Thursday 26 September 2013

‘Kwa Babu’ wampokea Pinda kwa mabang



 
Na Mussa Juma

Posted  Alhamisi,Septemba26  2013  saa 24:0 AM
Kwa ufupi
“Wananchi wanataka amani kwani migogoro imeshasababisha vifo na mali nyingi kupotea sasa tunataka amani,”

Samunge. Wakazi wa Kata ya Samunge, wilayani Ngorongoro Mkoa wa Arusha, jana walimpokea Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kwa mabango wakiomba Serikali iligawe Jimbo la Ngorongoro na ikomeshe mapigano ya kikabila.
Wananchi wa Kijiji cha Yasimdito, wakiwamo wanafunzi walisimama pembeni mwa barabara na mabango hayo na Waziri Mkuu alilazimika kusimama na kuwataka wananchi hao kufafanua maudhui ya mabango hayo.
Diwani wa Kata hiyo, Jackson Sandea alisema wananchi hao ambao ni Wasonjo wamechoshwa na vita na Wamasai wa koo ya Loita kugombea ardhi na kwamba wanataka mipaka ianishwe.
“Wananchi wanataka amani kwani migogoro imeshasababisha vifo na mali nyingi kupotea sasa tunataka amani,” alisema Sandea.
Kiongozi wa mila wa jamii ya Wasonjo (Batemi), Mwanamiji Peter Dudui alisema tangu uhuru, jamii yao yenye watu wachache haijawahi kuwa na mbunge wala kiongozi mwingine wa kuchaguliwa wa ngazi ya wilaya au mkoa. “Waziri Mkuu, tunaomba tuwe walau na jimbo letu kwani kutokana na uchache wetu, hatuwezi kupata mbunge. Pia tunaomba kupatiwa huduma bora za maji na elimu,” alisema Dudui.
Waziri Mkuu alisema Serikali itafanyia kazi maombi ya wananchi hao ili kuhakikisha wanaishi kwa amani na kupata maendeleo.

“Nadhani kama hoja ni kupata huduma muhimu, Serikali inaweza kutazama kama mnaweza kuwa na halmashauri mbili katika wilaya hii,” alisema.
Kuhusu mgogoro wa ardhi, alizitaka pande zote kumaliza uhasama na kwamba Serikali itaendelea kudumisha amani na kuhakikisha vijiji vinapimwa.

SOURCE: MWANANCHI