Friday 13 September 2013

Sekta ya madini : Uchimbaji urani Namtumbo na harufu ya ufisadi


Na Elias Msuya, Mwananchi

Posted  Alhamisi,Septemba12  2013  saa 11:0 AM
Kwa ufupi
Alipoulizwa kuhusu suala hilo, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo  anabainisha kwamba shauri hilo lipo mahakamani na kwamba kumekuwapo uovu mwingi kwenye sekta ya madini.


Urani inayochimbwa kote Tanzania haina hatari hadi isafishwe ndiyo maana inapatikana juu ya ardhi, Mungu ni wa ajabu kabisa.
Wakati Tanzania ikitegemea kuanza kufaidika na madini ya urani, tayari kuna harufu ya ufisadi inayogubika kampuni za uchimbaji wa urani wilayani Namtumbo Mkoa wa Ruvuma.
Akifafanua utafiti alioufanya kuhusu athari za uchimbaji madini ya urani nchini hivi karibuni jijini Dar es Salaam, mwanasheria wa mazingira Dk Lugemeleza Nshala anasema harufu hiyo inatokana na kampuni ya Mantra Resources Limited yenye leseni katika eneo la Mkuju River kujigawa katika kampuni mbili  yaani ARMZ na Uranium One.
Alipoulizwa kuhusu suala hilo, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo  anabainisha kwamba shauri hilo lipo mahakamani na kwamba kumekuwapo uovu mwingi kwenye sekta ya madini.
“Ni kweli kwamba Mamlaka ya Mapato Tanzania  (TRA) wamepeleka suala hilo mahakamani, lakini mkataba wa kuchimba madini hayo  ni mwingine kabisa. Nakubaliana na wewe pia kwamba kumekuwa na mikataba mibovu, sijui kuna watu wamekula, lakini Watanzania tuwe na mtazamo wa kuendelea siyo kuangalia nyuma.
 “Huo ni mtazamo wa kizamani, tumekuwa na muda mwingi wa kujadili matatizo tu, tumekuwa waoga mno wa kuthubutu, haya matatizo popote yapo. Mfumo wa dunia kwa sasa ni uwekezaji, tuwekeze ndani na nje ya nchi ili kupata fedha na ajira,”anabainisha Profesa Muhongo.
Ukwepaji kodi
Dk Nshala anasema: “Oktoba 2010 Mantra Resources Limited ya Australia inayomiliki leseni ya Mkuju River iliingia kwenye utekelezaji wa mkataba na kampuni ya Atomredmetzoloto (ARMZ) ya Russia katika makubaliano yao na ARMZ ilitakiwa iwalipe Mantra dola 1.6 bilioni za Marekani  ikiwa ni asilimia 100 ya kumiliki Mantra.
“Hivyo makubaliano ya kuuza hisa zake yalikuwa ni dola 8.00  za Australia kwa kila hisa, lakini kutokana na tetemeko lililotokea Fukushima Japan kwenye kinu chake cha nyuklia miezi minne baadaye, ARMZ wakataka kujitoa.
“Lakini baadaye wakaja na makubaliano mapya  na Mantra hawakuwa na la kufanya ila kuingilia makubaliano ya kushusha bei ya dola za Australia 7.02 kwa kila hisa ambayo ni sawa na dola 1.04 bilioni  za Marekani ya hisa zote. Hadi Juni 7, 2011 makubaliano yakafikiwa na ARMZ ikamilikishwa hisa zote.
“Mwaka huohuo, ARMZ ikaingia mkataba wa kununua hisa 51.4 za kampuni ya Uranium One ambayo ni kampuni tanzu ya Canadian uranium mining company,” anasema Dk Nshala.
Anaendelea kufafanua: “Hivyo kuhamishwa kwa Mantra Resources Limited   kutoka ARMZ ili wadau wa awali kupata dola 1.04 bilioni za Marekani bila kulipa kodi ya mapato kwa Tanzania.

 “Sheria ya madini ya mwaka 2010 inaruhusu kampuni ya madini kugawa faida yake baada ya kupata ruhusa kutoka  kwa mamlaka ya leseni ambaye kimsingi ni kamishina wa madini.
Kifungu cha 36(1) cha Sheria ya Kodi ya mapato kinaonyesha  Mantra Resources Limited ya Australia ilitakiwa kulipa kodi kwa Serikali ya Tanzania,” anabainisha Dk Nshala.
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ilipeleka mfululizo madai kwa ARMZ  ikitaka kulipwa dola 200 milioni za Marekani kama kodi ya faida. Sasa TRA imepeleka kesi hiyo Bodi ya Rufaa ya Kodi ya Mapato.
Jitihada za kuutafuta uongozi wa Mantra Tanzania ili kuzungumzia suala hilo hazikuzaa matunda licha ya Mkurugenzi Mtendaji, Assa Mwaipopo kumtaka mwandishi kumtumia maswali kwanza ayaone jambo mbalo mwandishi wa makala haya alifanya hivyo.  Licha ya Mwaipopo kupelekewa maswali na kukumbushwa mara kwa mara kujibu, mpaka leo hakujibu maswali hayo.
“Kwa sasa niko kwenye mkutano wa bajeti, nitumie maswali kwanza niyaone,” anasema Mwaipopo kwa njia ya simu.
Mazingira
Mbali na kuwapo utata katika ulipaji wa kodi, Dk Nshala amesema katika taarifa yake Tanzania bado haijawa tayari kwa uchimbaji huo kwani hakuna maandalizi ya kutosha.
Anaeleza kwamba utoaji wa leseni kwa Kampuni ya Mantra Tanzania Ltd na ziara ya Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Makamu wa Rais, Dk Terezya Huvisa katika ofisi za Mantra  Tanzania na wilayani Namtumbo, ilikuwa kinyume cha sheria ya EMA kifungu cha  95 na 206(2(c) na unaweza kupingwa katika Mahakama ya Rufaa ya Mazingira.
 “Waziri alikaririwa akisema kampuni kupitia taarifa yake ya mradi imemshawishi kwamba mradi umejengwa nje na mbali ya makazi ya watu hivyo ina faida.”
Dk Nshala anabainisha sheria haisemi popote kwamba Waziri anatakiwa akubaliane na mawasilisho ya mradi huo kama alivyofanya yeye.
Dk Huvisa anasema: “Kwa nini nisitembelee mradi huo, Watanzania ni watu wa ajabu sana, mimi kama Waziri najiamini na nina hofu ya Mungu kwa nini nisiende?
Nimetembelea machinjio, nimetembelea Double Tree hotel na hatua zimechukuliwa, kwa nini  niende kwenye mradi wa Mantra?” anahoji Dk Huvisa.
SOURCE: MWANANCHI