Friday 13 September 2013

Sadc; Ulaya kataeni fedha zinazoibwa Bara la Afrika


Na Peter Saramba, Mwananchi

Posted  Alhamisi,Septemba12  2013  saa 11:21 AM
Kwa ufupi
  • Kampuni kubwa za kibiashara zinatumia udhaifu wa taasisi za serikali kukwepa kulipa ushuru  sahihi.
  • Miongoni mwa nchi zinazotumia udhaifu wa taasisi za serikali ni; Visiwa vya Cayman, Switzerland, Luxembourg,  Bermuda na Visiwa vya Jersey.
  • Mjumbe wa kamati ya PAC wa Uganda, Ssewungu Gonzaga anasema tabia ya wabunge wengi kuweka mbele itikadi za vyama vyao badala ya umma ni kikwazo cha maendeleo.


Kushusha thamani bidhaa na malighafi za Bara la Afrika ukilinganisha na bei halisi ya soko ni mbinu inayotumika zaidi kuiba theluthi mbili ya fedha na rasilimali zinazotoroshwa na wageni.
Mkutano wa 10 wa wabunge wajumbe wa kamati za hesabu za serikali kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Uchumi Kusini mwa Afrika, (Sadc), umekwisha jijini Arusha huku washiriki wakibainisha sababu kadhaa zinazokwamisha vita dhidi ya wizi, ufisadi na uporaji wa rasilimali za umma kutoka nchi zinazoendelea, likiwamo Bara la Afrika.
Pamoja na sababu kadhaa, nchi zilizoendelea katika Bara la Ulaya na Marekani pia zinadaiwa kuchochea wizi wa fedha na rasilimali za umma kwa kukubali kuzihifadhi baada ya kuibwa kwenye mataifa maskini barani Afrika.
Mjumbe wa Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) kutoka nchini Sudan Kusini, Goc Mukleac Mayol, amewatuhumu wahisani kwamba ni walimu wa wizi na uporaji wa fedha na rasilimali katika nchi za Afrika.
“Kama kweli hawa wenzetu (Ulaya na Marekani), wanaotufundisha kuthibiti fedha na rasilimali zetu wana nia njema na Afrika, basi kwanza wakatae kupokea fedha zetu zinazoibwa na kuhifadhiwa kwenye mabenki zao na wawataje ili wajulikane kwa umma badala ya kuwakumbatia,” anasema Mayol.
Mayol anasema tabia ya wizi na ufisadi siyo sehemu ya utamaduni wa Mwafrika bali ni mafundisho kutoka kwa baadhi ya watawala wa kikoloni wanaoendelea kutumia uwezo wa kiuchumi wa nchi zao kupora fedha na rasilimali za Bara la Afrika.
“Hadithi zetu za kale zinatufundisha kuwa kijana mdogo hawezi kuwa mwizi bila kufundishwa na kaka yake mkubwa.
Tunapozungumzia wizi na ufisadi wa fedha na rasilimali za umma barani Afrika, lazima tukubaliane kuwa ni mafundisho kutoka kwa kaka zetu (Ulaya na Marekani), ambao huwalinda wanaotuibia na kuhifadhi fedha zetu kwenye benki zao,” anabainisha Mayol.
Anataja baadhi ya miji mikuu ambako fedha na rasilimali zinazoibwa Afrika zimefidhiwa kuwa London, Switzerland na miji mingine mikubwa ya Ulaya na Marekani.
“Wezi wa fedha za Afrika wanalindwa na serikali za nchi hizo ambazo kila siku zinatuimbia nyimbo na ngonjera za kudhibiti wizi na matumizi mabaya ya rasilimali za umma,” anasema.
Mwenyekiti wa PAC Tanzania, Zitto Kabwe anasema tatizo la wizi na utoroshaji wa fedha na rasilimali za umma kutoka nchi zinazoendelea kwenda nchi zilizoendelea ni janga kubwa linalohitaji kushughulikiwa kikamilifu.
 
Zitto anasema kati ya mwaka 2000-210 zaidi ya dola 844 bilioni za Kimarekani zilitoroshwa kutoka nchi zinazoendelea kwenda nchi za Ulaya na Marekani. Asilimia 69 ya fedha hizo, sawa na dola 582 bilioni za Marekani zimetoroshwa kutoka barani Afrika, ndani ya kipindi hicho.

Kwa mujibu wa Zitto, miongoni mwa mbinu zinazotumika kutorosha fedha na rasilimali za nchi za Afrika,  ikiwamo Tanzania ni wizi, rushwa, bakshishi kupitia mikataba (Ten Percent), ukwepaji kodi na kushusha thamani za bidhaa au maligafi kutoka Bara la Afrika.

SOURCE: MWANANCHI