Wednesday 25 September 2013

Kuwagwaya wahamiaji haramu tutaumia

Rais Jakaya Kikwete 


Posted  Jumatano,Septemba25  2013  saa 24:0 AM
Kwa ufupi
Tumetiwa moyo na ufafanuzi wa Rais ambao tunadhani haukuacha shaka yoyote kwa yeyote aliye na nia njema na nchi yetu.


Rais Jakaya Kikwete mwishoni mwa wiki alijikuta katika wakati mgumu akiwa ziarani nchini Marekani alipolazimika kutumia muda mrefu kukanusha madai kwamba operesheni ya kuwaondoa wahamiaji haramu nchini imelenga kuwaondoa wakimbizi. Hatua hiyo ya Rais Kikwete imekuja baada ya kuwapo kwa upotoshaji wa makusudi kuhusu uamuzi wa Serikali kuwarudisha makwao wahamiaji wote walioingia nchini kinyume cha sheria.
Upotoshaji huo wa makusudi ulianza taratibu mwezi uliopita mara tu baada ya Rais Kikwete kuwapa wahamiaji hao haramu wiki mbili kurudi makwao na kusema muda huo ukiisha ingeanzishwa operesheni ya kuwaondoa watu hao kwa nguvu. Bila shaka Rais alipoondoka nchini kuelekea Marekani hakuwa na chembe ya fununu kwamba upotoshaji huo ungesababisha awekwe ‘kiti moto’ na moja ya Kamati za Bunge la nchi hiyo kuhusu madai hayo.
Kinachotutatiza hapa siyo Rais wetu kutoa ufafanuzi, isipokuwa kile kinachoonekana kama usahaulifu kwa upande wa jumuiya ya kimataifa kwamba Tanzania kwa miongo mingi imekuwa kimbilio kubwa la maelfu kwa maelfu ya wakimbizi kuliko nchi nyingine yoyote barani Afrika. Hivyo, kufikiri kwamba Tanzania inaweza ghafla kubadili sera yake ya kuhifadhi wakimbizi na badala yake kuwa moja ya nchi zinazowanyanyasa, kuwatesa na kuwatenga ni jambo ambalo hakika haliingii akilini. Tanzania sasa inahifadhi wakimbizi 264,000 kutoka Congo (DRC) na Burundi katika kambi zilizopo mkoani Kigoma.
Tumetiwa moyo na ufafanuzi wa Rais ambao tunadhani haukuacha shaka yoyote kwa yeyote aliye na nia njema na nchi yetu. Kwamba Tanzania haijamfukuza mkimbizi hata mmoja, isipokuwa waliofukuzwa ni wahamiaji haramu walioingia na kuishi nchini kinyume cha sheria na taratibu za uhamiaji. Kama alivyosema mwenyewe, Tanzania haina sababu ya kuwafukuza wakimbizi na kama ingelazimika kufanya hivyo, taratibu za kimataifa zingefuatwa, ikiwa ni pamoja na kuwasiliana na Umoja wa Mataifa na mamlaka za nchi walizotoka.
Sasa hapo shida iko wapi? Hivi wapotoshaji wa Operesheni hiyo wana ajenda gani? Kwamba ni haki kweli Tanzania iendelee kubeba mzigo wa wakimbizi, huku pia ikiendelea kuwa kichaka cha wahamiaji haramu ambao wanashutumiwa kwa vitendo vya ujambazi, utekaji nyara mabasi, uvamizi wa misitu ya asili na hifadhi? Ni haki kweli waachwe waendelee kuingiza maelfu ya mifugo katika maeneo tengefu na kusababisha mmomonyoko wa ardhi? Ni haki kweli Watanzania waendelee kuishi kama mateka na watumwa katika nchi yao kwa kuogopa kuwatimua wahamiaji haramu wanaosababisha raia kuishi maisha ya zahama na hofu?
Sisi tunasema Rais Kikwete na Serikali yake wasirudi nyuma mpaka hapo mhamiaji haramu wa mwisho atakapokuwa ameondoka katika ardhi yetu. Tunaambiwa kwamba wahamiaji haramu 194 waliorudishwa makwao wamekataliwa na nchi zao na kurejeshwa tena nchini. Tunasema watu hao wakabidhiwe kwa UN, kwani Tanzania tayari imetimiza wajibu wake.
Pamoja na yote hayo, lazima tukubali ukweli kwamba nchi yetu imefanywa shamba la bibi kutokana na udhaifu wa watendaji katika ngazi zote za uongozi kuendekeza vitendo vya rushwa. Wahamiaji haramu wengi hawakuingia nchini kwa kificho, bali walifanya hivyo mchana kweupe na kwa baraka zote za baadhi ya viongozi wa vitongoji hadi wilaya. Ni vyema sasa Serikali ikafunga ukurasa huo wa aibu wa wahamiaji haramu kuiona nchi yetu kama haina wenyewe.

SOURCE: MWANANCHI