| 
 
* Uhamiaji yawagawia vibali kinyemela 
* Wizi mifugo ya wazawa wakithiri, mazingira yaharibiwa 
 
  
Wakati
 Serikali kupitia kwa Mkuu wa Operesheni Kimbunga, Simon Sirro, 
ikijigamba kufanikiwa katika kazi ya kuwakamata wahamiaji haramu na 
kuwarudisha kwao, JAMHURI imebaini kuwa 
wahamiaji wengi wanaishi na mifugo yao katika Pori la Akiba la Kimisi, 
Wilaya ya Ngara mkoani Kagera, huku wakikingiwa kifua na baadhi ya 
vigogo wa Idara ya Mifugo, na Uhamiaji wilayani hapa. 
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili tangu operesheni hiyo ilipoanza, 
umebaini kuwa baadhi ya vigogo wa idara hizo waliigeuza kazi hiyo kuwa 
mradi wa kujineemesha kinyume cha lengo lililokusudiwa na Serikali, hali
 ambayo imesababisha kuwapo kwa migogoro isiyoisha baina ya wenyeji wa 
eneo hilo na wahamiaji haramu. 
  
Migogoro
 hiyo ambayo chanzo chake ni baadhi ya vigogo wa Idara ya Uhamiaji 
kuwagawia kama njugu wahamiaji haramu vibali vya kuishi nchini kwa muda,
 ambao kwa kiburi cha vibali hivyo wameamua kuvamia na kujenga katika 
maeneo ya wazi yaliyotengwa na Serikali za Vijiji husika kwa ajili ya 
shughuli za maendeleo ya umma. 
  
Hali
 hiyo imesababisha viongozi wa vijiji husika kuishi kama wakimbizi, huku
 wakihofia kuuawa kwa kinachoelezwa kuwa Serikali wilayani Ngara imeziba
 masikio. 
  
Tukio
 la hivi karibuni, ambalo linadaiwa kuchochewa na baadhi ya vigogo wa 
idara za Uhamiaji, na Mifugo waliowekwa mfukoni na kufanya watakavyo 
kinyume cha taratibu za nchi, ni la wafugaji wawili kuuawa kinyama kwa 
kukatwa kwa panga na kuchomwa mikuki na wananchi. Pia ng’ombe 12 
waliuawa katika tukio hilo kijijini Kasulo. 
  
Chanzo
 cha mauaji hayo kimeelezwa kuwa ni uhasama wa muda mrefu kati ya 
wananchi na wafugaji hao, wanaodaiwa kuingiza mifugo kijijini hapo bila 
ridhaa ya Serikali ya Kijiji, bali kwa mgongo wa vigogo wa idara za 
Uhamiaji, na Mifugo. 
  
Waliouawa
 kwenye tukio hilo lililotokea Septemba 19, mwaka huu, saa 11:00 jioni 
ni Ngabo Godfrey (24) na mwingine ambaye hakutambulika mara moja na 
kwamba ng’ombe waliouawa kwa kuchomwa mikuki na kukatwa mapanga, nyama 
zao zilichukuliwa na wananchi hao kwa ajili ya kitoweo. 
  
Mwenyekiti wa Kitongoji cha Ngoma B, kijijini Kasulo, lilipotokea tukio hilo, Simon Nzakaya, aliieleza JAMHURI
 kuwa miili ya wafugaji hao ilipatikana siku moja baada ya mauaji na 
tayari watu wanane waliokuwa wakishikiliwa na vyombo vya dola kwa 
mahojiano zaidi. 
  
Hata
 hivyo, baadhi ya watu walizitupia lawama baadhi ya mamlaka za Serikali 
zikiwamo Idara ya Uhamiaji, Mifugo na Halmashauri ya Wilaya kupitia 
Kitengo cha Sheria, kwa kushindwa kuchukua hatua mapema mara baada ya 
kuombwa kuingilia kati mambo ya uvamizi wa wafugaji katika eneo hilo. 
  
“Mgogoro
 huu si wa leo… wenzetu Idara ya Uhamiaji, Mifugo na Mwanasheria wetu wa
 Halmashauri walishakuwa mawakala wa wafugaji na wahamiaji haramu… na 
ndiyo sababu za mauaji kama haya maana wananchi wameshachoka… na 
ninakueleza ndugu mwandishi huu ni mwanzo tu, iwapo Serikali 
haitazinduka ikasafisha idara hizi na kuleta wazalendo, mauaji 
hayatakoma maana wafugaji wanaoingia kinyemela kupitia mlango wa nyuma 
ni wengi,” amesema mmoja wa wanakijiji aliyeomba kutotajwa jina 
gazetini. 
  
Gazeti
 hili, mbali ya kuzungumza na baadhi ya wananchi kwenye vitongoji vya 
Njiapanda na Ngoma B ilikofukuta migogoro hiyo na kuelezea kero 
wanazokumbana nazo kutoka kwa wafugaji na wahamiaji haramu 
inayosababishwa na kukithiri kwa rushwa, pia limefanya mahojiano na 
baadhi ya viongozi wa maeneo hayo wakatoa dukuduku zao. 
  
Brighton
 Kemikimba, Mwenyekiti wa Kitongoji cha Njiapanda, amesema tatizo la 
uingizaji wa mifugo kutoka ndani na nje ya nchi kuja kijijini hapo na 
maeneo mengine ndani ya Wilaya ya Ngara, limechangiwa kwa kiasi na idara
 ya Mifugo na ya Uhamiaji ambazo kwa miaka mingi zimekuwa zikiwapa 
wafugaji hao vibali kinyume cha sheria. 
  
“Idara
 hizi mbili, hususan ya uhamiaji imesababisha maeneo tunayoishi kugeuzwa
 kambi za kufugia mifugo ya wahamiaji… maana wamekuwa wakifika kisha 
kujimilikisha maeneo ya kufugia na kuishi bila kufuata taratibu za 
umilikaji wa ardhi. 
  
“Watu
 tukiwa hatuna hili wala lile tunashtukia wapo kijijini… kama viongozi 
tumeshafanya vikao vya kijiji, mikutano ya hadhara ya vijijji na kutoa 
maazimio hawa watu waondoke katika ardhi yetu na warudi walikotoka, 
lakini cha kushangaza wamekuwa wakikimbilia Uhamiaji na kupewa ‘pamiti’ 
kinyemela, jambo ambalo limezidisha migogoro kila uchao na hatujui la 
kufanya,” amesema Kemikimba. 
  
Alifafanua;
 “Sheria ya Ardhi Namba 5 ya mwaka 1999 ya Vijiji inatoa mamlaka kwa 
Serikali ya Kijiji kuyajadili maombi ya watu wanaoomba kuhamia kijiji 
husika, na mkutano wa hadhara wa kijiji ndiyo hutoa mamlaka kwa wahusika
 kuishi eneo hilo, lakini hayo yote hayafanyiki, badala yake mamlaka za 
kijiji zimeporwa na Uhamiaji.” 
  
Naye
 Silvester Katongale, mjumbe wa Serikali ya Kijiji cha Kasulo, amesema 
malalamiko yao kuhusiana na Idara ya Uhamiaji kugawa vibali kwa 
wahamiaji ambao wamekuwa wakivamia maeneo yao bila kufuata taratibu, ni 
ya muda mrefu na kwamba hata Mkuu wa Wilaya aliyekuwapo, Luteni Kanali 
Nyakonji, alijaribu kufuatilia bila mafanikio. 
  
“Huyu
 DC aliwahi kuagiza iundwe kamati ya kufanya sensa ya mifugo 
iliyoingizwa kinyemela ili ijulikane idadi yao, lengo likiwa kuangalia 
uwezo wa kijiji, lakini alikwama na hakuna kilichofanyika, badala yake 
wahamiaji na mifugo yao wanaendelea kuingia, yaani imekuwa vurugu kubwa 
kwani watu wenye asili ya Rwanda wamekuwa mbogo kana kwamba hii ni ardhi
 yao. 
  
“Wizi
 wa mifugo ya wenyeji umetawala kutokana na wingi wa wafugaji wavamizi 
kuingia kila kukicha na pia kumejitokeza uharibifu mkubwa wa mazingira 
kwani hali ya mazingira ilivyokuwa awali na sasa ni tofauti na 
inavyoonekana, wilaya imeshindwa, hivyo tunamwomba Rais Jakaya Kikwete 
aingilie kati,” amesema Katongale. 
  
Mwingine
 aliyeathiriwa na wimbi la wahamiaji kuvamia na kuweka makazi kijijini 
hapo kinyume cha taratibu, ni Dauda Yunusu, mjumbe wa Serikali ya Kijiji
 na Mjumbe wa Kamati ya Wafugaji na Ardhi katika Kijiji cha Kasulo. 
  
Yunusu
 amesema; “Niliposikia Rais akitoa tamko la kuhakikisha wahamiaji haramu
 wanakamatwa na kurejeshwa kwao nilifarijika nikijua ndiyo mwisho wa 
migogoro hiyo, lakini cha ajabu zoezi [kazi] nzima lilihujumiwa na Idara
 ya Uhamiaji ambayo kwa makusudi iligeuza operesheni hiyo kuwa 
kitegauchumi kwa kuwagawia kinyemela wahamiaji vibali vya kuendelea 
kuishi nchini bila ridhaa ya kijiji husika. 
  
“Unavyoniona
 ndugu mwandishi mimi, Brighton, na Afisa Tarafa ya Nyamiyaga, pamoja na
 Serikali ya Kijiji tumeshitakiwa mahakamani na Evarist David na Medadi 
Muhutu, ambaye ni asili ya Rwanda, lakini ana kibali cha kuishi nchini 
na kwenye kesi hiyo namba 35/2012 tunadaiwa milioni [shilingi] 17 na 
ukichunguza yote ni kwa kuwa tunapigania ardhi yetu, badala ya kuondoka 
wanatuburuza mahakamani, hii ndiyo Serikali tunayoitumikia kwani hata 
halmashauri imetutelekeza kupitia mwanasheria wake,” ameongeza. 
  
Yunusu
 amekwenda mbali zaidi kwa kudai kuwa usimamizi mbovu wa sheria ndiyo 
chanzo cha matatizo waliyonayo, kwani pamoja na Rais Kikwete kutoa tamko
 la kuwaondoa wahamiaji haramu na mifugo yao, watu wanaolisha mifugo 
katika misitu ya hifadhi ukiwamo wa Kimisi hawakuondolewa, badala yake 
walipatiwa vibali vya kuendelea kuishi humo. 
  
Amedai
 pia kwamba wahamiaji haramu waliokamatwa katika Msitu wa Kimisi na 
ardhi ya Kasulo na kuonekana hawana vigezo vya kuishi nchini 
walirudishwa nchini kwao, lakini cha kushangaza mifugo yao ilibaki 
nchini pamoja na wafanyakazi wao wanaolisha mifugo. 
  
Baadhi
 ya wahamiaji haramu waliorudishwa kwao wakiacha mifugo na wafanyakazi 
wao kwenye ardhi ya Tanzania katika Kijiji cha Kasulo ni Benoni 
Mnyechwi, Kadugala, Katubu na watoto wa ndugu wa mzee Bulalisi 
wameondoka huku mifugo yao ikiendelea kubaki yalipo makazi yao katika 
Kitongoji cha Kamuri katika Kijiji cha Kasubo, jambo linaloashiria 
watarudi nchini. 
  
Ameiomba
 Serikali ifanye jitihada za kunusuru hali hiyo, kutokana na ukweli kuwa
 operesheni imefanyika ndivyo sivyo kinyume cha matarajio ya Rais Jakaya
 Kikwete, hasa ikizingatiwa kuwa bado kuna wahamiaji wanaoishi katika 
Msitu wa Hifadhi Kimisi wakiwa na mifugo yao. 
  
“Serikali
 iingilie kati hawa watu waondolewe katika Msitu wa Kimisi na waliohodhi
 ardhi ya wazawa kinyemela kwa kisingizio cha kuwa na vibali walivyopata
 kinyemela waachie ardhi ya watu, vinginevyo yanaweza kutokea machafuko 
au mauaji kama yaliyotokea ya wafugaji na mifugo yao kuuawa kinyama. 
  
“Na
 hili si la kufanywa tena na Serikali ya Ngara maana imeshindwa 
kudhibiti mianya ya rushwa, iundwe tume kuchunguza na kunusuru hali hii 
maana Uhamiaji wamekuwa wakitoa vibali vinavyowaruhusu kuishi nchini kwa
 muda, jambo ambalo limewafanya wananchi kukosa imani na idara hiyo,” 
amesema. 
  
Kwa
 upande wake, Mwenyekiti wa Kijiji cha Kasulo, Yusuph Katula, akifafanua
 utaratibu wa kuomba vibali vya kuishi nchini kwa muda, amesema kwa 
kawaida mwombaji wa kibali cha kuishi eneo husika anapaswa ajadiliwe na 
kijiji baada ya kupeleka maombi kwenye Halmashauri ya Kijiji na si 
vinginevyo. 
  
“Kijiji
 kinapomjadili na kumkubali wanampa muhtasari wa kikao kile ili apeleke 
Uhamiaji Wilaya, ambao nao hupeleka mkoani ambako hutoa ‘pamiti’ na huo 
ndiyo utaratibu tofauti na sasa, kwani Uhamiaji wanatoa vibali hivyo 
kama njugu na kuzidisha migogoro isiyo ya lazima kwani wahamiaji wa 
kijiji chetu hawakupata vibali walivyonavyo kwa kufuata utaratibu, 
wamevipata kwa njia ya panya, rushwa imetawala,” amesema. 
  
Kutokana
 na hali hiyo, viongozi waliokuwa wakiongoza zoezi hilo [Operesheni 
Kimbunga] hawakuhusishwa kwenye uamuzi ili kujiridhisha na vielelezo vya
 wahamiaji haramu kwa aliye halali kuishi na asiye halali, badala yake 
wengi wa wahamiaji haramu waliachwa na Polisi wakishirikiana na Uhamiaji
 na hata walipohoji walitishiwa maisha na hadi sasa wanaishi kwa kuhofia
 usalama wao. 
  
Akinukuu
 kumbukumbu za Serkali ya kijiji, alidai kuwa Aprili 24, mwaka jana, 
Serkali ya kijiji ilitoa orodha ya wafugaji wanaodaiwa kuvamia kijijini 
hapo, wakiingia na maelfu ya mifugo yao wakiwataka kuondoka na kuomba 
msaada kutoka mamlaka husika kwa maandishi kuwaondoa, lakini hakuna 
hatua yoyote iliyochukuliwa. 
  
Ameongeza
 kuwa Desemba 12, mwaka jana, pia uongozi  wa wilaya ulijulishwa kwa 
taarifa ya kumtaka mfugaji mwingine kuingia kijijini hapo kwa nguvu naye
 kuondoka Desemba 28, kulitolewa taarifa kama hiyo, lakini hakuna hatua 
yoyote iliyochukuliwa hadi sasa. 
  
Diwani
 wa Kata ya Kasulo inayodaiwa kuongoza kwa kuathiriwa zaidi na wimbi la 
ufugaji usio na tija na wahamiaji wenye vibali pamoja na wale wanaotoka 
wilaya jirani na mikoa, wangeweza kudhibitiwa kama mamlaka za wilaya na 
mkoa zingeweza kuingilia katika kukisaidia kijiji mapema kabla ya hali 
hiyo kujitokeza. 
  
Ameongeza
 kuwa hatua ya Idara ya Uhamiaji kutoa vibali kwa wahamiaji kutoka nchi 
jirani na kutumia vibali hivyo kuingiza maelfu ya mifugo katika kata 
hiyo na katika hifadhi za Kimisi, Biharamulo na Burigi kumekuwa chanzo 
cha mgogoro huo. 
  
Ameongeza
 kuwa ukiondoa wafugaji kutoka wilaya na mikoa jirani wanaolalamikiwa 
kuingia kinyemela, wengi wanaolalamikiwa ni wahamiaji wanaoingia na 
mifugo yao ama baada ya kupata vibali, au uraia na kisha kuingiza mifugo
 yao bila ridhaa ya kiijiji. 
  
Amesema
 kinachoonekana ni kwa baadhi ya watumishi wa Serikali wasio waadilifu 
kutanguliza zaidi maslahi yao binafsi kunakotokana na mgogoro huo badala
 ya kuupatia ufumbuzi kwa maslahi ya wananchi, wilaya na Taifa. 
  
Diwani
 Kiiiza amedai kuwa suala hilo siyo siri, kila kiongozi na wananchi 
wanatambua kuwa Idara ya Uhamiaji kupitia vibali inavyovitoa ndivyo 
vimekuwa vinatumiwa na wahamiaji hao kama kigezo cha kuingia na maelfu 
ya mifugo yao bila kuomba kuingia kijijini, wakitumia ubabe huku 
kukiwapo tetesi za kukingikiwa kifua. 
  
Katika
 hatua nyingine, Idara ya Mifugo Wilaya imekuwa haichukui hatua hata 
inapojulishwa juu ya kuwapo uingizwaji wa mifugo kutoka nchi jirani au 
wilaya na mikoa jirani, badala ya kuchukua hatua yenyewe hubariki na 
hivyo wanakijiji kupitia Serikali za kijiji kugeuka yatima. 
  
Mkuu
 wa Wilaya ya Ngara,  Costantine Kanyasu, ambaye amekiri kuikuta baadhi 
ya migogoro hiyo, alipohojiwa kwa njia ya simu kuhusiana na malalamiko 
ya zoezi la kukamata na kuwarudisha kwao wahamiaji haramu kutawaliwa na 
rushwa, amekana Uhamiaji kugeuza zoezi hilo kuwa kitegauchumi chao huku 
akiahidi kufuatilia ili kubaini ukweli halisi. 
  
Aidha,
 amekiri kupokea baadhi ya malalamiko, ingawa hata hivyo, amedai 
yalikuwa yakielekezwa kwa mamlaka nyingine kwa hatua na ofisi yake 
kupewa nakala kutoka kijijini hapo, na sasa atakachokifanya ni kuchukua 
hatua za haraka kuhakikisha tukio kama hilo halitokei tena. 
  
Kanyasu
 aliyehamia wilayani hapa hivi karibuni, amekiri kuwapo kwa baathi ya 
changamoto zinazotolewa na wananchi, lakini zikiwamo za baadhi ya 
mamlaka kulalamikiwa kutowajibika juu ya tukio la mauaji. Uchunguzi wake
 unaendelelea. 
  
SOURCE: JAMHURI MEDIA  
 |