi na kasi ya Watanzania kupeleka watoto wao kusoma nje ya nchi.

Alisema: "Ukiacha shule kama hii (St. Anne Marie) ikafa ni hasara kwa taifa, serikali inaangalia kuona namna bora ya kuzisaidia kwa kuzipatia ruzuku ili kuzipunguzia gharama za uendeshaji.”

Kwa upande mwingine, Simbachawene aliwaasa vijana kuwa makini katika kukabiliana na kuzishinda changamoto zilizo katika jamii, ikiwamo maambukizi ya Virusi vya Ukimwi (VVU) na matumizi ama usafirishaji wa dawa za kulevya.

Meneja wa shule hiyo, Jasson Rweikiza, alisema serikali imekuwa na kigugumizi katika mambo mbalimbali katika sekta ya elimu, hali inayosababisha  kudumaa kwa sekta hiyo na watoto kukosa ufaulu mzuri.

Kwa mujibu wa Rweikiza ambaye pia ni Mbunge wa Bukoba Vijijini, mpaka sasa mitaala ya elimu na sera za elimu hazipo wazi, hali inayosababisha walimu wakose mwongozo wa kufundishia.

Alisema wadau wa elimu hususani wamiliki wa shule binafsi, wanakabiliwa na kazi kubwa ya uendeshaji, huku kukiwa na changamoto kadhaa kama vile matumizi ya mitaala isiyoeleweka.

Pia alisema sera zinazohusiana na elimu hazipo wazi, na kutoa mfano kuwa sera haielezi kama ni kosa ama si kosa inapotokea kuwapo mwanafunzi asiyejua kusoma.

“Maendeleo hayawezi kwenda bila kuboresha sekta ya elimu...tunaiomba serikali isimame imara katika kuinusuru sekta ya elimu nchini,” alisema.

Rweikiza alisema wahitimu wa darasa la saba wanapaswa kuondokana na dhana inayowafanya kujiona wamemaliza shule, bali kiwango hicho kuwa msingi wa safari ndefu inayowakabili maishani.
CHANZO: NIPASHE