Monday 14 October 2013

Wanawake watatu wadaiwa kukutwa na dawa za kulevya


14th October 2013
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu
Wanawake watatu, wakazi wa Dar es Salaam, wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashtaka ya kukamatwa na dawa za kulevya aina ya mirungi gramu 19,400  zenye thamani ya Sh. milioni 1.08.

Washtakiwa hao Mtumwa Mohamed (40), Mariam Hamisi (24) na Bahati Abeid(30), walisomewa mashtaka na Wakili wa Serikali, Adolf Mkini, mbele ya Hakimu Sundi Fimbo.

Katika shtaka la kwanza, mshtakiwa wa kwanza, Mtumwa alidaiwa Septemba 22, mwaka huu katika Feri ya Zanzibar Wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam alipatikana na dawa za kulevya gramu 6000 za mirungi zenye thamani ya Sh. 300,000. Wakili Mkini alidai mshtakiwa wa pili, Mariam katika siku, tarehe na mahali hapo alipatikana na gramu 6800 za mirungi zenye thamani ya Sh. 400,000.

Aidha, katika shtaka la tatu linalomkabili Mshitakiwa Bahati alidaiwa katika tarehe, mwezi na mahali hapo alipatikana na gramu 6600 za mirungi zenye thamani ya Sh. 380,000.
 
CHANZO: NIPASHE