Thursday 5 September 2013

Kwanini timua timua ya CCM inalalia kwa Wazanzibari?

“Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete aliwahakikishia  Watanzania wote, narudia wote, uhuru wa kutoa maoni kwa upeo wao, na waseme wanachotaka kukisema, Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Warioba vile vile naye akarejea yale yale aliyosema Kikwete
 
Na Joyce Mmasi, Mwananchi  (email the author)

Posted  Jumatano,Septemba4  2013  saa 12:10 PM
Kwa ufupi
Mansour aliwahi kuwa waziri asiyekuwa na Wizara ya Maalumu katika utawala wa awamu ya saba  ya Dk Ali Mohammed Shein, pia aliwahi kuwa naibu waziri wa Wizara ya Kilimo kabla ya kuwa Waziri wa Maji, Ujenzi, Nishati na Ardhi katika utawala wa Rais Mstaafu Amani Abeid Karume.


Hii si mara ya kwanza kwa CCM kufukuza wanachama wake wa upande wa Zanzibar wanaoonekana kuwa na misimamo tofauti.
Miaka ya nyuma iliwafukuza aliyekuwa Waziri Kiongozi Maalim Seif Sharif Hamad, ambaye kwa sasa ni Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF).
Wiki iliyopita Chama Cha Mapinduzi (CCM) kilibariki rasmi kufukuzwa uanachama kwa mwakilishi wake wa Jimbo la Kiembesamaki, Mansour Yussuf Himid kwa kile kilichoitwa  usaliti kwa chama hicho kwa kuunga mkono Muungano wa mkataba.
Kufukuzwa kwa Mansour, kunakuja baada ya CCM  Taifa kupokea uamuzi kutoka chama hicho Mkoa wa Mjini Magharibi, Zanzibar ambapo mwanachama wake huyo anatoka ya kutaka afukuzwe kwa madai ya kupinga sera ya Muungano wa Serikali mbili.
Wakati CCM ikimfukuza Mansour, imetengua uamuzi wa uongozi wa chama hicho Mkoa wa Kagera wa kuwafukuza madiwani wake wanane.
Wanane hao walifukuzwa na CCM Mkoa kufuatia kukaidi agizo la mwenyekiti wao, Constancia Buhiye kuonekana kuhusika katika mgogoro baina ya Meya Dk Anatory Amani na Mbunge wa Bukoba Mjini, Balozi Khamis Kagasheki.
Mansour aliwahi kuwa waziri asiyekuwa na Wizara ya Maalumu katika utawala wa awamu ya saba  ya Dk Ali Mohammed Shein, pia aliwahi kuwa naibu waziri wa Wizara ya Kilimo kabla ya kuwa Waziri wa Maji, Ujenzi, Nishati na Ardhi katika utawala wa Rais Mstaafu Amani Abeid Karume.
Kwa muda mrefu, mwanasiasa huyo ameonekana kuchukizwa na kile anachokiita matatizo ya Muungano anayodai kuwa yanaikandamiza Zanzibar, msimamo unaoungwa mkono na Wazanzibari walio wengi wakiwemo baadhi ya wana- CCM, ingawa hakuna aliyekuwa tayari kusimama wazi kueleza msimamo wake hadharani kama alivyofanya.
Hata hivyo, hii si mara ya kwanza kwa CCM kufukuza wanachama wake wa upande wa Zanzibar wanaoonekana kuwa na misimamo tofauti.
Chama hicho kimewahi kufanya hivyo miaka ya nyuma kwao Maalim Seif Sharif Hamad aliyekuwa Waziri Kiongozi, pamoja na aliyekuwa Rais wa nane wa Zanzibar na makamu wa rais wa Jamhuri ya Muungano, Mzee Aboud Jumbe Mwinyi.
Vilevile, CCM imewahi kuwafukuza aliyewahi kuwa Naibu Waziri wa Mambo ya ndani, Hamad Rashid Mohamed, Alhaji Pandu, Machano Khamis Ally, Shabani Khamis Mloo, Hatibu Khasan  na Sudi Yusuph Mgeni.
Wakati ikiwafukuza wazanzibar, CCM haijawahi kuwafukuza uanachama kiongozi au wanachama wake upande wa bara wanaoonekana kutofautiana na msimamo wa chama.
Hali hii ya kuwa wepesi kufukuza uanachama wanachama na viongozi wake wa Zanzibar, na kupata kigugumizi kwa wa upande wa bara imezua hisia na mitazamo tofauti kwa wafuatiliaji wa masuala ya kisiasa nchini ambao waliopata fursa ya kuzungumzia hali hii wanasema, CCM inawaonea wazanzibar.
Mtazamo wao
Wanahoji iweje CCM imekuwa na wepesi kuchukua hatua kali, dhidi ya wanachama wake kutoka visiwani huku ikiwawia vigumu kufanya vivyo hivyo kwa wanachama wake wa Tanzania Bara.
Mfano wa wazi na mwepesi ni ule wa madiwani wa Mkoa wa Kagera ambao chama kupitia vikao vyake vya juu , NEC na CC vilibatilisha uamuzi wa kuwafukuza licha ya uongozi wa CCM mkoa kutangaza kuwafukuza uanachama na nyadhifa zao zote ndani ya chama.
Je, nini mtazamo wa Wazanzibari kuhusiana na hali hii, Said Miraji ni mwenyekiti wa Chama cha ADC, anasema hali hiyo ni ushahidi tosha kuwa CCM siyo chama cha Wazanzibari na kuwa hakioni shida kumchukulia hatua kiongozi wa ngazi yoyote upande wa Zanzibar tofauti na wale wa upande wa bara.Anasema Miraji kuwa yanayoonekana ndani ya chama hicho ni kiashiria kuwa hakuna kuvumiliana ndani ya CCM hasa upande wa Zanzibar na kwamba Wazanzibari hawatakiwi kupaza sauti zao kwa yale wanayoyaamini.
“Hii inaashiria kuwa CCM siyo ya Wazanzibari, jambo lolote dogo linalofanywa nao linafanywa kuwa kubwa, lakini jambo hilo hilo  likifanywa mwanachama wa bara linaonekana kuwa dogo na hakuna hatua yoyote anayochukuliwa mhusika,” anasema nna kuongeza:
“Siwasemei, lakini wenyewe waone na wajiulize, iweje wajumbe wa CC na NEC, wameshindwa kubariki uamuzi wa Mkoa wa Kagera wa kuwafukuza madiwani, lakini suala la Mansour mwakilishi wa jimbo na mtu mwenye historia kubwa sana katika visiwa hivi, anaonekana hana thamani na anafukuzwa…hili wenyewe wana CCM wanapaswa kulitafakari.”
Miraji anasema mitazamo  tofauti ya mawazo miongoni mwa wanachama ni kukuza ustawi wa demokrasia ndani ya taasisi na kwamba ni vyema kuwe na utamaduni wa kuvumiliana, kuthamini mawazo ya kila mtu hata kama hayaendani na matakwa na msimamo wa taasisi husika.
Miraji pia anaongeza kuwa kuzuia watu kutoa maoni yao ya kile wanachokiamini au kukiwaza ni kuua demokrasia, na kwa kawaida demokrasia ni lazima ianze ndani ya chama…CCM inapaswa ielewe kuwa uhuru wa mawazo sio baina ya chama na chama isipokuwa ni kwa kila mtu mmoja mmoja, popote pale alipo.
 “Na hili sio jambo jipya maana hata marekani mambo ya namna hii yapo, chama kinakuwa na msimamo wake lakini kiongozi anasimama na kuunga mkono sera au mtazamo wa chama kingine kutokana na utashi na mawazo yake….na hili likitokea hakuna kufukuzana, kwanini haya yanatokea kwetu”
Kuogopana
Ambari  Khamis, makamu mwenyekiti wa NCCR- Mageuzi Zanzibar anasema kinachoonekana ni kuwa kuna kuogopana kati ya CCM Bara na  CCM Zanzibar.


“CCM Taifa inaiogopa kamati maalum ya CCM Zanzibar, haiwezekani kuweza kumfukuza mansour ikaogopa kumfukuza diwani…CCM ina hofu, ukiwakatalia nao watawakatalia mambo kadhaa” na ndicho.
Ambari anasema kutokana na kuogopana huko, CCM upande wa Zanzibar ikiamua jambo lake hata kama lina madhara kiasi gani kwa chama, CCM bara inalazimika kulipitisha, na inasababishwa na ukweli kuwa yapo mambo ambayo Bara inahitaji kuyafanya kuwa msimamo wa watanzania na ukweli ni kuwa watanzania bara ndio wanaong’ang’ania zaidi Muungano.
Hata hivyo, anasema kufukuzwa kwa Mansoor hakumpunguzii kitu bali kunamzidishia heshima yake kwa Wazanzibari kutokana na kuonekana dhahiri kusimamia kudai haki za Zanzibar za uchumi na kupata mamlaka kamili.
Kauli ya Mansour Himid
Kwa upande wake, Mansour anaeleza kuwa hakuna jambo baya alilofanya na lililostahili kufukuzwa ndani ya chama hicho.
“Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete aliwahakikishia  Watanzania wote, narudia wote, uhuru wa kutoa maoni kwa upeo wao, na waseme wanachotaka kukisema, Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Warioba vile vile naye akarejea yale yale aliyosema Kikwete.
Vilevile, Dk Ali Mohamed Shein aliwahakikishia  Wazanzibari wote sio kwa tabaka wala chama, kwamba wanao uhuru wa kutoa maoni yao” anasema.
Anaongeza mbali na kauli za viongozi hao katiba zote mbili, ile ya Muungano na ya Zanzibar zinawahakikishia uhuru  na vile vile sheria nayo inawahakikishia uhuru wananchi wake wote
Kwa mtizamo wangu mimi, wakati tunaelekea kwenye mchakatoi huu, huwezi kuwawekea masharti ya aina yoyote… nimemsikia Nape anasema msimamo wa Chama ni serikali mbili, ni jambo la ajabu sana, inabidi tujiulize, tujiulize sisi watanzania hatuna uhuru…kwa maana sasa tunaambiwa watu wazima wa Zanzibar, kila anayeenda pale ni zidumu fikra za mwenyekiti,  ni serikali mbili ondoka…. uko wapi utu na heshima na uhuru wetu,. Hatuwezi kuzuiwa kwa misingi hiyo” anasema.
Mansour anaongeza kuwa hata aliyekuwa makamu mwenyekiti wa CCM, Pius Msekwa aliweka bayana pale alipobainisha kuwa, licha ya sera za chama kuwa ni serikali mbili, lakini ni huru kila mwanachama kutoa maoni anavyoona yeye ni sawa.
“Hili linaloendelea hivi sasa, tafsiri yangu naona wapo watu hasa hapa Zanzibar  ambao wana fikra za kidikteta na mawazo mgando, wanataka kutuadhibu sisi tunaotofautiana na mawazo yao… mimi sijaanza kusema leo, kuhusu msimamo wangu, narejea, mfumo huu wa serikali mbili sikubaliani nao, siwezi kubadili msimamo huu maana nitapoteza utu wangu na jamii itanisuta,” anasema.

source: Mwananchi