Friday 13 September 2013

Mbilimbi hutumika kufanyia mazoezi ya kubeba dawa za kulevya Jijini D’Salaam


Kulingana na utafiti uliofanywa na mwandishi wa makala hii katika vijiwe, baadhi ya vijana wamebuni utamaduni wa kufanya mazoezi ya kubeba dawa za kulevya tumboni kwa kumeza mbilimbi bila kutafuna, ili iwapo itatokea nafasi ya aina hiyo muda wowote, wawe tayari kuingia kazini. Uchunguzi uliofanywa maeneo ya Kinondoni, Magomeni, Vingunguti, Manzese, Msasani, na Temeke, umegundua zao la mbilimbi limekuwa likitumika kama kifaa cha kupima uwezo wa mbebaji wa dawa za kulevya. 

Na Mwandishi Wetu, Mwananchi

Posted  Ijumaa,Septemba13  2013  saa 12:28 PM
Kwa ufupi
Katika tukio la jana, raia wa Canada, Tabitha Leah Ritchie (28) amekamatwa nchini Colombia baada ya kujaribu kupanda ndege kurejea Canada akiwa na tumbo bandia la ujauzito alimokuwa ameficha dawa ya kulevya aina ya Cocaine.


Ni wazi kwamba vita vya kupambana na dawa za kulevya si ndogo, kwani kwa namna inavyoonekana ni kwamba wenye kujihusisha na biashara hiyo, licha ya baadhi kudaiwa kushirikiana na wafanyakazi wasio waaminifu katika vyombo vya ulinzi, wanabuni mbinu tofauti kukwepa mkono wa sheria.
Tatizo la dawa za kulevya ni la dunia nzima, sio Tanzania au Afrika tu, kuna raia wengi wa kigeni wamenaswa nchini Colombia mwaka huu wakiwa na dawa za kulevya.
Katika tukio la jana, raia wa Canada, Tabitha Leah Ritchie (28) amekamatwa nchini Colombia baada ya kujaribu kupanda ndege kurejea Canada akiwa na tumbo bandia la ujauzito alimokuwa ameficha dawa ya kulevya aina ya Cocaine.
Leah aliyekuwa anajifanya mtalii akirejea Toronto, alihojiwa na polisi katika uwanja wa ndege wa Bogota. Polisi alimshuku na kumuuliza alikuwa amesalia na miezi mingapi kujifungua.
Alijibu kwa ukali mno , hali iliyomfanya ofisa mmoja wa polisi kumtilia shaka zaidi na kuamua kumfanyia ukaguzi zaidi.
Ofisa huyo aligusa tumbo na kuhisi lilikuwa baridi mno na Ngumu sana, ndipo wakaamua kumkagua zaidi.
Walimkuta na dawa za kulevya zilizokuwa zimefungwa ndani ya tumbo hilo bandia ambalo mwanamke huyo alikuwa amelivaa kwa kufunga tumboni.
Inasemekana alisema ana miezi saba ya ujauzito lakini baada ya polisi kumkagua walimpata na Cocaine kilo mbili iliyokuwa ndani ya vipochi viwili
Leah atashtakiwa na huenda akafungwa jela kwa miaka mitano au minane.
Mwaka huu pekee karibu watu 150 wamekamatwa na dawa za kulevya katika uwanja wa ndege wa Bogota.
Karibu theluthi moja ya waliokamatwa walikuwa raia wa kigeni, kwa mujibu wa maofisa wakuu nchini Colombia.
Wakati hayo yakiendelea nje, hapa nchini inabainika kwamba kushamiri kwa biashara ya dawa za kulevya kumeleta utamaduni mpya katika baadhi ya vijiwe vya vijana jijini Dar es Salaam.

Kulingana na utafiti uliofanywa na mwandishi wa makala haya katika vijiwe, baadhi ya vijana wamebuni utamaduni wa kufanya mazoezi ya kubeba dawa za kulevya tumboni kwa kumeza mbilimbi bila kutafuna, ili iwapo itatokea nafasi ya aina hiyo muda wowote, wawe tayari kuingia kazini.
Uchunguzi uliofanywa maeneo ya Kinondoni, Magomeni, Vingunguti, Manzese, Msasani, na Temeke, umegundua zao la mbilimbi limekuwa likitumika kama kifaa cha kupima uwezo wa mbebaji wa dawa za kulevya.
Sababu kubwa ya kutumiwa kwa mbilimbi ni ukweli kwamba ukubwa wa kete za dawa za kulevya unakaribiana na ule wa zao hilo (mbilimbi).
Mwandishi alishuhudia vijana wakiwa katika makundi ya watu 10 hadi 15, kwa nyakati tofauti wakiwa natika vijiwe wakishindana kumeza mbilimbi bila kutafuna. Kuna baadhi walionekana kuwa na uwezo wa kumeza mpaka mbilimbi 30 kwa robo saa, huku wengine wakienda mbali zaidi ya hapo, japo wengine walionekana kushindwa.
Kwa mujibu wa maelezo yao ni kwamba ukifikia hatua hiyo, unapewa cheo cha Punda, jina linalomaanisha kuwa uko tayari kubeba mzigo na kusafirisha kwenda nchi yoyote utakayotumwa.
Kwa mujibu wa vijana hao, wale wanaoonekana kumeza mbilimbi hizo ndio huchukuliwa, na kutengenezewa pasi za kusafiria na kuendelea kupewa miongozo mingine. Kutokana na mazoezi hayo, inasemekana hata upatikanaji wa zao hilo ambalo mara nyingi hutumika kutengeneza chachandu, umeanza kuwa wa taabu hasa baada ya bei yake kupanda tofauti na awali.
Baadhi yao huwalazimu watumiaji kuagiza tunda hilo kutoka katika Mkoa wa Tanga, na wengine Mombasa, Kenya ambako hupatikana kwa wingi.
“Kwa Dar es salaam, Mbilimbi zinapatikana Kisutu tu kwa sasa na kwa baadhi ya watu ambao wamepanda miti labda uani kwao na sio kubwa kama zile ambazo tunatakiwa kumeza kwa hiyo inabidi sasa kuanza kuingia mikoani kuzisaka”, alisema mmoja wa vijana waliokutwa maeneo ya Feri, Dar es Salaam.
Inasemekana kutokana na uhaba wa matunda hayo ambayo hustawi sana katika mikoa ya Pwani, wakazi wengi wa Jijini Dar es Salaam wameanza kulima miti hiyo ndani ya uzio wa nyumba zao ili kuweza kuhudumia wateja wao kwa ukaribu.
Maeneo ya Magomeni Mikumi yanatajwa kuwa maarufu kwa zao hilo, wakazi wengi hasa kinamama wamekuwa wakipanda zao hilo ndani ya uzio wa nyumba zao na kulihudumia ipasavyo ili kupata matunda yenye ukubwa unaotakiwa kwa ajili ya matumizi ya vijana wanaofanya mazoezi ya kubeba mzigo. Hata hivyo si wote wanaopanda mbilimbi kwa ajili ya kujifanyia mazoezi ya dawa za kulevya.
SOURCE: MWANANCHI