Monday 4 November 2013

Mjumbe wa Tume ya Katiba acharangwa mapanga Dar


Rais Jakaya Kikwete (wa pili kushoto) akiwa na mkewe Mama Salma pamoja na Mwenyekiti wa chama cha NCCR- Mageuzi James Mbatia, na daktari wa zamu wakimwangalia mjumbe wa tume ya mabadiliko ya katiba, Dk Sengondo Mvungi, aliyelazwa katika taasisi ya mifupa Muhimbili (MOI) jana, baada ya kujeruhiwa na watu wanaosadikiwa kuwa ni majambazi. Picha na Ikulu 

Na Waandishi Wetu, Mwananchi

Posted  Jumatatu,Novemba4  2013  saa 7:50 AM
Kwa ufupi

Dk Mvungi, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Katiba, Sheria na Haki za Binadamu wa NCCR-Mageuzi aliwahishwa kwenye Taasisi ya Mifupa Hospitali ya Muhimbili (MOI), ambako amelazwa katika wodi maalumu huku hali yake ikiwa mbaya.


Dar es Salaam. Mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba nchini, Dk Sengondo Mvungi amejeruhiwa usiku wa kuamkia jana, baada ya kukatwa kwa mapanga na watu wasiojulikana waliovamia nyumbani kwake Mpiji-Magohe, jijini Dar es Salaam.
Dk Mvungi, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Katiba, Sheria na Haki za Binadamu wa NCCR-Mageuzi aliwahishwa kwenye Taasisi ya Mifupa Hospitali ya Muhimbili (MOI), ambako amelazwa katika wodi maalumu huku hali yake ikiwa mbaya.
Taarifa kutoka kwa ndugu na watu waliomtembelea hospitalini hapo wanasema kwamba hali ya Dk Mvungi ni mbaya kwani alikuwa hawezi hata kuzungumza.
Akisimulia tukio hilo, dereva wa Dk Mvungi anayeitwa Emmanuel Ntaro, alisema akiwa nyumbani kwake majira ya saa 6:30 usiku, alisikia mlipuko mkubwa kisha zikasikika kelele zikitokea nyumbani kwa bosi wake.
“Nilifika na kukuta hajitambui, tukampeleka Hospitali ya Tumbi Kibaha mkoani Pwani alikopatiwa huduma ya kwanza kabla ya kumpeleka MOI ambako anaendelea kuchunguzwa na kupatiwa matibabu,” alieleza Ntaro
Alisema kuwa watu wapatao sita, walivamia nyumbani kwa Dk Mvungi ambako baada ya kuvunja mlango na kuingia ndani, walimjeruhi kwa kutumia mapanga huku wakidai wapatiwe fedha. Watu hao walimsababishia majeraha usoni, kichwani na sehemu nyingine za mwili.
Akizungumza na Mwananchi jana, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia alisema mbali na kupata matibabu MOI, pia walilazimika kumpeleka Hospitali ya Aga Khan kwa ajili ya vipimo zaidi katika mashine ya CT Scan kama walivyoshauriwa na madaktari wa zamu.
Mbatia alisema kuwa baada ya Dk Mvungi kufanyiwa kipimo hicho alirudishwa tena MOI kwa matibabu na uangalizi maalumu. “Hali yake inaanza kuimarika tofauti na nilivyomuona saa nne asubuhi, “ alisema Mbatia muda wa saa 12 jioni jana alipozungumza na gazeti hili.
Alisema kwamba pia watu waliohusika na tukio hilo waliiba kompyuta mpakato (laptop) pamoja na bastola ya Dk Mvungi.
Kamanda wa Mkoa wa kipolisi Kinondoni, Cammilius Wambura alithibitisha kutokea kwa tukio hilo.
“Kweli hilo ni tukio la kihalifu na sisi tunaendelea kulifanyia kazi. Tunawahakikishia Watanzania kuwa watu hao watapatikana na kufikishwa kwenye mkono wa kisheria,” alisema.
Kilichotokea 

Akisimulia tukio hilo, mtoto wa Dk Mvungi anayeitwa Deogratius Mwarabu, alisema kuwa walipigiwa simu na mdogo wao saa 7.00 usiku wa kuamkia jana na aliwaeleza kuwa baba yao alikuwa amevamiwa na watu wanaodhaniwa kuwa majambazi.
Mwarabu alisema watu wapatao sita walivamia katika nyumba ya Dk Mvungi na kwenda chumba cha nje cha nyumba hiyo anachoishi fundi wa nyumba hiyo.
Watu wanne ndio walikwenda katika chumba hicho na kumpiga na nondo mfanyakazi huyo na kumlazimisha awaonyeshe chumba cha Dk Mvungi. Mwarabu alisema baada ya kumpiga walimfunga kamba mfanyakazi huyo kisha kwenda kwenye nyumba kubwa kwa kupitia mlango wa jikoni. Alisema kuwa baada ya Dk Mvungi kusikia kelele aliamua kutoka chumbani na ndio akakutana na watu hao wakiwa tayari kwenye nyumba anayoishi.
“Walimkata panga utosini halafu wakampiga usoni kwa kutumia ubapa wa panga. Aliangukia upande wa uso,” alisimulia Mwarabu.
Baada ya tukio hilo, watu hao walimwamuru mfanyakazi aliyekuwa amefungwa kamba alale chini huku wengine wakiendelea kufanya upekuzi kwenye nyumba hiyo.
Alisema baada ya hapo walikwenda kwenye chumba anacholala Dk Mvungi na kumkuta mkewe, ambaye walimwamuru awape fedha.
“Mama alitoa fedha, lakini hatukuweza kujua ni kiasi gani alichotoa. Maana tumemwacha apumzike kwanza,” aliongeza Mwarabu.
Kwa mujibu wa Mwarabu, majambazi hao baada ya kupewa fedha, walidai kuwa fedha hizo hazitoshi na kutaka mke wa Dk Mvungi awaongezee zaidi.
“Walimtishia mama kuwa wangemchinja kama asingetoa fedha zaidi, naye akasisitiza hakuwa na fedha na kuwaruhusu wamchinje,” alisema Mwarabu.
Katika kushinikiza atoe kiasi cha fedha zaidi, watu hao walimpiga kwa stuli Mama Mvungi na kumuumiza miguu yake ndipo wakaanza kupekua kwenye makabati ya chumba chao cha kulala.
Kwa mujibu wa mtoto huyo wa Dk Mvungi, mbali na kuchukua kompyuta na bastola watu hao walichukua simu tano, ambapo mbili zikiwa za Dk Mvungi, mbili za mama yao na moja ya mfanyakazi wao. Alisema katika nyumba hiyo wanaishi watu sita. Dk Mvungi, mkewe, fundi wa nyumba na wajukuu watatu.
Mwananchi ilipomtafuta tena Mwarabu jana jioni kujua hali ya Dk Mvungi, alisema kwamba bado baba yake yuko mahututi na kwamba alikuwa hawezi kuzungumza

JK amjulia hali
Rais Jakaya Kikwete alikuwa miongoni mwa viongozi waliokwenda kumwona Dk Mvungi hospitalini alikolazwa.
Viongozi wengine waliokwenda kumtazama ni pamoja na Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali Said Mwema, Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Joseph Warioba na Makamu wake Jaji Agustino Ramadhan.
Warioba asikitika 
Naye Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba alisema tukio hilo ni baya na limewashtua na kuwaachia simanzi. Alisema kuwa wanasubiri taarifa itakayotolewa na vyombo vya usalama kuhusu tukio hilo.
“Hali ya mwenzetu ni mbaya, nimemwona hospitalini na kwa kuwa alikuwa bado anahudumiwa na madaktari, sina cha kueleza zaidi ya kuwaomba matabibu wetu waendelee kupigania afya yake ili arejee katika hali yake ya kawaida,” alieleza Jaji Warioba.
Jaji Warioba aliwaomba Watanzania wote waungane kumwombea mjumbe huyo, ambaye ni kiungo muhimu katika tume hiyo na kwamba kumkosa katika kipindi hiki ni dhahiri kutaongeza pengo katika utendaji wa kila siku.
Naibu Katibu wa Tume hiyo, Casmir Kyuki alisema tukio hilo analichukulia kuwa ni la kihalifu na kwamba kuna uwezekano ndio athari za kauli zinazotolewa na wanasiasa dhidi yao (watumishi wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba), kwamba wanalipwa pesa nyingi.
“Hawa watu walilenga kupata pesa ambazo waliamini mwenzetu alikuwa nazo. Hii inatokana na watu hasa wanasiasa kusema maneno bila hata kujiridhisha,” alieleza Kyuki.
Kyuki alisema wajumbe wa tume wanaishi uraiani bila ulinzi wowote kwa sababu wanafahamu hali zao ni za kawaida, lakini kutokana na maneno dhidi yao jamii inadhani kuwa wana fedha nyingi sana.
“Magari tunayotumia yana nembo, watu wanafanya kazi mpaka usiku, matokeo yake ndiyo hayo,” alisema Kyuki.

SOURCE: MWANANCHI