Friday 13 September 2013

Busara za kina Job Ndugai, Mbowe na askari wa Bunge

 
Posted  Jumatano,Septemba11  2013  saa 12:1 PM
Kwa ufupi
Badala yake, Ndugai akatumia jazba, akimtaka Mbowe akae chini na alipokaidi, akaita polisi waje kumtoa nje, hapo ndipo vurugu zikaanza.


Mambo yaliyotokea bungeni mjini Dodoma wiki moja iliyopita hayawezi kupita bila kujadiliwa. Mengi yamezungumzwa ikiwamo chanzo cha vurugu kiasi cha baadhi ya wabunge kuburutwa kama vibaka ndani ya ukumbi huo.
Kwangu mimi naona kuna ukosefu wa busara kwa viongozi wetu kiasi cha kuwa sababu ya vurugu za mara kwa mara ndani ya ukumbi huo. Ninamzungumzia na hata kutofautiana na Naibu Spika, Job Ndugai ambaye mara nyingi hapendi kusumbuka pale utata unapojitokeza katika vikao, bali huishia kuita polisi.  Siku ya tukio hilo, baada ya Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe kuomba nafasi ya kuzungumza baada ya kura kupigwa na wabunge wa CCM kushinda, ilitakiwa busara kidogo ili kuepusha zahma ile.
Badala yake, Ndugai akatumia jazba, akimtaka Mbowe akae chini na alipokaidi, akaita polisi waje kumtoa nje, hapo ndipo vurugu zikaanza.
Hivi ingekuwaje kama Mbowe angeachwa azungumze, kisha Ndugai akamjibu kulingana na hoja yake?
Mbowe naye kama mwanasiasa angekaa chini, kuheshimu kanuni, asingeweza kulalamika kwa kutumia kanuni hizo zilizopo, angekosa nini na kwa nini hakufanya hivyo? Najiuliza, Ndugai angeweza kuahirisha hoja hiyo aijibu katika kikao kingine. Hapo zisingetokea vurugu zozote. Ingekuwaje kama mbunge wa CCM kama vile, Waziri William Lukuvi ambaye pia ni Mnadhimu wa chama hicho, naye angeitiwa polisi? Au, angekuwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda amesimama anahitaji ufafanuzi fulani angekaripiwa vile?
Sikatai kwamba kazi ya polisi ni kulinda amani na utawala wa sheria, lakini haimaanishi kwamba mwenye mamlaka wakati wowote ni kutumia nguvu tu. Busara ya hali ya juu inahitajika kuendesha Bunge letu.
Nasema hivyo kwa sababu Spika wa Bunge letu na naibu wake ni makada wa CCM tena wanahudhuria vikao vya juu vya chama, kwa hiyo uwezekano wa kufanya upendeleo ni mkubwa.  Kwa hiyo, linapotokea suala lenye masilahi ya CCM, wanaweka kando masilahi ya wananchi, wanatetea chama kwanza. Ndicho alichokifanya Ndugai, japo yeye ni mhimili wa Bunge anatumia nguvu nyingi kuitetea Serikali ambayo ni mhimili mwingine.
Hata hivyo, kama askari nao wangekuwa na busara wasingeingia kichwa kichwa,  kufanya walichofanya, bila shaka tusingeona aibu kama hiyo. Busara ya kuendesha vikao kwa kutoa nafasi sawa kwa wabunge na wakati mwingine kuziba mianya ya vurugu bila hata kuita polisi.
Labda kama mapendekezo ya Rasimu ya sasa ya Katiba Mpya yatakubalika ambayo yanataka spika wa Bunge asiwe mwanachama wa chama chochote cha siasa. Kwa hali ilivyo sasa, inamlazimu mno kiongozi wa Bunge kutumia busara za hali ya juu kuendesha vikao.

SOURCE: MWANANCHI