Wednesday 25 September 2013

Mlinzi mkuu alipigwa risasi nane alipotaka kuwazuia magaidi


Na Boniface Meena

Posted  Jumanne,Septemba24  2013  saa 24:0 AM
Kwa ufupi
Eunice alisema aliutambua mwili wa mume wake alipofika katika Hospitali ya M.P SHAR ambako ndipo ulipohifadhiwa na kwamba wanafanya taratibu za kuusafirisha kwenda Kakamega kwa ajili ya mazishi.

Nairobi. Imeelezwa kuwa magaidi waliovamia jengo kubwa la maduka la Westgate jijini Nairobi, Kenya mwishoni mwa juma lililopita waliingia na magari matatu aina ya Nissan na kumuua mlinzi mkuu wa eneo hilo, Morris Adembesa kwa kumpiga risasi nane.
Akizungumzia tukio hilo kwenye Hospitali ya Aga Khan Nairobi, mke wa mlinzi huyo, Eunice Kavesa alisema ameuona mwili wa mumewe na kusema una matundu manane ya risasi alizopigwa na magaidi hao.
Alisema aliuawa baada ya walinzi wenzake kumwita getini ili kuzungumza na magaidi hao ambao walikuwa wamekataa kupekuliwa.
“Walikataa kukaguliwa ndipo walipomwita mume wangu ambaye ni mkuu wa ulinzi hapo na alipofika tu wakammiminia risasi nane hapohapo,” alisema mama huyo.
Alisema mume wake alihamishiwa katika kituo hicho akitokea Mombasa wiki moja iliyopita na siku mauti yalipomkuta ilikuwa ni siku yake ya nne tangu alipoanza kazi hapo.
Eunice alisema aliutambua mwili wa mume wake alipofika katika Hospitali ya M.P SHAR ambako ndipo ulipohifadhiwa na kwamba wanafanya taratibu za kuusafirisha kwenda Kakamega kwa ajili ya mazishi.
“Ameniachia watoto wawili niliozaa naye na yuko mwingine, maisha yatakuwa magumu kwa kuwa ninafanya kazi za kawaida tu na yeye ndiye aliyekuwa akitunza familia,” alisema Eunice.
Wakati akisema hayo mashambulizi yalikuwa yakiendelea katika eneo hilo la Westgate ambalo limezingirwa na vikosi mbalimbali vya usalama vya ndani na nje ya Kenya. Jana ilikuwa siku ya tatu tangu magaidi hao walipoliteka jengo hilo na kuua watu 62 huku wakiwajeruhi 175.

SOURCE: MWANANCHI