Saturday 14 September 2013

VIWANDANI: Mkemia mkuu: Kemikali zilizoisha muda ni hatari



Na Beatrice Moses, Mwananchi,

Posted  Ijumaa,Septemba13  2013  saa 10:59 AM
Kwa ufupi
Wahusika hao ni pamoja na wamiliki wa viwanda mbalimbali vyenye maabara, shule zinazotumia kemikali katika masomo ya vitendo na hospitali.  


Huweza kusababisha madhara makubwa kwa viumbehai hususan binadamu, hasa zile zilizoisha muda wa matumizi.
Dar es Salaam. Mkemia Mkuu wa Serikali, Profesa Samwel Manyere, amewataka waliohifadhi kemikali zilizochakaa kujisalimisha na kutoa maelezo kwenye ofisi yake, ili kunusuru maisha ya watu na mazingira kwa jumla.
Akizungumza na gazeti hili jana, Profesa Manyere alisisitiza kuwa, kuna kemikali ambazo ni hatari kuendelea kuhifadhiwa kwa muda mrefu kwa kuwa licha ya kuharibu mazingira zinaweza kulipuka na kusababisha moto unaoweza kuchangia hasara ya mali na maisha pamoja na kuleta maafa.
Wahusika hao ni pamoja na wamiliki wa viwanda mbalimbali vyenye maabara, shule zinazotumia kemikali katika masomo ya vitendo na hospitali.  
“Kemikali zilizochakaa, zimetunzwa kwa muda mrefu ni hatari(sumu) kwa ardhi na maji ambayo yakitumiwa pia yanaweza kusababisha madhara kwa viumbe hai ikiwamo mimea na binadamu, hivyo tumewatumia barua wahusika ili watujulishe wamezitunza kwa muda gani,” alisema na kuongeza:
“Kwa kuwa tunaamini zipo ambazo hazina lebo pengine hata hazijulikani majina yake,tutazichunguza kwa umakini ili zinazotakiwa kuharibiwa ziharibiwe na zitakazofaa kwa somo la kemia tuweze kuzipeleka kwenye shule za sekondari zisaidie katika masomo ya vitendo,” alisema Profesa Manyere.
Wakati huo huo Mkemia Mkuu huyo alizungumzia kuhusu vibali vya uingizaji na usafirishaji wa tindikali kuwa mwisho wake ni Novemba 30,mwaka huu,hivyo wote wenye uhitaji wajisajili upya ili Serikali iweze kuwafuatilia kwa karibu baada ya matumizi yake kugeuzwa  silaha .
Alisema mwitikio wa kujisajili umepokewa vyema katika ofisi za kanda ikiwamo Arusha, Mwanza, Mbeya na Dar es Salaam tangu wito huo ulitolewa mapema Agosti mwaka huu.
SOURCE: MWANANCHI