Sunday 15 September 2013

Lowassa ‘avamia’ ngome ya Sitta


Na Mwandishi Wetu, Mwananchi

Posted  Jumapili,Septemba15  2013  saa 2:2 AM
Kwa ufupi
Lowassa jana alikuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya miaka 124 ya Shujaa wa Unyanyembe, Mtemi Isike Mwana Kiyungi, yaliyofanyika mkoani Tabora anapotokea Sitta ambaye ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki.


Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa amefanya ziara mkoani Tabora na kusimikwa kuwa Mtemi wa Unyanyembe na mlezi wa watemi akisema watemi na wakuu wengine wa kimila wana nafasi kubwa kuzuia mmomonyoko wa maadili katika jamii.
Lowassa jana alikuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya miaka 124 ya Shujaa wa Unyanyembe, Mtemi Isike Mwana Kiyungi, yaliyofanyika mkoani Tabora anapotokea Sitta ambaye ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Lowassa aliweka jiwe la msingi la ujenzi wa mnara wa kumbukumbu ya Isike. Tukio hilo la kuwa mgeni rasmi na kusimikwa kuwa mtemi ndani ya mkoa huo ulio asili na makazi yake Sitta linaweza kutafsiriwa kisiasa kuwa sawa na Lowassa kuvamia ngome ya mwanasiasa huyo mkongwe.
Sitta na Lowassa wote wanatajwa kutaka kuwania urais wa Tanzania huku kila mmoja akielezwa kuwa na kambi yake ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) akiwa pia na jimbo lake la uchaguzi pamoja na ngome yake kisiasa. (Mwandishi Wetu)
, Mwananchi
Wakati Lowassa ni mbunge wa Monduli mkoani Arusha, Sitta ni mbunge wa Urambo Mashariki, mkoani Tabora, wote wakiwahi kushika nyadhifa za juu kitaifa ambapo Lowassa aliwahi kuwa Waziri Mkuu na baadaye kujiuzulu, wakati huo Sitta akiwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Akizungumza katika hafla hiyo Lowassa alisema: “Hawa machifu wanaweza kusaidia tatizo hili, Mimi kule kwetu Monduli ni Laigwanan mkuu.., kuna wakati maambukizi ya Ukimwi yalikuwa makubwa kwa Wamasai, nikawaita Malaigwanan wezangu nikawaomba waondoe baadhi ya mila zinazochangia hali ile. Tukakubaliana na kupita kijiji kwa kijiji kuelezea na kweli ikaleta mafanikio makubwa, maambukizi yale yakapungua.”
Aidha, Lowassa alipongeza hatua ya kuenzi kumbukumbu hiyo na kusema kuwa kizazi cha sasa kina kila sababu ya kuiga mfano wa Mtemi Isike wa kutetea utu wake huku akiwataka pia wakazi wa Tabora kuwekeza katika mkoa huo aliouelezea kuwa wa kitalii kutokana na historia yake.
Maadhimisho hayo yamefanyika katika Kijiji cha Itetemia ilipo Ikulu ya Mtemi huyo wa Unyanyembe, aliyepigana dhidi ya majeshi Mjerumani, Von prince(Mwana Sakaraga) kuanzia mwaka 1889 hadi 1893.
SOURCE: MWANANCHI