Sunday 15 September 2013

Kisumo: Ndugai, Mbowe wote wana makosa


Mwanasiasa mkongwe nchini, Peter Kisumo 

Na Daniel Mjema, Mwananchi

Posted  Jumapili,Septemba15  2013  saa 2:0 AM
Kwa ufupi
Kisumo ambaye ni mwenyekiti wa Taifa wa Baraza la Wadhamini wa CCM, alisema ameanza kupata wasiwasi kuhusu mhimili wa Bunge hususan kiti cha Spika hasa katika suala la Mbowe.


Moshi. Mwanasiasa mkongwe nchini, Peter Kisumo amezungumzia vurugu zilizotokea bungeni akisema Naibu Spika, Job Ndugai na Kiongozi wa Upinzani, Freeman Mbowe, wote wana makosa.
Kisumo ambaye ni mwenyekiti wa Taifa wa Baraza la Wadhamini wa CCM, alisema ameanza kupata wasiwasi kuhusu mhimili wa Bunge hususan kiti cha Spika hasa katika suala la Mbowe.
Mwanasiasa huyo aliyasema hayo wakati akizungumza na gazeti hili jana ku tokana na vurugu zilizotokea Bungeni wiki iliyopita baada ya Naibu Spika kuamuru kutolewa nje kwa nguvu kwa Mbowe.
Kisumo alisema alichopaswa kufanya Ndugai baada ya Mbowe kukaidi amri ya kutoka nje ni kumwita mpambe wa Bunge (Sergeant at Arm) na kama ataendelea kukaidi alitakiwa kuahirisha Bunge.
“Mbowe alitolewa na Polisi nadhani Naibu Spika alikosea…Mpambe ndiye alipaswa amtoe na akishindwa alipaswa aahirishe Bunge halafu amshtaki kwenye kamati husika,” alisema Kisumo.
Kisumo alisema kitendo cha Ndugai kuamuru Polisi kuingia ndani ya Bunge ambao wamefunzwa kutumia nguvu, kilikuwa ni makosa makubwa na kusisitiza katika hilo Ndugai alikosea.
Hata hivyo alisema hata Mbowe, naye alikuwa na makosa pale alipokataa kutii maagizo ya kiti (Naibu Spika).
“Mbowe na chama chake kisichukulie ubabe wao katika mikutano ya hadhara ambayo haina lugha ya kibunge na kuzipeleka bungeni haya ni makosa makubwa,” alisema.
Kisumo alisema binafsi anapenda vyama vingi lakini hapendi aibu ya kupigana mahali patakatifu kama bungeni na kuutaka upinzani pamoja na uchache wao Bungeni, kushindana kwa hoja zenye nguvu.
“Vyama vya upinzani haviwezi kushinda hoja yoyote bungeni itakayoamuliwa kwa njia ya kura kwa sababu ya uchache wao… Wao waendelee kutoa hoja na mwisho wa siku umma utawaelewa,”alisema.
Kisumo alisisitiza kuwa Chadema wasichukulie mambo yao ya majukwaani yaliyojaa kile alichodai tamaa ya madaraka kuongoza nchi wakayapeleka bungeni ambako kuna kanuni na taratibu
SOURCE: MWANANCHI