Monday 16 September 2013

Hivi ndivyo raia wa Ujerumani walivyoshibishwa demokrasia


Na Othman Miraji,Mwananchi

Posted  Jumatatu,Septemba16  2013  saa 12:59 PM
Kwa ufupi
Demokrasia haisemi kwamba walio wengi ndio wana haki ya kila kitu, haitaki kuwepo udikteta wa walio wengi, lakini inataka upinzani usikilizwe na upewe nafasi huru ya kuwashawishi walio wengi wabadilishe mawazo yao, kama inawezekana. 

Bado siku sita raia wa nchi hiyo kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu ambapo kitaifa itakuwa ni Septemba  22, mwaka huu. 
Raia wa Ujerumani wamebakiza siku sita kushiriki katika uchaguzi mkuu nchini humo huku kila chama kikiwa na Itikadi zake.
Hakuna utawala wowote wa kisiasa duniani usiojigamba kwamba ni wa kidemokrasia, hata zile nchi ambazo waziwazi unaziona ni za kidikteta.
Hata pale Wajerumani wanaposema demokrasia yao ni sawa kabisa na tafsiri asilia ya neno hilo utawala ambao chimbuko lake ni matakwa ya wananchi lakini hivyo sivyo asilimia mia moja katika utekelezaji.
Katika miji ya Uyunani ya kale, ambako neno demokrasia lilianzia, wanaume waliokuwa huru walikusanyika masokoni na kuamua juu ya sheria za kutumiwa katika miji yao.
Hata hivyo, katika miji mikubwa ya kisasa duniani, jambo kama hilo ni muhali kutekelezeka. Wananchi wanaweza tu kuelezea maoni yao kupitia wawakilishi wao waliowachagua. Siasa ni ushindani wa kuwania madaraka. Hivyo ndivyo ilivyo pia kwa nchi ya Ujerumani. Katika siku ya uchaguzi wapiga kura huamua vipi mamlaka ya Serikali yagawiwe katika kipindi cha miaka minne ijayo ya bunge.
Vyama vya kisiasa na wanasiasa baada ya kuchaguliwa hutakiwa kutilia maanani mkondo wa hisia, maoni na matakwa ya wananchi unavyokwenda kabla ya kufikia maamuzi.
Hali hii inafanya kila Serikali, ambayo wananchi wanaweza kuiondoa kutoka madarakani, ijitahidi kuhakikisha wananchi wanaridhika nayo.
Ni wazi kwamba pale Serikali yeyote inapohisi haiwezi kuondolewa kutoka madarakani na wananchi basi inakuwa haijali na hujifanyia mambo inavyotaka.
Uchaguzi hutoa nafasi kwa upinzani kuingia madarakani pale wananchi wanapoamua wanataka mabadiliko.
Raia ndio wenye kuamua juu ya namna ya kugawa madaraka ya kisiasa na ni ndiyo wenye kuhalalilsha mgawo huo.
Hata raia wasiokwenda kupiga kura nao wana ushawishi juu ya Serikali ijayo. Wingi wa wapiga kura unaathiri matokeo ya uchaguzi na sura ya Serikali ijayo.



Msingi wa demokrasia ni wengi wape. Programu ya kundi liliopata kura nyingi ndio inayotekelezwa, bila ya shaka kutilia maanani pia maoni ya walio wachache.
Demokrasia haisemi kwamba walio wengi ndio wana haki ya kila kitu, haitaki kuweko udikteta wa walio wengi, lakini inataka upinzani usikilizwe na upewe nafasi huru ya kuwashawishi walio wengi wabadilishe mawazo yao, kama inawezekana.
Nchini humo upinzani hukaa chonjo kusubiri kuingia madarakani pale wananchi wanapotaka yafanyike mabadiliko.
Raia wote wa Ujerumani wana haki ya kupiga na kupigiwa kura bila ya kujali dini, kiwango cha elimu, jinsia, kipato na kazi gani ambayo  anaifanya.
Shuruti ni kwamba mpiga kura asiwe chini ya umri wa miaka 18, japokuwa baadhi ya mikoa inaruhusu wenye umri wa miaka 16 kushiriki katika chaguzi za mabunge ya mikoa.
Tangu mwaka 1992  ulipotiwa saini Mkataba wa Maastricht raia wa nchi za Umoja wa Ulaya wanaweza kupiga kura katika chaguzi za Serikali za mitaa.
Shirikisho la Jamhuri ya Ujerumani ni demokrasia inayotegemea vyama ambavyo hupigania kuungwa mkono programu zao.
Wajerumani wanapopiga kura hutilia maanani sana programu za vyama, viongozi wa vyama hivyo, na kwa kiwango kidogo wagombea wa vyama hivyo.
Christian Democratic, CDU, chama kinachoongozwa na Kansela wa  sasa, Angela Merkel, kwa muda wa miaka 41 kimekuwa kikishiriki katika Serikali mbalimbali za mseto.
Kansela wa kwanza wa Ujerumani na wa kutoka Chama hicho, Konrad Adenauer ( 1949-1963),  alikuwa alama ya kuifungamanisha Ujerumani na Jumuiya ya Kujihami ya Magharibi, NATO, na Umoja wa Ulaya.
Pia Kansela wa kutoka Chama hicho, Helmut Kohl (1973-1998) anatajwa kuwa ni muasisi wa Umoja wa Ujerumani. Angela Merkel ndiye sasa mgombea wa ukansela wa chama hicho
Social Democratic, SPD, kutokana na programu yake ya Godesberg ya mwaka 1959, kiliachana na wito wa kutaka kuweko mapambano ya kitabaka na kikakubali kuweko uchumi wa masoko, lakini wenye kutilia maanani maslahi ya watu wasiojiweza.
Mwishowe kilikubali nchi hii ifungamanishwe na kambi ya Magharibi. SPD imeunda Serikali za mseto na vyama tofauti.
Mwenyekiti wake ni Sigmar Gabriel, lakini mgombea wake wa ukansela hivi sasa ni Peer Steinbrueck.
Christian Social ni chama ndugu na CDU, lakini kinafanya shughuli zake tu katika mkoa wa kusini wa Bayern, ambako huko CDU haiko.
Tangu mwaka 1957  Waziri kiongozi wa Mkoa wa Bayern alitokea chama hicho. Kiongozi wake hivi sasa ni Horst Seehofer. CSU hakina mgombea wa ukansela, lakini kinamuunga mkono Angela Merkel.
Chama cha kiliberali cha Free Democratic kwa muda kimekuwa kikishiriki katika serikali za mseto. Kinataka Ujerumani ibakie imefungamana na Umoja wa Ulaya na Jumuiya ya NATO,  na kuweko nchini uchumi wa masoko huru. Kiongozi wake hivi sasa ni Philipp Rösler, ambaye pia ni waziri wa uchumi. Hakina mgombea wa ukansela.
Chama cha Kijani, kilichoundwa mwaka 1980, kinapigania ulinzi wa mazingira na usawa wa kijinsia katika nyadifa za kisiasa na serikalini. Hakina mgombea wa ukansela. Viongozi wake wenza ni Claudia Roth na Cem Ozdemir.
Die Linke, chama cha  mrengo wa shoto, kinapinga Ujerumani kuwemo katika Jumuiya ya kijeshi ya NATO na hakiitaki sarafu ya Ulaya ya Euro.
Katika uchaguzi wa mwaka 2009 chama hicho kilijipatia asilimia 11.9. Kinapinga jeshi la Ujerumani kujiingiza katika nchi za nje.
Mafanikio au kuhindwa kwa chama chochote kati ya hivyo ndiko kutakoamua Serikali ya namna gani wanayostahili kuwa nayo Wajerumani baada ya Septemba 22

SOURCE:MWANANCHI