Wednesday 11 September 2013

Mfumko wa bei washuka


 
Na James Maga

Posted  Jumanne,Septemba10  2013  saa 21:43 PM
Kwa ufupi
Kwesigabo alizitaja bidhaa za vyakula zilizochangiwa kupungua kwa mfumuko wa bei na kiwango cha punguzo kwa asilimia katika mabano kuwa ni pamoja na mikate na nafaka (2.2), vitafunwa (3.8), mahindi ( 1.6), unga wa ngano (2.5), unga wa muhogo ( 0.6) na unga wa mtama (3.4).


Dar es Salaam. Mfumuko wa bei nchini umezidi kupungua na sasa umefikia asilimia 6.7 kwa mwezi Agosti, 2013, kutoka asilimia 7.5, Ofisi ya Takwimu ya Taifa (NBS) imebainisha, katika taarifa yake ya matokeo ya mfumuko wa bei kwa mwezi Agosti.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mkurugenzi wa Sensa na Takwimu za Jamii wa NBS, Ephrahim Kwesigabo alisema kupungua kwa mfumko huo wa bei kunamaanisha kuwa kasi ya upandaji wa bei za bidhaa na huduma kwa mwezi Agosti imepungua kulinganisha na mwezi Julai.
“Kwa kiasi kikubwa kupungua kwa mfumuko wa bei nchini kumechangiwa na kupungua kwa mfumko wa bei za bidhaa za vyakula na vinywaji baridi kutoka asilimia 8.0, mwezi Julai hadi asilimia 6.5, mwezi Agosti, 2013.”, alisema Kwesigabo.
Hata hivyo Kwesigabo alisema kwa upande mwingine kasi ya ongezeko la bei kwa bidhaa zisizo za vyakula imebakia kuwa ileile ya asilimia 7.3, kama ilivyokuwa Julai 2013.
Alisema kupungua kwa mfumuko huo wa bei kuna maanisha kuwa kuna unafuu wa maisha kwa mlaji na kwamba hiyo inaonesha kuwa Tanzania inapiga hatua nzuri katika uchumi wa nchi.
Kwesigabo alizitaja bidhaa za vyakula zilizochangiwa kupungua kwa mfumuko wa bei na kiwango cha punguzo kwa asilimia katika mabano kuwa ni pamoja na mikate na nafaka (2.2), vitafunwa (3.8), mahindi ( 1.6), unga wa ngano (2.5), unga wa muhogo ( 0.6) na unga wa mtama (3.4).
Bidhaa nyingine ni kuku wa kienyeji (0.9), samaki wabichi (2.6), karanga (2.0, mbogamboga (2.4), nyanya (9.9), vitunguu maji ( 2.0), viazi vitamu ( 4.8), mihogo (4.1) na sukari ( 0.5).
“Bidhaa zisizo za vyakula zilizochangia kupungua kwa mfumuko wa bei ni viatu (0.3), samani (0.1), vyombo vya udongo (1.0), vifaa vya elektroniki vya kurekodia picha na sauti (0.3).”, aliongeza Kwesigabo.
Akizungumzia uwezo wa shilingi ya Tanzania katika kununua bidhaa na huduma, alisema umepungua kwa Sh28.54 na kufikia Sh71.46, kutoka mwezi Septemba, 2010 hadi sasa.

soource: Mwananchi