Wednesday 25 September 2013

Kutengwa EAC tunahitaji mkakati mpya

Waziri wa Afrika Mashariki,Samuel Sitta 


Posted  Jumanne,Septemba24  2013  saa 24:0 AM
Kwa ufupi
Hoja ya Tanzania hapa ni kwamba miradi inayozungumziwa na nchi hizo tatu haitofautiani hata kidogo na ile iliyojadiliwa mwaka jana chini ya uenyekiti wa aliyekuwa Rais wa Kenya, Mwai Kibaki.

Hatua ya Serikali kukiri hadharani kwamba nchi za Kenya, Rwanda na Uganda kutoihusisha Tanzania katika mambo yanayohusu Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), kunatishia uhai wa jumuiya hiyo ni ishara kwamba mpasuko katika chombo hicho ni mkubwa mno kuliko wengi tulivyodhani.
Mipasuko baina ya nchi na nchi au miongoni mwa nchi zilizo katika jumuiya kama zilivyo nchi wanachama wa EAC ni jambo la kawaida. Hata hivyo, migogoro kama hiyo hutatuliwa kufuatana na taratibu za kidiplomasia na kiitifaki zilizopo. Tulitegemea tofauti zilizopo miongoni mwa baadhi ya nchi wanachama wa jumuiya hiyo zitatuliwe kwa kufuata taratibu hizo.
Hivyo, Waziri Samuel Sitta alipojitokeza hadharani wiki iliyopita na kuzilaumu nchi hizo kwa kuitenga Tanzania, wachunguzi wa masuala ya kidiplomasia waliiona hatua hiyo kama ishara ya nchi za EAC kushindwa kupata suluhisho la migogoro iliyopo. Mgogoro uliopo hivi sasa unafuatia hatua ya Rwanda, Kenya na Uganda kuanzisha ushirikiano wa pamoja katika maeneo ya miundombinu, biashara na visa ya pamoja.
Tanzania imevunjwa moyo na mwenendo wa nchi hizo, lakini imesema kwa vile nchi hizo zimechukua uamuzi huo, Tanzania itapaswa kujiweka kando. Pamoja na Ibara ya 7(3) iliyounda jumuiya hiyo inatoa fursa kwa nchi wanachama kuwa na ushirikiano wa pekee, Tanzania inasema hatua ya nchi hizo tatu ilipaswa kujadiliwa na nchi zote wanachama kabla ya hatua hiyo kuchukuliwa.
Hoja ya Tanzania hapa ni kwamba miradi inayozungumziwa na nchi hizo tatu haitofautiani hata kidogo na ile iliyojadiliwa mwaka jana chini ya uenyekiti wa aliyekuwa Rais wa Kenya, Mwai Kibaki. Miradi hiyo ni pamoja na ujenzi wa reli itokayo Isaki hadi Rusumo mpakani mwa Rwanda na ile ya Ivinza mpakani mwa Burundi. Mkutano huo pia ulikubaliana kushirikiana katika nyanja za nishati na mafuta.
Tanzania pia inazilaumu nchi hizo tatu kwa kulazimisha kuwapo kwa Shirikisho la Afrika Mashariki, huku zikijua kwamba suala hilo liliundiwa kamati ambayo inatazamiwa kutoa ripoti yake katika mkutano wa wakuu wa nchi Novemba mwaka huu. Msimamo wa Tanzania ni kwamba ina uzoefu wa muda mrefu katika masuala ya muungano, hivyo haitaki kuburuzwa na kuingizwa kichwakichwa katika mambo yanayohitaji tathmini jadidi na umakini mkubwa kabla ya kuyatekeleza.
Hata hivyo, zipo tetesi kwamba Tanzania imeziudhi nchi hizo kwa mwendo wake wa kinyonga katika kutoa msimamo katika mambo mengi nyeti, ikiwa ni pamoja na: Kuanzisha visa ya pamoja; Suala la umiliki wa ardhi; Sarafu ya pamoja; na Kuanzishwa haraka kwa Shirikisho la Afrika Mashariki. Tanzania inaonekana kwa nchi hizo kutokuwa na utashi wa kisiasa na kudaiwa kuegemea zaidi katika umoja wa nchi za SADC badala ya EAC.
Lakini suala lisilozungumzwa hadharani ni hofu iliyozikumba nchi hizo kutokana na fursa za kiuchumi ilizonazo Tanzania hivi sasa, kiasi cha kuiwezesha kuipiku hata Kenya kama nchi yenye uchumi mkubwa kuliko nyingine katika Ukanda huu katika miaka michache ijayo. Hivyo, katika hali ya sasa Tanzania haina sababu ya kutaharuki. Ni kwa manufaa yake kubaki katika EAC kama mwanachama, lakini kama Waziri Sitta alivyosema, isikubali kuburuzwa na kuingizwa kichwakichwa katika mambo yasiyo na tija kwa wananchi wa Tanzania.

SOURCE: MWANANCHI